Wasichana yenye umri mdogo wametakiwa kuacha tabia ya kujihusisha 
na vitendo vya ngono katika umri mdogo kwani wanajiweka kwenye hatari 
kubwa ya kupata maambukizi ya magonjwa hatari ikiwemo Saratani ya mlango
 wa kizazi pampja na gonjwa hatari la UKIMWI. 
Rai hiyo imetolewa na Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, na mkuu wa 
wilaya ya Monduli Mhe. Idd Kimanta wakati wa uzinduzi wa chanjo mpya ya 
Saratani ya Mlango wa Kizazi katika halmashauri ya Arusha, uliofanyika 
kwenye hospitali ya wilaya ya Olturumet.
Mkuu wa wilaya huyo amewaasa wasichana kuacha tabia ya kujihusisha na
 vitendo vya ngono, licha ya kupata kinga ya Saratani ya Mlango wa 
Kizazi  na kuongeza kuwa chanjo hiyo haizuii kupata maambukizi ya 
magonjwa mengine yanayoombukizwa kwa njia ya kujamiiana.
Amefafanua kuwa, vitendo vya ngono katika umri mdogo vinachangia sana
 kukatisha ndoto za wasichana wengi na wakati mwingine husababisha 
wasichana wengine kupoteza maisha.
Hata hivyo Kimanta amewataka wazazi, walezi na jamii nzima 
kuhakikisha wasichana wenye umri wa miaka 14, wanakwenda kupata chanjo 
hiyo huku akiwataka viongozi wa kata zote kusimamia zoezi hili kwa 
ufasaha na kuhakikisha hakuna mtoto atakayekosa chanjo hiyo pamoja na 
kuwaonya watu watakaokwamisha zoezi hilo kuchukuliwa hatua kali za 
kisheria. 
Naya mratibu wa chanjo halmashauri ya Arusha Dkt. Yassin  Winga , 
amesema kuwa halmashauri inategemea kuwapatia chanjo jumla ya wasichana 
4,239 itakayotolewa kwenye vituo 50 vilivyopo kwenye vituo vya kutolea 
huduma za afya   ndani ya halmashauri na zoezi litafanyika ndani ya wiki
 nzima.
Dkt. Winga amefafanua kuwa, zoezi la chanjo litatolewa pia kwa 
kutumia 'Mobile Clinic' kwa wakazi wa maeneo ya pembezoni na kusema kuwa
 chanjo hii itatolewa mara mbili na mara tatu kwa wasichana wenye 
maambukizi ya VVU ndani ya miezi sita.
Aidha baadhi ya wanafunzi waliofika kituoni hapo na kupatiwa chanjo 
hiyo, wamekiri kuridhishwa na chanjo hiyo na kusema kuwa wanaamini 
chanjo hiyo itawakinga na ugonjwa wa Saratani ya Mlango wa Kizazi na 
kukiri kutokujihusisha na vitendo vya ngono katika umri mdogo.
Asnath Melau msichana aliyepatiwa chanjo amesema kuwa, chanjo 
waliyoipata ni muhimu kwa maisha ya msichana hasa ukizingatia wanawake 
wengi hupoteza maisha kutokana na ugonjwa wa kansa ya mlango wa kizazi.
"Hii chanjo ni nzuri na ni muhimu kwetu wasichana, kwa kuwa wakina 
mama wengi wanakufa na kansa ya mlango wa kizazi, tunashukuru serikali 
kwa kutupatia kinga na inatupa amani ya kutokupata maambukizi" amesema 
Asnath.
Hafla hiyo imeambatana na igizo lililohamasisha jamii kuhakikisha 
wasichana wa miaka 14 wanapata chanjo ya Saratani ya Mlango wa Kizazi 
pamoja na upimaji wa afya, lililotolewa na kikundi cha sanaa cha vijana 
cha ACE AFRICA.
Hata hivyo Mkuu wa Wilaya Kimanta amelishukuru shirika lisilo la 
kiserikali la ACE AFRICA kwa kujitoa kwa halina mali kushiriki shughuli 
mbalimbali za kijamii ndani ya halmashauri ya Arusha
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni