Meneja wa kinu cha kuchenjua dhahabu wa Mgodi wa Buzwagi Festo Shayo 
(wa kwanza kulia) akitoa maelezo kwa Naibu waziri ofisi ya makamu wa 
rais anaeshughulikia mazingira na Muungano, Luhaga Mpina namna mgodi 
wake unavyohifadhi maji yaliyotumika kusafishia dhahabu.
Naibu 
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Luhaga 
Mpina, ameupongeza Uongozi na wafanyakazi wa Mgodi wa Buzwagi kwa 
kuzingatia sheria za mazingira Mgodini hapo.
Pongezi
 hizo alizitoa wakati alipofanya ziara ya kushitukiza katika Mgodi huo 
kwa lengo la kujionea namna mwekezaji huyo anavyozingatia maelekezo ya 
wataalamu wa wizara yake juu ya utunzaji wa mazingira.
Akiwa 
katika ziara hiyo Naibu Waziri huyo alitembelea bwawa maalumu kwa ajili 
ya kuhifadhia maji yalitumika kuchenjulia dhahabu na kujionea namna 
ambavyo mgodi huo unavyochukua tahadhari ya hali ya juu katika 
kuhakikisha maji yanayohifadhiwa ndani ya bwawa hilo hayawezi kuwa na 
madhara kwa Jamii, pia naibu Waziri huyo alitembelea kituo cha udhibiti 
taka, Uwanda wa kuvuna maji ya mvua mgodini hapo pamoja na karakana ya 
mgodi huo.
Naibu 
Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira na Muungano Luaga Mpina (wa 
kwanza kushoto), akisikiliza maelezo ya Afisa Mazingira wa Mgodi wa 
Buzwagi bwana Frank Ngoroma (wa kwanza mkono wa kulia), aliyesimama 
katikati ni meneja mkuu wa mgodi wa Buzwagi Mhandisi Asa Mwaipopo.
“Bwawa
 hili kama unavyoliona usanifu wake, umezingatia tahadhari zote 
kuhakikisha hakuna maji yoyote yanatoka nje na hasa ukizingatia maji 
yanayopatikana hapa ni yenye mchanganyiko wa madawa yanayotumika 
kuchenjua dhahabu” Alisema Meneja wa Kituo cha Uchenjuaji dhahabu bwana 
Festo Shayo, wakati alipokuwa akitoa maelezo juu bwawa hilo.
Kwa 
upande wake naibu Waziri Mpina amesema licha ya kufanya ziara katika 
Migodi mingi bwawa la kuhifadhia maji yanayotoka katika kinu cha 
kuchenjulia dhahabu la Buzwagi ni la kiwango cha juu na ameitaka Migodi 
mingine pia kutembelea kwa lengo la kujifunza usanifu wake.
“Ni 
seme tumepita maeneo mengi ila hapa mmejitahidi kuhakikisha wananchi 
wanaowazunguka wako salama, nafikiri kuna haja ya migodi mingine kuja 
kujifunza hapa, karakana yenu pia ni nzuri na inazingatia utunzaji wa 
mazingira. Alisema mh Mpina.
Naibu 
Waziri pamoja na wataalamu wake wakikagua moja ya maeneo ambayo NEMC 
yalitoa ushauri kuwa yafanyiwe kazi katika ziara zao, ambapo wakati wa 
ziara hii utekelezwaji wake ulikutwa umeisha kamilika kama walivyokuwa 
wameelekezwa.
Aidha 
akiwa katika kituo maalumu cha udhibiti taka Mgodini hapo Naibu Waziri 
huyo ameutaka uongozi kujenga paa kwenye eneo la udhibiti wa taka za 
vyuma ili kuzuia maji ya mvua kugusa taka hizo.
“Mmejitahidi
 kuhakikisha taka zinawekwa katika utaratibu mzuri, ila kukosekana kwa 
paa hapa ni tatizo, hivyo nawaagiza ndani ya siku therathini eneo hili 
liwe na paa” alisema Naibu Waziri Mpina.
Awali 
akiukaribisha ugeni wa naibu Waziri huyo Meneja Mkuu wa Mgodi wa Buzwagi
 Mhandisi Asa Mwaipopo alimueleza naibu Waziri huyo kuwa sekta ya madini
 kwa sasa duniani imekumbwa na changamoto ya kuporomoka kwa bei ya 
dhahabu, hali ambayo imepelekea wawekezaji wengi kujikuta wakijiendesha 
kwa hasara.
“Mheshimiwa
 naibu Waziri, Mgodi wa Buzwagi toka uanze shughuli zake umekuwa 
ukishirikiana na Jamii katika kutekeleza miradi mbalimbali ya Maendeleo 
na tunaendelea kufanya hivyo, Hata hivyo changamoto ni kubwa kwani kila 
siku bei ya dhahabu inashuka na hii inatufanya tushindwe kujiendesha kwa
 faida”alisema Mwaipopo.
“Tumeanza
 mchakato wa maandalizi ya kusitisha shughuli za uchimbali maana gharama
 zinazidi kuwa kubwa hata hivyo kama bei ya soko itabadilika tutafikiria
 vinginevyo” aliongeza Mwaipopo.
Akizungumzia
 hatua ya mgodi huo kutaka kusitisha shughuli za uchimbaji naibu Waziri 
Waziri ofisi ya makamu wa rais anaeshughulikia mazingira na muungano 
Luaga Mpina, amewaomba wawekezaji hao kuangalia namna ingine 
itakayowawezesha kuchimba kwa gharama ndogo inayoendana na bei ya 
dhahabu.
“kwa 
kweli serikali inawahitaji sana wawekezaji na tunaposikia mnaondoka 
kwetu sisi ni hasara kwa sababu kodi mbalimbali ambazo mmekuwa mkilipa 
kwa halmashauri ya mji wa Kahama hazitakuwepo tena na hii itafanya 
miradi mingi ya Maendeleo isitekelezeke baada ya ninyi kuondoka, 
tunawaombea bei ya dhahabu ipande ili muendelee kuwepo” Alisema Mpina.
Ziara 
hiyo ya kushitukiza ili lenga kujionea namna ambavyo mgodi wa Buzwagi 
unazingatia maelekezo mbalimbali ya wataalamu wa wizara yake.
Mh Luhaga Mpina akisisitiza jambo wakati wa ziara hiyo katika eneo la kituo cha Uthibiti wa taka mbalimbali mgodini hapo.
Mmoja wa maafisa wa mazingira aliyekuwa ameandamana na naibu Waziri akiuliza jambo wakati wa ziara hiyo.
 Meneja Mkuu wa Mgodi wa Buzwagi Mhandisi Asa Mwaipopo akifafanua jambo wakati wa ugeni wa naibu Waziri wa mazingira. 
Baadhi
 ya maofisa wa Mgodi wa Buzwagi wakitoa maelezo mbele ya Naibu Waziri 
Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira na Muungano Luaga Mpina 
Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa wa Shinyanga.
Na Dixon Busagaga wa Globu ya Jamii Kanda ya Kaskazini.








Hakuna maoni:
Chapisha Maoni