ZANZIBAR YASHAURIWA KUANZA KUTENGENEZA BARABARA KWA KUTUMIA MADINI MAALUM


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif kati kati aliyevaa Kofia ya Kiua akizungumza na Uongozi wa Kampuni ya Kimataifa ya utengenezaji wa Madini ya Margania yanayotumika katika utengenezaji wa Bara bara kutoka Nchini Uturuki Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
Mratibu Mkuu wa Kampuni ya Kimataifa ya utengenezaji wa Madini ya Margania kutoka Nchini Uturuki Bwana Ahmet Nesih ONAL kati kati akitoa maelezo kwa Balozi Seif ya Utengenezaji wa Bara bara kwa kutumia Madini ya Margania.
Bwana Ahmet Nesih akifafanua jambo wakati wa maelezo yake mbele ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi.
Bwana Mohamed wa Kampuni ya Kimataifa ya utengenezaji wa Madini ya Margania Tawi la Tanzania liliopo Dar es salaam akifafanua jambo juu ya Teknolojia hiyo ya Kisasa. Picha na – OMPR – ZNZ.

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshauriwa kuangalia uwezekano wa kutumia Teknolojia Mpya ya utengenezaji wa Bara bara kwa kutumia madini maalum ambayo uchanganyaji wake baadae unageuka kuwa zege linaloweza kudumu kwa miaka mingi.

Ushauri huo umetolewa na Mratibu Mkuu wa Kampuni ya Kimataifa ya utengenezaji wa Madini ya Margania kutoka Nchini Uturuki Bwana Ahmet Nesih ONAL wakati wa mazungumzo yake na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Vuga Mjini Zanzibar.

Bwana Ahmet Nesih alisema Bara bara mbali mbali zinazotengenezwa kwa kutumia Maadini ya Margania zinaipunguzia Serikali gharama Kubwa ya Fedha sambamba na matumizi mengi ya Vifaa wakati wa ujenzi wa miundombinu hiyo kwa ajili ya mawasiliano ya usafiri Mijini na Vijijini.

Mratibu Mkuu huyo wa Kampuni ya Kimataifa ya utengenezaji wa Madini ya Margania alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba Uongozi wa Kampuni yake umeshuhudia ujenzi wa Bara bara nyingi katika maeneo mbali mbali Duniani zinazotumia mfumo wa Lami ambao unaweza kuepukwa kwa kupungua matumizi.

Alisema yapo baadhi ya Mataifa Ulimwenguni kama Qatar, Kuweit, Saudi Arabia na Iraq zilizoanza kutumia Teknolojia hiyo ya Madini ya Margania na kufanikiwa kupunguza gharama kubwa.

Akitoa Shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Zanzibar ni miongoni mwa Nchi kadhaa Duniani zinazoendelea kujikwamua Kiuchumi kwa kujenga Miundombinu kadhaa ikiwemo ile bara bara ambayo hurahisisha mfumo wa Mawasiliano.

Balozi Seif aliuomba Uongozi wa Kampuni hiyo ya utengenezaji wa Madini ya Margania ya Nchini Uturuki kuandaa Mpango Maalum utakaowawezesha Wahandisi wa Sekta ya Mawasiliano Zanzibar kuiona Teknolojia hiyo na kuangalia mazingira ya Zanzibar iwapo inaweza kutumika.

Alisema licha ya juhudi kubwa zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya uimarishaji wa Miundombinu ya Bara bara lakini bado zipo baadhi ya Bara bara Mjini na Vijijini zinahitaji kuimarishwa kwa kutumia Teknolojia itakayoziwezesha zidumu kwa kipindi kirefu.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
11/4/2018.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni