
Serikali imesema kuanzia septemba 5, mwaka huu visimbuzi vitaanza kuonesha channeli zote za ndani bila kutoza gharama yoyote kwa mtazamaji.
Akiwaeleza waandishi wa habari jana jijini Dar es salaam, 
kuhusu yaliyozungumzwa katika  kikao kati ya Waziri wa Habari, 
Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe na wadau na wamiliki
 wa televisheni nchini, Mkurugenzi wa Idara ya Habari-MAELEZO na Msemaji
 Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi amesema kuwa serikali imefikia 
uamuzi huo baada ya visimbuzi vya AZAM, ZUKU na DSTV kutoonesha channeli
 za ndani, kulingana na aina ya leseni zao.
“Ningependa watanzania wafahamu kwamba kuanzia septemba 5 
mwaka huu, visimbuzi vya Ting, Starmedia, Continental na Digtek 
vitaonesha takribani channeli  34 za ndani bure, ili kutoa fursa ya kila
 mwananchi kuwa na  haki ya kupata taarifa” alisema Dkt. Abbasi
Aidha, alielezea kuwa wadau hao na wamiliki wa televisheni 
wameonesha kuridhishwa na hatua hiyo  kwa vile Serikali imetengeneza 
miundombinu itayoruhusu channeli zao kuonekana nchi nzima.
Dkt. Abbasi, alisisitiza kuwa “nchi imeandaa mfumo, ambao 
unaweza kufanyakazi bila kutegemea kampuni kutoka nje ya nchi kwa ajili 
ya kuonesha channeli za ndani au matangazo, kwa hivyo wadau au wamiliki 
wa vyombo vya habari wasihofu kuhusu hilo”
Kikao kati ya Waziri Mwakyembe na wadau  na wamiliki wa 
televisheni  nchini, kimefanyika kwa lengo la kuwa na majadiliano ya 
pamoja baina serikali na wadau hao ili kupata muafaka kuhusu kutooneshwa
 kwa chaneli za ndani katika visimbuzi vilivyokiuka masharti ya leseni 
zao.
Aidha, kikao hicho pia kilihudhuriwa na Mkurugenzi Mkuu wa 
Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), Injinia James Kilaba, pamoja na 
wataalamu wake.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni