BALOZI SEIF AKAGUA BANDARI YA MKOANI ZANZIBAR


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Katikati akiambatana na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bandari Zanzibar Nd. Abdulla Juma kushoto yake akikagua Bandari ya Mkoani inayokusudiwa kutoa huduma za Kimataifa.

Balozi Seif kati kati akiwa pamoja na Mkuu waMkoa Kusini Pemba wakiangalia mandhari ya Bandari ya Mkoani Kisiwani Pemba akimalizia ziara yake ya siku Tatu Kisiwani Pemba.

Balozi Seif akitembezwa katika eneo linalotarajiwakujengwa kwa ajili ya uwekwaji wa makontena pembezoni mwa Bandari ya Mkoani Kisiwani Pemba.
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seifa akiambatana na Uongozi wa Hospitali ya Abdulla Mzee Mkoani kukagua shughuli za huduma za Afya zinazotolewa katika Hospiytali hiyo. 
Balozi Seif akiagiza uwajibikaji uliobora kwawafanyakazi wa Hospiali ya Abdulla Mzee alipokagua Kitengo cha X RAY.

Balozi Seif akionyesha kufarajika kwake na huduma zauchunguzi wa Maabara zinazotolewa na Hospitali ya Abdulla Mzee wakati alipokagua kitengo cha Maabara Hospitalini hapo.


Daktari Mkuu wa Hospitali ya Abdulla Mzee MkoaniDr. Haji Mwita Haji akielezea changamoto wanazopambana nazo watendaji wa Hospitali hiyo wakati wanapotoa huduma za Afya kwa Wananchi.Picha na – OMPR – ZNZ.

Shirika la Bandari Zanzibar limejipanga kuimarisha miundombinu yake
katika kuona Bandari ya Mkoani Kisiwani Pemba inatoa huduma zinazokidhi kiwango cha Kimataifa.

Mamlaka ya Mapato Tanzania { TRA } tayari imeshatoa idhini na kutangaza kwamba Bandari ya Mkoani Pemba inaweza kutoa huduma za Kimataifa ikiwemo shughuli za kupokea na kusafirisha Makontena kutokana na kukuwa kwa biashara katika Kisiwa hicho.

Msaidizi Mkurugenzi wa Shirika la Bandari Tawi la Pemba Nd. Hamad Salum alieleza hayo wakati Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar balozi  Seif alipofanya ziara ya kukagua shughuli za Bandari hiyo akimalizia ziara yake ya siku Tatu Kisiwani Pemba.

Ndugu Hamad alisema Uongozi wa Shirika la Bandari tayari umeshaanza
hatua ya kufanya maboresho ya Baboya, Umeme pamoja na huduma za Maji
safi na salama yaliyokwenda sambamba na Ununuzi wa Krini ya Kuteremshia Vitu vizito Bandarini.

Alisema hatua hiyo imekuja baada ya kukamilika kwa Utafiti wa Kitaalamu wa kuiangalia upya Banadari hiyo uliofanywa mwaka 2016 kwa lengo la kuunga mkono maamuzi ya Mamlaka ya Mapato Tanzania. Msaidizi Mkurugenzi huyo wa Shirika la Bandari Tawi la Pemba alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba Bandari ya Mkoani hivi sasa inaendelea kupokea Meli za mizigo na Abiria kutoka Unguja na Mombasa Nchini Kenya.

Alisema kwa sasa Bandari hiyo imeshapokea meli zenye uwezo wa kubeba
Tani 200 kutoka Unguja na Makontena 300 yenye ujazo wa Tani 300 kutoka
Pemba licha ya kwamba bado wapo baadhi ya Wafanyabiashara wenye
kigugumizi cha kuteremsha makontena yao moja kwa moja kutoka nje ya
Zanzibar.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bandari Zanzibar Nd. Abdulla Juma
alisema kwa Vile Shirika lake tayari limeshanunua Krini Moja ya kuteremshia Mizigo, uwezo wa kushusha makontena ya wafanyabiashara katika Bandari ya Mkoani upo na kinachohitajika kwa sasa ni kuona Mizigo ya Wafanyabiashara kutoka Nje ya Zanzibar inakwenda Pemba moja kwa moja badala ya kupitia kisiwani Unguja na Mombasa Nchini Kenya.

Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alisema wazo la Uongozi wa Shirika hilo la Bandari kuimarisha Bandari ya Mkoani ni jema na la msingi kwa sababu litasaidia kufungua njia zaidi za Kibiashara kati ya Visiwa vya Zanzibar na Mataifa mengine Duniani.

Balozi Seif alisema shughuli za Bandari ni miongoni mwa maeneo ambayo
Serikali Kuu inategemea kuongeza Mapato yake sambamba na kupanuka kwa
fursa za ajira zitakazowanufaisha Wananchi Wazalendo hasa Vijana.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliuagiza Uongozi wa Shirika la Bandari na washirika wake vikiwemo vyombo vya Ulinzi kuhakikisha kwamba udhibiti wa uingiaji na utokaji katika maeneo ya Bandari unaimarishwa ipasavyo.

Alisema wapo baadhi ya watu hutumia harakati za wasafiri kuingiza mambo yao ikiwemo usafirishaji wa bidhaa haramu lakini pia uingiaji wa wageni wasiozingatia sheria na utaratibu uliowekwa na Taifa wa Uhamiaji.

Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alitembelea Hospitali ya Rufaa ya Abdulla Mzee iliyopo Mkoani Mkoa wa Kusini Pemba kuangalia huduma za Afya zinazotolewa na watendaji wa Hospitali hiyo.

Daktari Mkuu wa Hospitali ya Abdulla Mzee Dr. Haji Mwita Haji alimueleza Balozi Seif kwamba mazingira bora ya miundombinu ya Vifaa, Majengo na watendaji yamepelekea Wananchi wa Kisiwa cha Pemba kuwa kimbilio la kutaka kupata huduma za Afya.

Hata hivyo Dr. Haji Mwita alisema zipo changamoto zinazoikabili Hospitali hiyo pamoja na Watendaji wake akazitaja baadhi kuwa ni pamoja na umbali wa Makaazi ya watendaji hao jambo ambalo linaleta usumbufu wakati inapoteka uchelewaji wa usafiri.

Dr. Mwita alizitaja changamoto nyengine kuwa ni uhaba wa Dawa, huduma
za umeme wa dharura, ongezeko la wagonjwa pamoja na utaalamu mdogo wa
watendaji wake kwa baadhi ya amashine za Kisasa zilizomo ndani ya Hospitali hiyo na kushairi kuandaliwa mpango maalum wa kupatiwa mafunzo.

Akizungumza na baadhi ya Madaktari na watendaji wa Hospitali hiyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Madaktari na Wauguzi wa Hospitali hiyo wanalazimika kuwajibika ipasavyo ili hadhi ya Hospitali hiyo iendelee kubakia.

Balozi Seif alisema mfumo huo wa uwajibikaji ulioambatana na vifaa vipya na vya kisasa unaweza kushawishi wagonjwa kutoka nje ya Visiwa vya Zanzibar kutaka kupatiwa huduma za Afya kwenye Hospitali hiyo ya Abdulla Mzee Mkoani.

Alielezea masikitiko yake kutokana na Hospitali nyingi nchini kulalamikiwa kutokana na huduma zake hawa wakiguswa zaidi Wauguzi kutokana na kauli zao za kuwavunja moyo wagonjwa wanaokwenda kutaka kupatiwa huduma za Afya.

Akizungumzia Makaazi ya Madaktari wa Hospitali hiyo Makamu wa Pili wa
Rais wa Zanzibar alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tayari imeshaamua kujenga nyumba Nne za Ghorofa kwa nia ya kuondosha tatizo
hilo.

Alisema Serikali kupitia Wizara ya Afya imeshazungumza na Kampuni iliyojenga Hospitali hiyo kwa ajili ya kuangalia uwezekano wa kujenga
Nyumba hizo ili kupunguza gharama za kumtafuta mkandarasi mwengine wa
ujenzi huo wakati utakapowadia.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar katika nasaha zake kwa watendaji
hao wa Hospitali ya Rufaa ya Abdulla Mzee Mkoani Pemba alisema Serikali isingependa kuona huduma za afya zinazotolewa kwenye Hositali
hiyo zinaambatana na ushabiki wa Kisiasa.

Balozi Seif alisema Hospitali ni sehemu ya huduma inayompasa mwananchi
ye yote mwenye matatizo ya kiafya anapatiwa huduma zinazostahiki bila
ya ubaguzi wala itikadi za kisiasa.

Alionya kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haitamvumilia mtendaji ye yote wa Sekta ya Afya atakayeonekana ana tabia hiyo ya kushabikia masuala ya Kisiasa.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
301/2017.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni