WAZIRI MKUU WA ETHIOPIA AMALIZA ZIARA NCHINI TANZANIA

Waziri Mkuu wa Shirikisho la Jamhuri ya Kidemokrasi ya Ethiopia Mhe. Hailemariam Dessalegn ameondoka nchini leo kurejea nchini mwake Ethiopia baada ya kumaliza ziara yake rasmi ya kiserikali hapa nchini aliyoifanya kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli.

Katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Mhe. Hailemariam Dessalegn ameagwa na mwenyeji wake Mhe. Rais Magufuli aliyeongozana na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.


Akiwa nchini Mhe. Hailemariam Dessalegn amefanya mazungumzo na mwenyeji wake Mhe. Rais Magufuli Ikulu Jijini Dar es Salaam, amehudhuria dhifa ya kitaifa iliyoandaliwa na Mhe. Dkt. Magufuli kwa heshima yake na leo asubuhi ametembelea bandari ya Dar es Salaam ambapo amesema nchi yake ipo tayari kuitumia bandari hiyo sambamba na kuanzisha kituo cha huduma za usafirishaji wa mizigo kwa ndege (Cargo Hub) katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere kupitia shirika lake la ndege la Ethiopia Airline.


Emmanuel Buhohela
Kaimu Mwandishi wa Habari wa Rais Msaidizi

Dar es Salaam

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni