Mshiriki Miss Tanzania Akiri Kudanganya Umri..!!!



Aliyekuwa mshiriki wa mashindano ya urembo ya Miss Tanzania mwaka 2008, Nelly Kamwelu, amekiri kudanganya umri katika mashindano hayo wakati huo ili apate fursa ya kushiriki mashindano hayo.

Nelly ambaye aliingia katika fainali za Miss Tanzania baada ya kushika nafasi ya tatu katika Miss Ilala, amesema wakati huo umri wake ulikuwa ni miaka 15, lakini ilibidi ajikuze ili kukidhi vigezo na kuamua kuandika umri wa miaka 18.

Nelly amefunguka siri hiyo hivi karibuni akiwa kwenye kipindi cha Friday Night Live cha EATV ambapo amesema sababu kubwa ya kulazimisha kushiriki katika mashindano hayo ni ndoto aliyokuwa nayo tangu akiwa mdogo, lakini pia umbile lake lilikuwa linamruhuruhusu kwa kuwa alionekana kuwa na mwili mkubwa licha ya kuwa na umri mdogo.

Ukweli huo unaonesha jinsi ambavyo ni rahisi kwa warembo kudanganya umri wao katika mashindano hayo, pasipo kugundulika

Nelly mbali na kushiriki mashindano hayo ya Miss Tanzania ambayo hakuambulia kitu, anasema hakukata tama na hivyo kuingia katika mashindano mengine ya urembo ambayo yalikuwa ni Miss Universe Tanzania mwaka 2011 na kuibuka mshindi.

Hadi sasa anashikilia rekodi ya kuwa mrembo pekee ambaye ameiwakilisha Tanzania katika mashindano manne tofauti ya dunia ndani ya mwaka mmoja, kwani katika mwaka huo wa 2011, licha ya kuiwakilisha Tanzania katika Miss Universe nchini Brazil pia aliiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Miss International mwaka 2011 nchini China na Miss Earth mwaka 2011 Manila, nchini Ufilipino ambapo katika mashindano hayo yote hakufanya vizuri.

Pia ndani ya mwaka huo huo w 2011 aliiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Miss Tourism Queen International yaliyofanyika Xian, China na kufanikiwa kukamata nafasi ya 5.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni