Ajisalimia Polisi Baada Ya Mahindi Aliyoiba Kunasa Mabegani

Kijana  Frank Japhet (23), mkazi wa Mbezi, Dar es Salaam, amelazimika kujisalimisha katika Kituo cha Polisi Mlandizi, Kibaha, Pwani, baada ya mzigo wa mahindi unaokadiriwa kuwa na uzito wa kilogramu 20, anaodaiwa kuuiba kung’ang’ania mabegani.
Wakati akihojiwa kituoni hapo, mtuhumuwa huyo amesema mzigo huo, uliofungwa kwenye kiroba aliuiba kwa mama mmoja eneo la Mtaa wa Nyambwiro, Mlandizi, Kibaha, mkoani Pwani majira ya saa 7.00 usiku wa kuamkia leo Mei 3, 2018, akaongeza kwamba aliondoka na mzigo huo hadi eneo la Stendi ya Mlandizi alipokuwa auache kwa mwenzake ili arudie mzigo mwingine, ambapo mzigo huo uling’ang’ania kichwani.
Ameendelea kusema kwamba alijitahidi kufanya kila aliloweza ili mzigo huo utoke kichwani ikiwa ni pamoja na kulala ili akinyanyuka ubaki chini lakini aliponyanyuka, alinyanyuka nao kichwani! Baada ya kuzunguka nao kwa muda mrefu, alidai alichoka hivyo akalazimika kujisalimisha polisi ili asije akauawa na raia wenye hasira watakapobaini kuwa ni mwizi.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Pwani Jonathan Shanna  amesema walilazimika kumtafuta mhusika wa mzigo huo ili kuweza kumsaidia kijana Frank Joseph ambaye aliiba kiroba hicho, baada ya wao kushindwa kumtua.
Kamanda Shanna ameendelea kusimulia kuwa wakati wakijaribu kumtua kijana huyo kiroba cha mahindi alichoiba alikuwa akilalamika kupata maumivu makali, na ndipo wakamsaka mmiliki wa mzigo ili kumsaidia.  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni