Na: Mahmoud Ahmad, Dodoma.
Serikali imesema kuwa pamoja na 
huduma za bidhaa ya fedha kuamuliwa na nguvu ya soko  kwa upande wake 
imekuwa ikichua hatua za kisera ili kuhakikisha kuwa riba za mikopo 
zinapungua katika soko hapa nchini.
Hayo yameelezwa leo Bungeni Jijini
 Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Ashatu Kijaji 
alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Konde, Mhe. Khatibu Haji juu ya 
Serikali inachukua hatua gani ili benki ziweze kupunguza viwango hivyo 
vya riba?
“Baadhi ya hatua zilizochukuliwa 
na Serikali kupitia Benki Kuu ni pamoja na kuzitaka benki za biashara 
kutumia mfumo wa kuhifadhi na kutoa taarifa za wakopaji (Credit 
Reference Bureau System). Aidha, Benki hiyo imekuwa ikitoa mikopo ya 
muda mfupi kwa benki za biashara kwa kiwango cha asilimia 6.89,” amesema
 Dkt. Kijaji.
Dkt. Kijaji amezitaja hatua 
nyingine zilizochukuliwa kuwa ni Benki Kuu kushusha riba (Discount Rate)
 kutoka asilimia 16.0 hadi asilimia 9.0 pamoja na kupunguza kiwango cha 
chini cha amana kinachotakiwa kuwekwa Benki Kuu na benki za biashara 
(Statutory Minimum Reserve Requirememnt (SMR)) kutoka asilimia 10.0 hadi
 asilimia 8.0.
Vile vile Serikali imeendelea 
kulipa malimbikizo ya madai yaliyohakikiwa kwa lengo la kupunguza 
kiwango cha mikopo chechefu na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi.
Aidha, amesema baada ya hatua hizo
 za kisera kuchukuliwa na Serikali, baadhi ya benki za biashara hapa 
nchini zimeanza kupunguza riba za mikopo.
Ameongeza kuwa, Serikali 
itaendelea kuchukua hatua za kisera ili kuhakikisha kuwa riba za mikopo 
katika soko zinaendelea kupungua.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni