Selemani
 Jaffo, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi) akisikiliza 
maelezo kutoka kwa mama Abia Magembe kuhusu bidhaa zinazotokana na zao 
la muhogo. Kushoto kabisa ni Mratibu wa Mradi wa Green Voices kutoka 
Hispania, Alicia Cebada na kulia ni Mratibu wa mradi huo nchini 
Tanzania, Secelela Balisidya.
NAIBU 
Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Selemani 
Jaffo, amesema halmashauri zinawajibu wa kuunga mkono jitihada za 
utunzaji wa mazingira na kupambana na mabadiliko ya tabianchi.
Kutokana
 na hali hiyo, ameonya mtu yeyote asikwamishe jitihada zinazofanywa na 
akinamama washiriki wa mradi wa Green Voices Tanzania huku akiahidi kuwa
 serikali iko nao bega kwa bega. Alisema kwamba, endapo kuna mtu katika 
idara zilizo chini ya wizara yake atakwamisha jitihada zao, basi 
akinamama hao wawasiliane naye moja kwa moja.
Akizungumza
 wakati wa uzinduzi wa awamu ya pili ya mradi wa Green Voices nchini 
Tanzania uliofanyika kwenye Hoteli ya Golden Tulip jijini Dar es Salaam,
 Naibu Waziri Jaffo alisema kwamba, wizara yake ndiyo yenye jukumu kubwa
 la kuwawekea mazingira mazuri akinamama hao kutekeleza miradi yao chini
 ya halmashauri husika, hivyo akawaahidi kuwapatia ushirikiano wa 
kutosha kuhakikisha miradi hiyo inakuwa endelevu na suala la mazingira 
linapewa kipaumbele.
Mradi 
wa Green Voices unatekelezwa katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, 
Morogoro, Kigoma, Mwanza na Kilimanjaro, kukiwa na miradi 10 ikiwemo ya 
kilimo cha mihogo, kilimo cha matunda, uyoga, ufugaji wa nyuki, 
ukaushaji wa mbogamboga na utengenezaji wa majiko rafiki wa mazingira.
Bidhaa za mbogamboga zilizokaushwa kutoka Morogoro.
Akinamama walioanzisha miradi hiyo – miradi na mikoa watokayo vikiwa kwenye mabano –ni Regina Kamuli (Mkuranga, Pwani – Majiko Banifu), Abiah Magembe (Kisarawe, Pwani – Usindikaji wa Muhogo na Mtama), Magdalena Bukuku (Kinondoni, Dar es Salaam – Kilimo cha Uyoga), Mariam Bigambo (Dakawa, Morogoro – Ufugaji wa Nyuki), na Esther Muffui (Morogoro – Ukaushaji wa Mboga na Matunda).
Wengine ni Farida Makame (Kilimanjaro – Majiko ya Umeme-Jua), Leocadia Vedastus (Ukerewe, Mwanza – Kilimo na Usindikaji wa Viazi Lishe), Monica Kagya (Kisarawe, Pwani – Ufugaji wa Nyuki), Dkt. Sophia Mlote (Kinyerezi, Dar es Salaam – Kilimo Hai cha Nyanya na Mbogamboga), na Evelyn Kahembe (Uvinza, Kigoma – Kilimo cha Matunda).
Kupitia
 miradi hiyo, zaidi ya wanawake 300 wamepatiwa mafunzo mbalimbali huku 
program nyingine za mafunzo kwa vitendo zikiendelea katika makundi yao.
“Serikali
 ya Tanzania na hasa wizara hii, na wizara hii Mheshimiwa Rais mwenyewe 
ni wizara yake, naomba niwahakikishie kwamba tutashirikiana na Green 
Voices kwa nguvu zote na nitawapa pasiwedi ya kuwasiliana na ofisi yangu
 moja kwa moja ili kama mnakwama mambo yenu yaweze kwenda huko katika 
halmashauri mlipo,” alisema Jaffo, ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la 
Kisarawe mkoani Pwani. 
Akaongeza:
 “Nitawaunganisha na mkurugenzi maalum wa idara za serikali katika 
wizara yangu, kwamba ninyi mkikwama katika halmashauri kwa jambo lolote 
lile mnawasiliana naye  moja kwa moja mradi mambo yenu yaweze kwenda 
mpate sapoti, sauti ya wanawake iweze kusikika, mambo ya mazingira 
yaweze kubadilika, kilimo, mifugo na kadhalika ili mwisho wa siku watu 
waseme kwamba kuna kundi la watu walikwenda Hispania na wakajifunza 
wakaleta mabadiliko nchini.”
Aidha,
 Naibu Waziri Jaffo alisema kundi hilo la akinamama wa Green Voices ni 
muhimu na serikali itahakikisha inawaunga mkono kwa kila hali.
"Ninyi
 ni kioo cha jamii na watu wengi wanatakiwa wajifunze kutoka kwenu. 
Kumbukeni, katika suala la mazingira maeneo mengi yameathirika sana, 
mnaweza kuona jinsi maeneo mengi yanavyokumbwa na mafuriko kutokana na 
watu kukata miti na kuharibu mazingira, wakati mwingine tunashuhudia 
ukame wa kutisha. 
“Kwahiyo
 ninyi mradi wenu unakwenda kukabiliana na changamoto hizi, ni muhimu 
sana, mna wajibu mkubwa sana kwa sababu suala la mazingira ni muhimu na 
linaathiri dunia. 
“Tunatakiwa
 tutoke katika miradi isiyo halisi (artificial projects) na kwenda 
kwenye miradi halisi ili tuweze kubadilisha maisha ya watu.” 
Vile vile, aliwaasa akinamama hao kwamba, wakienda huko waongee lugha rahisi na wananchi ili iwe rahisi kueleweka. 
“Ninyi
 hapa wote ni wasomi, lakini mkienda huko ongeeni lugha rahisi ili 
mwananchi wakawaida akisikia aweze kuielewa na kuleta mabadiliko ya 
kweli. Mama mwingine hajasoma hata darasa moja na inawezekana kuwepo 
kwako wewe kukabadili maisha yake,” alisema.
Naibu Waziri wa Tamisemi, Selemani Jaffo, akizungumza katika uzinduzi huo. 
Secelela Balisidya akipokea cheti.
Mmoja 
wa washiriki wa mradi wa Green Voices, Mariam Bigambo, mkulima wa 
Mvomero ambaye amejikita katika ufugaji wa nyuki akiwa na kikundi cha 
wanawake 15, alisema kwamba licha ya umuhimu wa mradi huo, lakini 
wanakabiliwa na changamoto nyingi ambazo zinakwamisha maendeleo yao.
“Changamoto
 kubwa tunayokabiliana nayo ni kushushwa kwa mizinga yetu na watu 
wasiojulikana kwa sababu tumeiweka porini,” alisema na kuongeza: “Kila 
mara tunakuta mizinga yetu imeshushwa, tumekwishatoa taarifa kwa 
serikali ya kijiji pamoja na kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya 
Mvomero na hata Polisi.”
Aidha,
 alisema kwamba, ufugaji wa nyuki unahitaji uvumilivu na mpaka sasa 
baadhi ya wanakikundi wamevunjika moyo kwa sababu bado hawajanufaika na 
matunda ya kazi yao. Kutokana na hali hiyo, alisema, wameamua pia 
kugeukia kilimo cha uyoga ili kuongeza tija.
Mratibu
 wa mradi wa Green Voices nchini Tanzania, Secelela Balisidya, alisema 
awamu ya kwanza ya mradi huo ililenga katika uanzishwaji na uzalishaji, 
lakini awamu ya pili inalenga kuwapatia stadi akinamama ili kuboresha 
bidhaa wanazozizalisha ili ziongezeke ubora la kuwaletea tija.
“Hivi 
sasa katika awamu ya pili akinamama watapatiwa mafunzo ya namna ya 
kutengeneza bidhaa zao kama vifungashio ili kuongeza ubora na thamani na
 tunataka bidhaa zao ziingie sokoni katika viwango ambavyo 
vinakubalika,” alisisitiza.
Akizungumza
 katika uzinduzi huo wa awamu ya pili, Mratibu wa mradi wa Green Voices 
kutoka Hispania kutoka taasisi ya Women for Africa Foundation 
inayodhamini mradi huo, Alicia Cebada, alisema wamefarijika na mradi huo kwa kuwa umeonyesha mafanikio makubwa nchini Tanzania katika awamu ya kwanza na ndiyo maana wameamua kuwaongezea uwezo akinamama hao katika awamu hii.
“Tumekuwa
 tukiwasiliana mara kwa mara na Secelela (Mratibu wa Green Voices 
Tanzania) kuhusu mafanikio na changamoto za mradi huu na kwa kweli 
tunafarijika kuona miradi yote inakwenda vizuri,” alisema Alicia.
Alisema,
 changamoto pekee ambayo ipo mbele yao ni kuhakikisha miradi hiyo 
inasimama na kuwafundisha wanawake wengi kadiri wawezavyo ili 
kuhakikisha wanajiletea maendeleo katika maeneo yao kiuchumi na kijamii.
Mwaka 
2016 rais wa mfuko wa Women for Africa Foundation, Mama Maria Tereza 
Fernandez de la Vega, alizuru nchini Tanzania na kushiriki uzinduzi wa 
mradi huo Julai 11, 2016 ambapo ulizinduliwa rasmi na Makamu wa Rais wa 
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan.
Katika
 uzinduzi huo, Mama Samia aliahidi kwamba serikali yake itahakikisha 
inakuwa bega kwa bega kusaidia miradi hiyo iwe endelevu ili kuunga mkono
 juhudi za utunzaji wa mazingira na kupambana na mabadiliko ya 
tabianchi, kuongeza uhakika wa chakula, kuwakwamua wananchi na umaskini 
pamoja na kuongeza ajira, hasa kwa wanawake.
Kwa 
upande wake, Mama Maria Tereza, ambaye ni makamu wa rais mstaafu wa 
Hispania, alieleza kufurahishwa kwake na jitihada za akinamama wa 
Tanzania na kusema taasisi yake inaangalia namna ya kuwasaidia zaidi.
Mratibu
 wa Mradi wa Green Voices kutoka Hispania, Alicia Cedaba (kushoto) akiwa
 na Leocadia Vedasto kutoka Ukerewe anayeratibu kilimo cha viazi lishe 
pamoja na usindikaji wa bidhaa zake. Katikati ni mdau mwingine 
aliyehudhuria uzinduzi wa awamu ya pili ya Mradi wa Green Voices 
Tanzania.





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni