




Na Mwandishi Wetu
Asasi Ya Vijana, Tanzania Youth Vision Association kwa Kushirikiana Na International Republican Institute zimetoa mafunzo ya kuboresha Uwezo wa Vijana kuhusu mchakato wa mabadiliko ya Katiba nchini katika visiwa vya Unguja na Pemba, Zanzibar.
Mafunzo hayo yameweza kufikia vijana 250 kwa njia ya Warsha na Vijana na wananchi zaidi ya 200,000 kupitia mitandao ya kijamii.Ndugu Nasser Mtengera (Mkuu wa Idara ya Habari na Utafiti, TYVA) alielezea Lengo kuu la Mafunzo hayo ni kuongeza uelewa na ushiriki wa Vijana katika mchakato wa Mabadiliko ya Katiba.
Katika ufunguzi wa mafunzo hayo Chake chake, Pemba Mheshimiwa Zainab Mussa Bakari (Mbunge) alibainisha kuwa wananchi wana haki ya kikatiba ya kushirikishwa katika mchakato wa katiba mpya na kusema nini wanachotaka kiwemo ndani ya katiba.
Mwanaharakati Na Mtetezi wa HAKI za Binadamu ndugu Deus Kibamba (Mwenyekiti - Jukwaa la Katiba Tanzania) alipata kuwaelezea washiriki wa mafunzo hayo historia ya mchakato wa mabadiliko ya Katiba, Ushiriki wa wananchi katika mchakato wa Katiba, hatua muhimu katika Mchakato wa utengenezaji Katiba, Mambo ya Msingi yaliyomo katika Katiba inayopendekezwa na Mambo muhimu kuelekea kura ya Maoni ya Katiba Inayopendekezwa.
Alidokeza pia, katika mchakato wa Katiba, hasa katika hatua ya Bunge la Katiba ulikosa maridhiano ya Kitaifa. kuna haja ya kuwepo mkutano wa kitaifa utajaowaleta wadau na jopo la wataalamu mbalimbali kwa ajili ya kunyambua yale mambo yanayoendelea kuleta ukakasi linapaswa kufanyika.
Alidokeza pia Mchakato wa katiba ulitegemewa kuwa kimbilio la kutatua kero za Muungano.Afisa kutoka IRI, Tony Alfred aliwatarifu Vijana washiriki kusoma kuhusu Katiba na wanaweza kupata habari na taarifa zaidi kuhusu Katiba kupitia ujumbe mfupi wa maandishi kwa kutuma Neno "katibayetu" Kwenda 0684996494.
Ndugu Saddam Khalfan (Katibu Mtendaji wa TYVA) aliwashukuru vijana na wadau mbalimbali kwa kuhudhuria na kufanikisha mikutano ya Unguja na Pemba huku akihimiza Mkakati wa ushiriki wa vijana ni mahsusi kwa ajili ya kuhakikisha kuboresha maendeleo ya vijana kwa Tanzania ya sasa na baadae. Tanzania ambayo inatamaniwa na kundi la vijana lakini sambamba na makundi mengine yote.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni