POLISI mkoani Morogoro wanashikilia watu 11, wakazi wa Kijiji cha Mpofu wilayani Kilombero kwa tuhuma za kuvamia na kuchoma moto kituo kidogo cha polisi na ofisi ya serikali ya kijiji hicho.
Watuhumiwa
 hao ni sehemu ya zaidi ya watu 100 wanaodaiwa kufanya uhalifu huo 
katika kituo hicho cha polisi Mbingu, katika taarifa ya Mgeta.
Watuhumiwa
 hao wanadaiwa kufanya tukio hilo wakishinikiza polisi wamwachie 
mtuhumiwa aliyewekwa mahabusu katika kituo hicho, Bashiri Kadugula (25),
 kwa tuhuma za kumshambulia mkewe, Veronica Chabula (21) ili wamwadhibu.
Kamanda
 wa Polisi wa mkoa wa Morogoro, Leonard Paulo, alisema jana kuwa, 
Kadugula aliwekwa ndani kwa kumkata mkewe kwa panga sehemu mbalimbali za
 mwili kutokana na wivu wa mapenzi.
Alisema
 katika tukio hilo ni la Agosti 20, mwaka huu saa 4:00 usiku, mtuhumiwa 
huyo baada ya kufanya kitendo hicho kwa mkewe akitoroka na ndugu wa 
Veronica walifanikiwa kumkamata na kumfikisha kituo kidogo cha Polisi 
Mbingu, ili hatua za kisheria zichukuliwe.
Alisema
 baada ya ndugu kuondoka kituo cha polisi, kitambo kidogo kulitokea 
kundi la watu wakirusha mawe kituoni hapo, wakitaka wamuue mtuhumiwa 
huyo kwa kukerwa na kitendo chake cha kinyama. Kamanda Paulo alisema, 
askari waliokuwepo kituoni hapo walijitahidi kuwazuia watu hao lakini 
walizidiwa nguvu.
Alisema polisi walifanikiwa kumtoa mtuhumiwa mahabusu na kumwokoa sambamba na kuokoa silaha za kituo hicho.
Alisema,
 watu hao waliokadiriwa kuwa zaidi ya 100, walivamia kituo hicho kidogo 
cha Polisi na kukichoma moto ambapo nyaraka mbalimbali zilizokuwa ndani 
ya kituo hicho ziliungua na kuteketea kabisa.
Kamanda
 wa Polisi wa mkoa alivitaja vitu vilivyoteketea kwa moto kuwa ni pamoja
 na pikipiki tano zenye usajili T 979 BGA aina ya Sky Mark, T901 BUJ 
aina ya Sanlug, T801 BQA aina ya Sanlug, mali ya Askari Wilson, T194 BVR
 aina ya T-Better, mali ya Askari Isaya na T904 BUJ aina ya Tianda.
Alisema,
 kundi la watu hao baada ya kukichoma moto kituo kidogo cha polisi, 
lilivamia pia Ofisi ya Serikali ya Kijiji cha Mpofu na kisha kuchoma 
moto nyaraka mbalimbali, ambapo katika matukio hayo watuhumiwa 11 
walikamatwa.
Amewataja
 waliokamatwa kutokana na tukio hilo kuwa ni Imani Mwampombe (40), 
Geofrey Mwaikambo (46), Eugen Kikoti (41), Janken Mwaikambo (55), 
Meshack Kikoti (42), Eliud Chumbula (52) na Shukrani Lukimo (35) ambao 
ni wakulima na wakazi wa kijiji hicho cha Mpofu.
Wengine
 waliokamatwa ni madereva wawili wa bodaboda ambao ni Ramadhani Hussein 
(29), mkazi wa Kitongoji cha Ngajengwana, Salum Ngala (36), John Mtikila
 (55) na Rodrick Mwaikambo (36) wote wakulima na wakazi wa Kijiji cha 
Tandale- Igima.
Kamanda
 huyo wa Polisi wa mkoa alisema kwamba watuhumiwa hao wanaendelea 
kuhojiwa na watafikishwa mahakamani mara upelelezi utakapokamilika na 
kwamba polisi wanaendelea kuwatafuta watuhumiwa wengine waliotoroka na 
kusisitiza kuwa wananchi wanapaswa kutii sheria na kuacha kujichukulia 
sheria mkononi.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni