
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa 
amesema Serikali imetenga sh. bilioni 4.3 ili kujenga vituo vya 
kuhifadhi damu (satellite blood banks) kwenye mikoa 12.
Ameitaja mikoa hiyo kuwa ni 
Manyara, Katavi, Rukwa, Ruvuma na Njombe. Mingine ni Tanga, Arusha, 
Pwani, Singida, Songwe, Geita na Simiyu.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo 
(Ijumaa, Juni 29, 2018) bungeni jijini Dodoma katika hotuba yake 
aliyoitoa wakati wa kuahirisha Mkutano wa 11 wa Bunge. Bunge 
limeahirishwa hadi Septemba 4, mwaka huu.
Amesema lengo la mpango huo ni 
kuboresha upatikanaji wa damu hasa kwa akinamama wanaopoteza damu nyingi
 wakati wa kujifungua. “Serikali imedhamiria kupunguza vifo vya 
akinamama na watoto vitokanavyo na uzazi. Katika kutekeleza azma hiyo, 
Serikali kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo inaendelea kufanya 
ukarabati na ujenzi wa majengo ya upasuaji, maabara, wodi za wazazi, 
nyumba za watumishi na wodi za watoto,” amesema.
Amesema kukamilika kwa majengo 
hayo, kutaboresha huduma za uzazi kwa akinamama na watoto wachanga. 
“Hatua hii itawezesha upatikanaji wa huduma kamili za uzazi na kupunguza
 vifo vya mama na watoto. Katika mwaka 2018/2019, eneo litakalopewa 
kipaumbele ni kuimarisha upatikanaji vifaa na watumishi katika vituo 208
 vinavyoendelea kuboreshwa,” amesema.
Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo 
kuwasihi watumishi wa afya, waongeze juhudi ya kuhamasisha wananchi 
wajitolee damu na pia akawaomba wananchi nao wawe na utamaduni wa 
kuchangia damu ili kuwezesha upatikanaji wa damu salama itakayohifadhiwa
 kwenye benki hizo.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu amesema
 Serikali inaendelea kuimarisha huduma za kibingwa nchini kwa kutenga 
shilingi bilioni 14 ili kuanzisha huduma ya kuchunguza mwili bila 
upasuaji (PET Scan) katika taasisi ya Saratani ya Ocean Road.
Amesema kuanza kwa huduma hiyo
 kutapunguza asilimia 80 ya wagonjwa wa saratani waliokuwa wanapelekwa 
nje ya nchi kwa ajili ya kipimo hicho na kwamba Serikali itaweza 
takribani shilingi bilioni 5 kwa mwaka zilizokuwa zinatumika kwa ajili 
ya kulipia wagonjwa waliokuwa wakienda nje ya nchi kwa ajili ya kipimo 
hiki.
Amesema Serikali itasogeza huduma 
ya tiba ya saratani katika ngazi ya Hospitali za Kanda ikiwa ni pamoja 
na Hospitali ya Bugando Mwanza, Hospitali ya Kanda ya Kaskazini KCMC na 
Hospitali ya Rufaa ya Kanda za Nyanda za Juu Kusini, jijini Mbeya.
“Vilevile, katika mwaka 2018/2019,
 Serikali itaimarisha upatikanaji wa huduma za kibingwa katika hospitali
 za rufaa za mikoa kwa kuboresha miundombinu ya kutolea huduma za afya 
ikiwa ni pamoja na majengo, vifaa tiba na madaktari bingwa. Jumla ya 
shilingi bilioni 40 zimetengwa kwa ajili ya kuimarisha hospitali hizi,” 
amesema.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu
 amesema Serikali kwa kushirikiana na washirika wa maendeleo kupitia 
Mradi wa Lipa Kulingana na Matokeo (Education Performance for Results – 
EP4R) itaimarisha miundombinu kwenye shule zenye uhitaji mkubwa.
“Katika mwaka 2018/2019, Serikali 
itatumia shilingi bilioni 155.58 kwa ajili ya ukarabati wa shule kongwe 
25, ununuzi wa vifaa vya maabara, ujenzi wa mabwalo 85, vyumba vya 
madarasa 2,000 na motisha kwa Halmashauri kutokana na ufanisi katika 
utekelezaji wa vigezo vya EP4R,” amesema.
Amesema kwa sasa, Serikali 
inatarajia kuajiri walimu 4,785 wa shule za msingi zenye uhitaji mkubwa 
na kwamba tayari imeshatangaza nafasi za ajira kwa walimu 2,000 wa 
masomo ya sayansi, hisabati na lugha ambao watapangwa kwenye shule za 
sekondari zenye uhitaji mkubwa.
Amesema kuwa Serikali imetangaza 
nafasi za ajira kwa mafundi sanifu maabara 160 ambao nao pia watapangwa 
kwenye shule zenye uhaba wa wataalamu hao.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni