Na Benny Mwaipaja, WFM, Dodoma 
Rais
 wa Benki ya Maendeleo ya Afrika-AfDB, Dkt. Akinumwi Adesina, amemaliza 
ziara yake ya siku tatu nchini na kuahidi kuwa atahakikisha Tanzania 
inaendelea kunufaika na misaada na mikopo yenye masharti nafuu kutoka 
Benki hiyo kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya kisasa katika Jiji la 
Dodoma na mradi wa kuzalisha umeme wa Stieglers Gorge. 
Akiwa
 katika uwanja wa ndege Jijini Dodoma, Dkt. Adesina amemmwagia sifa Rais
 Dkt. John Pombe Magufuli kwa namna anavyosimamia ukuaji wa uchumi 
uliofikia wastani wa asilimia 7 kwa mwaka pamoja na kupambana na vitendo
 vya ufisadi, rushwa, kuimarisha uwajibikaji wa viongozi kwa wananchi, 
kupiga vita matumizi mabaya ya rasilimali za umma ili kuwaondoa wananchi
 wake katika umasikini. 
Dkt.
 Adesina amesema kwa kutambua mchango huo pamoja na umahili wa Waziri wa
 Fedfha na mipango Dkt. Philip Mpango, wa kusimamia uchumi na sera ya 
bajeti na fedha, benki yake itaendelea kuwekeza kiasi kikubwa cha fedha 
ili nchi iweze kupiga hatua kubwa kupitia miundombinu mbalimbali 
inayotekelezwa kupitia benki yake na washirika wengine wa maendeleo. 
Miongoni
 mwa miradi ambayo Benki hiyo imepanga kusaidia ni ujenzi wa Uwanja wa 
Ndege wa Kimataifa utakaojengwa katika eneo la Msalato, nje kidogo ya 
Jiji la Dodoma ambapo kwa kuanzia benki hiyo itatoa zaidi ya shilingi 
bilioni 200. 
“Tumekuwa
 na majadiliano ya kina na Mhe. Rais Dkt. John Magufuli kuhusu mradi wa 
kuzalisha umeme wa Stieglers Gorge ambao utazalisha Kw 2100, Benki yetu 
itaangalia namna ya kutoa fedha kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa mradi 
huo mkubwa” alisema Dkt. Adesina. 
Alisema
 kuwa suala la mapinduzi ya viwanda haliwezi kufanikiwa bila kuwa na 
nishati ya umeme ya uhakika na kwamba benki yake itawekeza dola za 
Marekani bilioni 1.5 kwa ajili ya sekta ya nishati na itaongeza kiasi 
kingine cha dola milioni 950 kwa ajili ya kazi hiyo. 
“Mwaka
 huu tutatoa fedha kwa ajili ya kuboresha nishati ya umeme katika ukanda
 wa Kaskazini Magharibi mwa Tanzania na tuna mpango pia wa kuboresha 
Shirika la Ugavi wa Umeme hapa nchini-TANESCO, ili liweze kuzalisha 
umeme wa uhakika na wenye gharama nafuu kwa ajili ya kuendeleza mpango 
wa Serikali wa kuwa na uchumi wa viwanda” aliongeza Dkt. Adesina 
Kwa
 upande wake, Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, ameelezea 
kufurahishwa na ujio wa Rais huyo wa Benki ya Maendeleo ya Afrika-AfDB, 
Dkt. Akinumwi Adesina, na kwamba ujio huo umeleta neema kwa nchi baada 
ya benki hiyo kuahidi kutoa shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kujenga 
Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato pamoja na kuahidi kutoa fedha 
kwa ajili ya kujenga barabara za mchepuko (mzunguko) Jijini Dodoma. 
Dkt.
 Mpango amewataka watanzania kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali 
za kuwaletea maendeleo na watembee kifua mbele kwa kuwa hivi sasa 
Tanzania imeshika nafasi ya pili katika Bara la Afrika kwa ukuaji wa 
uchumi kwa kasi ikitanguliwa na nchi ya Ethiopia, na Rais Adesina 
amelisemea vizuri jambo hilo. 
Ushirikiano
 wa Benki ya Maendeleo ya Afrika-AfDB na Tanzania ulianza tangu mwaka 
1971, ambapo mpaka sasa benki hiyo imewekeza kiasi cha dola bilioni 3.6,
 sawa na zaidi ya shilingi trilion 8, katika miradi mbalimbali ya 
kiuchumi ikiwemo umeme, barabara, maji na usafi wa mazingira, uboreshaji
 rasilimali watu pamoja na masuala ya utawala bora.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni