Maji kutoka katika kisima hicho yakitiririka kufuatia kufanyika kwa majaribio ya kuyatoa maji kutoka ardhini.
Kiongozi wa waendesha mitambo ya uchimbaji visima wa kampuni ya ZENTAS Bw. Sima Teodor ( kushoto) akitoa maelezo kwa wandishi wa habari kuhusu kazi ya uchimbaji wa kisima hicho katika eneo la mradi wilayani Mkuranga.
 Mtaalam wa mitambo wa 
Kampuni ya ZENTAS Sahtn Topal ( katikati) akifafanua teknolojia na vifaa
 vilivyotumika kuchimba kisima hicho.Picha na Aron Msigwa/ MAELEZO.
Na.Aron Msigwa- MAELEZO
Wananchi
 wa wilaya ya Mkuranga,mkoa wa Pwani wanatarajia kunufaika na mradi 
mkubwa wa usambazaji wa maji kufuatia kukamilika kwa zoezi la uchimbaji 
wa kisima cha maji chenye urefu wa mita 541 ambacho kina uwezo wa 
kuzalisha lita milioni  1.8  kwa siku.
Akitoa 
taarifa za kukamilika kwa kazi ya uchimbaji wa kisima hicho  mwakilishi 
wa kampuni ya kuchimba visima ya ZENTAS  kutoka Uturuki nchini Tanzania 
Dkt.Mohammed Akbar amesema wao kama wataalam wanaendelea na majaribio ya
 kuyatoa maji kutoka ardhini  jambo ambalo limeonyesha mafanikio 
makubwa.
 Amesema mtambo wa kuchimba kisima 
hicho uliwasili eneo la mradi Julai 9 mwaka huu na kuongeza kuwa mara 
baada ya kuwasili katika eneo la mradi kazi ya uchimbaji ilianza na 
kubainisha kuwa  sasa kisima hicho kinazalisha kiasi cha lita  76,000 
kwa saa na lita milioni  1.8 kwa siku.
Dkt. 
Akbar amesema endapo maji hayo yataunganishwa kwenye miundombinu ya maji
 ya mji huo yatakidhi mahitaji ya maji ya mji wa Mkuranga ambayo ni lita
 laki  Sita na Elfu mbili  kwa siku (602,000).
"
 Kwetu Haya  ni mafanikio makubwa ukizingatia mradi wenyewe haujaanza 
kusambaza maji kwani visima hivi vilikuwa ni kwa ajili ya utafiti, 
kiwango cha maji kilichopatikana ni kikubwa, kilichobakia sasa ni kwa 
mamlaka husika na Serikali kukamilisha mipango iliyobaki ili maji haya 
yawafikie wananchi" Amesema.
Ameongeza kuwa 
chini ya mradi huo wamechimba visima 9 na kati ya hivyo visima 7 
vinafanya vizuri na  2 vimeharibika na kueleza kuwa matarajio yao  ni 
kuona visima vitano ambavyo sasa  vimekamilika vizuri vikizalisha  lita 
milioni 55.
Meneja wa Mamlaka ya Maji Mkuranga 
mjini (MKUWASA) Muhandisi Filbert Pius akiuzungumzia mradi huo amesema 
kuwa utakapokamilika utawasaidia wananchi kupata maji safi na kuondoa 
tatizo la muda mrefu la ukosefu wa maji katika maeneo mbalimbali ya mji 
huo.
Amesema mahitaji ya maji katika mji huo ni
 makubwa kuliko uwezo wa sasa wa kuzalisha maji ambapo vyanzo vilivyopo 
vina uwezo wa kuzalisha lita 135,000 kwa siku  ikilinganishwa na 
mahitaji ya sasa ya lita 602,000 kwa siku kwa wakazi wapatao 25,847.
"
 Wananchi sasa watapata nafuu, tofauti kabisa na mwanzo, maji 
yanayozalishwa hapa ni mengi  lita 1,800,000 kwa siku hii inakidhi  mara
 mbili mahitaji yote ya wananchi wa mji wa Mkuranga " Amesisitiza 
Muhandisi Pius.
Ameiomba Serikali kuendelea 
kutoa fedha za kufanikisha ujenzi wa miundombinu yenye urefu wa kilometa
 2 inayotarajiwa kukamilika ndani ya mwezi huu ili Mkuranga  ambao sasa 
ni mji wa viwanda upate  huduma ya uhakika ya maji,
Pia
 amesema kukamilika kwa ujenzi wa matenki makubwa ya kuhifadhia maji 
eneo la Mkwalia ulipo mradi huo pamoja na eneo la Kurungu kutaiwezesha 
hospitali ya Wilaya ya Mkuranga kupata huduma ya uhakika ya maji ambayo 
imekuwa kero ya muda mrefu kwa wagonjwa wanafika kupata huduma.
Meneja
 Uhusiano wa Jamii wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASA) 
Bi.Nelly Msuya akifafanua kuhudsu mradi huo amesema unajengwa 
unatekelezwa na DAWASA kwa niaba ya Serikali na akifafanua kuwa maeneo 
yote yenye miundombinu ya maji katika wilaya ya Mkuranga yanatarajiwa 
kuanza kupata huduma hiyo ifikapo Oktoba mwaka huu.
Amesema
 mradi huo sasa uko katika hatua za majaribio na unatarajiwa 
kuwanufaisha wananchi wote mara  kukamilika kwa ujenzi wa miundombinu 
kwenye maeneo ambayo hayakuwa na mabomba ya kusambazia maji , ujenzi wa 
matenki makubwa ya kuhifadhia maji na kukamilika kwa  taratibu za 
kitaalam ili maji hayo yawafikie wananchi.
"Nachoweza
 kusema kwa upande wa wilayanya Mkuranga tumefika pazuri, sisi kama 
DAWASA watekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji kwa niaba ya Serikali 
tutahakikisha kero ya maji  katika wilaya hii  na maeneo mengine 
inapatiwa ufumbuzi,  tumeshatoa mamlaka kwa miji na wilaya  kubuni, 
kusimamia  na kuendeleza miradi ya maji ili wananchi wengi zaidi 
wanufaike" Amesisitiza.
Aidha, amebainisha kuwa
 mradi wa ujenzi wa visima 8 eneo la Mkuranga umegharimu kiasi cha 
shilingi bilioni 7.4 na kufafanua kuwa awamu inayofuata ni kuyapeleka 
maji hayo yakaunganishwe na mfumo wa kusambazia maji uliopo, ujenzi, 
uongezaji wa matenki makubwa ya kuhifadhia maji na ununuzi wa pampu ya 
kusukuma maji hayo kutoka kwenye chanzo.




Hakuna maoni:
Chapisha Maoni