Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya 
Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida akiingia katika 
ukumbi wa mkutano hoteli ya Double Tree by Hilton kwa ajili ya warsha ya
 vijana na ajira iliyofadhiliwa na  Mpango wa Shirika la Utafiti ya 
Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC) na kuratibiwa na ESRF.
Na Mwandishi wetu
VIJANA nchini Tanzania wanatakiwa 
kujitambua, kuacha kuwa kigeugeu na kufanya papara ya kupata fedha kama 
wanataka kuendelea na kufanikiwa kibinafsi na kiuchumi.
Kauli hiyo imetolewea jana na Meneja 
Ajira za Kifundi kwa vijana na Mratibu Kazi wa Shirika la Kimataifa la 
Kazi (ILO) Dk. Annmarie Kiaga kwenye warsha ya wadau wa kitaifa ya 
kujadili suala la ajira kwa vijana Tanzania .
Kauli yake hiyo kwa vijana hao 
waliojumuika katika hoteli ya DoubleTree by Hilton, Dar es salaam, 
ilitokana na tafiti mbalimbali zilizofanyika nchini ambazo zinaonesha 
kwamba vijana wengi hawana msimamo wa maisha, hawana maono, hawana 
malengo binafsi wala kutambua matarajio.
Amesema: “ Usipojitambua, leo nikija 
nikakueleza habari za kuanzisha biashara ya matofali utachangamkia. 
Kesho akija mtu mwingine akakueleza kuhusu uchimbaji wa madini utaacha 
kutengeneza tofali na kukimbilia machimboni”.
Akizungumza kwa ufasaha kabisa kuhusu 
vijana na ajira, alisema kila mmoja ana nafasi yake katika kuleta 
maendeleo yake na taifa na kwamba lazima kujituma na si kubweteka na 
kulalamika tu.
Akizungumza kwa mfano alimzungumzia  
kijana mmoja Joseph ambaye alikuwa mwadilifu sana na mwenye kumwamini 
Mungu. Anasema Kila siku Joseph aliamka asubuhi na kumuomba Mungu 
amsaidie aondokane na umaskini alionao.
Alifanyakazi hivyo kwa miaka 30 lakini maombi yake hayakumsaidia kuondokana na umaskini.
Siku moja, alisema, Mungu alimuona Joseph
 akiwa na masikitiko makubwa akamuuliza kulikoni, Joseph akamjibu: 
“Mungu ni miaka 30 leo tangu nianzie kukuomba uniwezeshe nishinde bahati
 nasibu. Mimi nimeishi maisha yangu kwa uadilifu nawe wajua . Lakini 
mbona maombi hayatimii?”
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya 
Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida akifungua warsha 
ya vijana na ajira iliyofadhiliwa na  Mpango wa Shirika la Utafiti ya 
Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC). Kushoto ni Meneja Ajira za 
Kifundi kwa vijana na Mratibu Kazi wa Shirika la Kimataifa la Kazi (ILO)
 Dk. Annmarie Kiaga na kulia ni Kiongozi Mpango wa Ukuaji na Ajira wa 
Taasisi wa Mpango wa Shirika la Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka
 Canada (IDRC) Dk. Arjan de Haan.
Naye Mungu akatabsamu akamwambia, Joseph, si ununue tiketi basi?
Dk Kiaga alisema kwa kuzingatia hadithi 
yake kila mmoja anatakiwa kufanya kitu na Joseph alisahau kwamba huwezi 
kushinda bahati nasibu bila kununua tiketi.
“Kumbuka haitoshi kuwa na elimu na ujuzi 
kama hutaweza kuweka elimu hiyo au ujuzi ulionao katika vitendo” alisema
 na kuongeza kuwa Joseph alikuwa anajua anahaitaji fedha ya kianzio 
lakini hakuchukua hatua ya kupata hela hiyo.
Alisema pamoja na ukweli kuwa asilimia 40
 ya watu  wasio na ajira duniani ni vijana, kwa maana ya kwamba kuna 
vijana wapatao milioni 75 duniani kote wanatafuta ajira huku vijana wa 
kike wakiwa na changamoto kubwa zaidi, ipo shida kubwa ya vijana kukata 
tamaa.
Aidha alisema kwamba hali ya kukata tamaa imewapeleka vijana kuongezeka katika soko la vijana wanaopata kazi zisizo na staha.
Alisema pamoja na sera zilizopo vijana wanatakiwa kuwa na shauku na kazi na pia kujitambua.
“Vijana wa siku hizi hawana mitazamo 
sahihi kuhusu ajira. Kwamba vijana hawana shauku na kazi na wana 
mitazamo hasi (ili mradi kazi..mkono uende kinywani?) . Matokeo yake ni 
kwamba vijana hawatumii ubunifu wowote katika kuboresha uwezekano wao wa
 kupata kazi zenye staha” alisema.
Amesema mtaji unahitaji kujiboreshea seti ya ujuzi katika kutafuta kazi ikiwa ni pamoja na uwezo, uzoefu na elimu.
Meneja Ajira za Kifundi kwa vijana na 
Mratibu Kazi wa Shirika la Kimataifa la Kazi (ILO) Dk. Annmarie Kiaga 
akizungumza kwenye warsha ya vijana na ajira iliyofadhiliwa na  Mpango 
wa Shirika la Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC) na 
kuratibiwa na ESRF.
Alisisitiza kuwa vijana waliowengi 
hawajitambui na kujiuliza ‘mimi ni nani’ au hawana malengo binafsi na 
matarajio mimi nataka kuwa nani na kusema bila kuyafanyia kazi mambo 
hayo mawili ya shauku ya kazi na kujitambua hakutakuwepo na mabadiliko.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya 
Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk Tausi Kida, akifungua warsha 
hiyo alisema pamoja na taifa kuwa mstari wa mbele kushughulikia ajira 
kwa vijana kwa kutunga sera zilizolenga kukidhi haja ya ajira,ikiwemo 
Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ya mwaka 2007, Sera ya Taifa ya 
Ajira ya mwaka 2008 na na mpango wa utekelezaji wa sera ya taifa ya 
ajira kwa vijana iliyo chini ya mtandao wa ajira unaofadhiliwa na 
shirika la kazi la Umoja wa Mataifa, changamoto bado zipo.
Aliwataka washiriki wa warsha hiyo wakiwemo vijana waliofanikiwa kueleza siri za fursa na kujiajiri ili kutoa mwanga kwa wenzao.
Pamoja na  warsha hiyo kutoa nafasi kwa 
vijana kujadili namna ya kutambua na kutumia fursa za kuichumi zilizopo 
nchini, kutoa ujuzi kwa vijana  wa namna ya kuingia katika soko la ajira
 ikiwa ni pamoja na kujiajiri, kukuza ujasiriamali na kuendeleza 
biashara, Dk Kida aliwasihi vijana kujitafutia riziki yake na kushiriki 
ipasavyo katika shughuli za kiuchumi na maendeleo.
Aliwataka kujijengea uwezo wa kufanyakazi pamoja na kubaini na kuzitumia fursa za kiuchumi na kibiashara zilizopo nchini.
Warsha hiyo iliyofadhiliwa na  Mpango wa 
Shirika la Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC) 
ilikutanisha vijana kutoka mikoa mbalimbali nchini Tanzania na 
kuwezeshwa kwa sehemu kubwa na Taasisi ya tamasha ambapo Mkurugenzi wake
 Mtendaji Richard Mabala alikuwa Mchokozaji mkuu.
Akiwasilisha salamu kutoka IDRC, kiongozi
 Mpango wa ukuaji na ajira wa taasisi hiyo. Dk Arjan de Haan alisema 
kwamba taasisi hiyo ya serikali ya Canada imekuwa ikitoa ushirikiano 
katika tafiti zilizolenga kuangalia utatuaji wa tatizo la ajira kwa 
namna inavyofaa.
Mtafiti Mwandamizi ESRF, Dk. Georgina Ole Saibul akiwasilisha mada katika semina ya vijana na ajira.
Alisema kwamba kwa kawaida taasisi yake 
husaidia pale inapoona utafutaji wa mbinu za kutatua tatizo 
unashirikisha na wahusika ili kupata suluhu endelevu ya tatizo husika.
Alisema ameridhishwa na kuona kwamba 
warsha hiyo imezingatia kanuni za IDRC za kutaka kutatua tatizo la ajira
 kwa kushirikisha vijana wenyewe, kuangalia na kushauri namna bora ya 
kukabili tatizo la ajira ambao kwa sasa ni changamoto kubwa duniani.
Alisema kwamba ipo haja ya kubadili baadhi
 ya sera kulingana na mahitaji ya sasa ili kuwezesha vijana wengi zaidi 
kuingia katika soko la ajira.
Wakati wa utambulisho na kuelezea kero zao
 katika  ajira wengi wa vijana waligusia kuwapo kwa sera ambazo si 
rafiki zinazotengeneza urasimu mkubwa katika kusaidiwa.
Ingawa wengi walisema fursa zipo, 
walizungumzia kutopata ushirikiano kutoka kwa wazazi , viongozi na 
taasisi mbalimbali zinazodai kupambana na ukosefu wa ajira kwa vijana.
Aidha vijana wengine walisema kwamba ni 
kweli kuna mtazamo hasi kwa vijana hasa kukata tamaa na pia kutaka 
maendeleo ya kasi huku wakikosa ubunifu.
Joachim Fanuel kutoka singida Youth 
Entrepreneurs and Consultants Cooperative Society (SYECLOS) alisema 
kwamba ingawa wao wanaendesha miradi ya kuku wa kienyeji na asali kama 
fursa zilizopo wanakabiliwa na tatizo la kukata tamaa kutokana na kuona 
kwamba inachukua muda mrefu kupata vitu wanavyotaka.
Aidha alisema kwamba wamekuwa 
hawasikilizwi na serikali na taasisi mbalimbali kwa kuwa hawana mali za 
kuwakilisha kama dhamana katika mambo mbalimbali.
 
Johari A. Sadik kutoka kampuni 
inayotengeneza nguo za kitamaduni Binti Africa,  akitoa ushuhuda kwamba 
vijana wanaweza kama watajitambua katika warsha ya siku mbili vijana na 
ajira inayofanyika hoteli ya DoubleTree by Hilton.
Kijana  Musa Mohammed kutoka Zanzibar 
alisema kwamba japo wana fursa za usindikaji wa vyakula, mizizi na 
matunda wamekuwa na tatizo la ujuzi katika uchakataji, sera duni 
zisizojibu mahitaji yao na kuwalinda katika soko.
Binti mmoja kutoka  Binti Africa Kampuni 
inayotengeneza nguo za kitamaduni alisema kwamba kuna shida ya kukata 
tamaa miongoni mwa vijana lakini pia hawajali kutafuta taarifa 
wanazohitaji wakisubiri kutafuniwa.
Vijana wengine walizungumzia ugumu wa 
mitaji, ukosefu wa taaluma na mfumo wa elimu kwuatengeneza kupata ajira 
katika serikali na taasisi zake.
Mshiriki Leticia Mango  kutoka Kigoma 
alisema kwamba ipo shida ya vijana wenye vipaji ambao hawana elimu 
vijijini kudharaulika na kutothaminiwa kwa kile kinachoonekana sio 
wasomi.
Alisema vijana wasomi wakiunganika na 
wenye vipaji wanaweza kuwa mbali zaidi na kusisitiza ipo haja vijana 
kuwa pamoja kwa maendeleo yao.
Joachim Fanuel kutoka Singida Youth 
Entrepreneurs and Consultants Cooperative Society (SYECCOS) akionesha 
chupa ya asali kutoka kwa mradi wa kikundi cha vijana ambao waliamua 
kujiajiri katika warsha ya vijana na ajira.
Joachim Fanuel kutoka Singida Youth 
Entrepreneurs and Consultants Cooperative Society (SYECCOS)  akizungumza
 na washiriki wa warsha ya vijana na ajira.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya 
Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida (kushoto) akiwa na
 Kiongozi Mpango wa Ukuaji na Ajira wa Taasisi wa Mpango wa Shirika la 
Utafiti ya Maendeleo ya Kimataifa kutoka Canada (IDRC), Dk. Arjan de 
Haan wakiwa katika warsha ya vijana na ajira.
Vijana wakishiriki kazi za vikundi kwenye warsha hiyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya 
Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Dk. Tausi Kida akiwa katika picha
 ya pamoja na vijana walioshiriki warsha ya vijana na ajira  hoteli ya 
Double Tree by Hilton jijini Dar.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni