Mwenyekiti
 wa Jumuiya ya Wazazi Tanzania Dk. Edmund Mndolwa akizungumza na 
Viongozi wa Jumuiya hiyo, leo mjini Tarime mkoani Mara. Kushoto ni 
Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo Erasto Sima, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo mkoa
 wa Mara Samweli Kiboya na Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi 
Tanzania uoande wa Zanzibar Haidar haji Abdallah na kulia ni Mwenyekiti 
wa CCM mkoa wa Mara Mrida Mshota.
Na Bashir Nkoromo, Tarime.
Mwenyekiti
 wa Jumuiya ya Wazazi Tanzania Dk. Edmund Mndolwa ameshangazwa na baadhi
 ya wanachama wa CCM na Jumuiya zake kushindwa kulipa ada ya uanachama 
ya sh. 1200 kwa mwaka, ambayo ni sawa ya bei ya soda moja.
Dk. 
Mndolwa ameelezea kushangazwa huko, wakati akizungumza na viongozi wa 
CCM na Jumuiya za CCM kutoka Wilaya za mkoa wa Mara, katika ukumbi wa 
CMG mjini Tarime, leo, akiwa katika ziara ya kikazi mkoani humo.
Kufuatia
 hali hiyo Dk. Mndolwa ameagiza viongozi kusimamia ipasavyo ili 
kuhakikisha kila mwanachama wa CCM na Jumuiya ya Wazazi Tanzania analipa
 ada yake ya kila mwezi, akisisitiza kuwa watakaoshindwa kufanya hivyo 
itakuwa ni mfano unaoonyesha kuwa hawafai uongozi kutokana na kushindwa 
kusimamia uhai wa Jumuiya hiyo na Chama Cha Mapinduzi.
"Unamkuta
 mtu kila mara anajinasibu kuwa ni mwanachama wa CCM au Jumuiya ya 
Wazazi, lakini wakati huo huo halipi ada ya uanachama ya kila mwaka 
mbayo gharama yake kwa kila mwaka ni sawa na bei ya soda moja ambayo 
kila siku anamudu kuinunua", alisema Dk. Mndolwa.
Alisema,
 ni jambo la muhimu kwa kila mwanachama kuhakikisha analipa ada yake ya 
uanachama kwa sababu kufanya hivyo ndiyo ishara pekee inayodhihirisha 
uanachama wake kwa kuwa asipofanya hivyo anakuwa mwanachama mfu 
asiyeshiriki katika kuimarisha uhai wa Chama.
Dk. 
Mndolwa amewasisitiza wanachama wa CCM kujiunga na Jumuiya za Chama 
akisema kwamba kufanya hivyo kunatoa fursa pana zaidi kwa mwanachama 
kuijenga CCM na pia hata kuwea kupata nafasi za uongozi kwa wepesi zaidi
 kuliko akiwa mwana CCM tu.
"Tazameni,
 hivi sasa mimi ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM lakini ni kwa sababu 
nimekuwa mwanachama wa Jumuiya ya Wazazi na kisha nikagombea kupitia 
huko na kupata Uenyekiti wa Jumuiya hii ambapo sasa kwa nafasi niliyo 
nayo ya Uenyekiti nimekuwa pia Mjumbe wa Kamati Kuu", alisema Dk. 
Mndolwa.
Akizungumzia
 maadili katika jamii, Dk. Mndolwa aliwatupia lawama wazazi kuwa ndiyo 
chanzo kikubwa cha kumomonyoka kwa maadili katika jamii kutokana na 
kuwaacha watoto wao kufanya wapendavyo katika masuala ya tabia.
"Unakuta
 binti anatoka nyumbani amefaa nguo za kubaka maungo na zinazoacha wazi 
baadhi ya maungo yanayostahili kusitiriwa, mzazi anaona lakini anamuacha
 bila kumkemea, matokeo yake binti anakuwa mitaani katika namna ya 
kutokuwa na maadili bora, ikitokea hivyo jua lawama ni kwa mzazi", 
alisema Dk. Mndolwa.
Alisema,
 hali kadhalika ni kosa la mzazi pale mtoto wa kiume anapotoka nyumbani 
huku amevaa katula au suruali inayoporomoka matakoni, kwa sababu mzazi 
anapaswa kukemea uvaaji huo kwa kuwa unatia aibu katika jamii.
"Unakuta
 mzazi anampa hela nyingi mtoto wakati anakwenda shuleni huku akisema 
kuwa kwa kuwa yeye alisoma katika mazingira ya taabu hataki mwanae asome
 kwa taabu, kumbe hajui kuwa kwa kufanya hivyo anamjengea mtoto 
vishawishi vya kutumbukia katika utumiaji wa dawa za kulevya na uvutaji 
bangi", alisema Dk. Mndolwa.
Dk. 
Mndolwa aliwataka wazazi kuwa mstari wa mbele kuwahakikisha wanasaidia 
kujenga maadili ya jamii kwa kuwakanya na kuwachukulia hatua thabiti 
watoto wao kila wanapowagundua au kuwaona wanajaribu kuanza kuiga tabia 
zinazomomonyoa maadili.
Akizungumzia
 mshikamano ndani ya Chama, Dk. Mndolwa aliwataka wana CCM kuachana 
kabisa na mtindo wa kung'ang'ania makundi kila baada ya uchaguzi na pia 
kuachana na tabia ya kuthani mtu fulani ni maarufu kuliko chama.
Dk. 
Mndolwa alisema, ikiwa wanachama wataachana na mambo hayo CCM inakuwa 
imejihakikishia kupata ushindi kila uchaguzi kwa kuwa inao wanachama na 
wapenzi wengi na kinachohitajika ni mshikamano tu.
"Hadi 
sasa kuna baadhi ya majimbo au Kata walizoshinda wapinzani katika 
uchaguzi uliopita, lakini kwa maoni yangu wapinzani hawakushinda maeneo 
hayo eti kwa sababu ni weledi sana, hapana. ukweli ni kwamba walishinda 
kwa sababu ya uzembe wa wana CCM wenyewe kung'ang'ania makundi baada ya 
kura za maoni", alisema Dk. Mndolwa.
Lengo 
la ziara hiyo ya Dk. Mndolwa katika mikoa ya Kanda ya ziwa na mkoa wa 
Singida, ni kuwashukuru wananchama wa Jumuiya ya Wazazi kwa kumchagua 
kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo na pia kuwatambulisha Makamu Mwenyekiti 
wa Jumuiya ya Wazazi Tanzania kwa upande wa Zanzibar Haidar Haji 
Abdallah na Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo Erasto Sima ambao ameambatana 
nao katika ziara hiyo.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni