Serikali kuwezesha tafiti zake kufikia uchumi wa kati

Na Ahmed Mahmoud
Serikali imeahidi kuendelea kuziwezesha kifedha taasisi  mbalimbali zinazojihusisha na  utafiti vikiwemo vyuo vikuu ili kuleta tija kwa taifa kufikia uchumi wa kati 
Akifungua Mkutano wa nne wa jumuia ya watafiti kutoka nchi za Afrika Mashariki (EARIMA), unaofanyika jijini Arusha,Mkuu wa wilaya ya Arumeru ,Jerry Muro akimwakilisha mkuu wa mkoa wa Arusha,amesema kuwa serikali itaendelea  kugharamia tafiti hizo ili kuwawezesha kuwafikia wakulima na wafugaji waweze kukua kiuchumi.
Amewaomba watafiti hao kuelekeza nguvu zao katika tafiti zinazofikika kwa jamii katika ukanda wa Afrika Mashariki kuhakikisha tafiti zao zinalinufaisha taifa na wananchi wake katika kushiriki shughuli za maendeleo
"Wataalamu na wabobezi wa tafiti mbalimbali mtusaidie kuzifanya tafiti hizi kuleta tija ili kulifikisha taifa katika uchumi wa kati"Amesema Muro
Amewataka watafiti hao kutoka nchi za Afrika Mashariki kuunganisha nguvu ya kutafuta njia zitakazosaidia tafiti zinazofanyika katika nchi hizo ziweze kwenda kwenye utekelezaji, hususani zile zinazolenga kutatua changamoto zinazowakabili wananchi wa Mataifa hayo.

Naye Mwenyekiti wa jumuiya ya watafiti wa Nchi za Afrika Mashariki (EARIMA), upande wa Tanzania Dk. Alfred Sebahene, amesema mkutano huo umekuja baada ya kuwa tafiti nyingi zinazofanywa bado hazijaleta tija ya kuchangia uchumi wa nchi hizo hususani katika kutatua matatizo yaliyopo kwenye  sekta za kilimo na Mifugo.

Amesema mkutano huo utajadili na kutoka na mapendekezo yatakayosaidia tafiti zinazofanywa ziweze kwenda kutatua changamoto zinazoikabili jamii ya mataifa hayo.
Amesema tafiti nyingi katika nchi mbalimbali za Afrika Mashariki zinafanana ila changamoto kubwa ni kutokana na mazingira yaliopo na hivyo mkutano huo utasaidia kubadilishana uzoefu .
Kwa upande wake mkuu wa sekretarieti ya EARIMA ambaye ni mhadhiri mwandamizi wa chuo kikuu cha Dar es salaam Dk. Edwinus  Lyaya amesema watafiti wamekuwa wakikabiliwa na changamoto ya bajeti ya kufikisha tafiti zao kwa jamii.

Amesema mkutano huo unalenga kusimamia utafiti na ugunduzi na kuhimiza tafiti za wataalamu ziweze kutoka kwenye makablasha na kuwafikia wananchi.

"Tunajadiliana ili kuzitoa tafiti kwenye maandishi na kufikia kwenye vitendo ili tafiti hizo ziweze kuzaa matunda kwa jamii" Amesema
Mmoja wa Watafiti kutoka Chuo kikuu cha Nelson Mandela Prof.Charlea Lugomela  alisema  chuo chao kimeshaanza kutoa tafiti mbalimbali zenye matumaini kwa Wakulima na Wafugaji.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni