Mkuu wa Mawasiliano  wa MultiChoice Tanzania Johnson Mshana
 akizungumza na waandishi wa habari Masaki jijini Dar es salaam leo 
wakati wa kutiliana saini mkataba wa udhamini na  Mwanariadha kinda 
Francis Damiano Damasi hayupo pichani  kushoto ni Wilhelm Gidabuday 
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT).
Mkuu wa Mawasiliano  wa MultiChoice Tanzania Johnson Mshana
 akimkabidhi mkataba Mwanariadha kinda Francis Damiano Damasi  baada ya 
kutiliana saini mkataba wa udhamini leo Masaki jijini Dar es salaam 
kushoto ni  wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) kulia ni Meta Petro 
Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) na 
kocha.
Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) na kocha akifafanua jambo katika mkutano huo.
Wafanyakazi wa Multichoice 
Tanzania kutoka kulia ni  Shumbana Walwa Afisa Masoko, Talha na Grace 
Mgaya  wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa hafla hiyo.
………………………………………………………………
MultiChoice Tanzania imetangaza 
kuendelea kudhamini mchezo wa riadha hapa nchini huku ikisaini 
makubaliano maalum ya kumdhamini mwanariadha kinda Francis Damiano 
Damasi. Udhamini huo unahusisha fedha ya kujikimu kwa mawanariadha huyo 
na mafunzo yake na wanariadha wengine katika kambi maalum ya mafunzo 
inayotarajiwa kuwa wilayani Mbulu.
Akizungumza wakati wa hafla ya 
kusaini mkataba wa udhamini kwa mwanariadha huyo, Mkuu wa Mawasiliano wa
 MultiChoice Tanzania Johnson Mshana, amesema kuwa dhamira kubwa ya 
MultiChoice ni kuhakikisha kuwa mchezo wa riadha unakuwa na mchango 
mkubwa katika kuliletea taifa sifa, kutoa ajira kwa vijana wengi na 
kuchangia kikamilifu katika kukuza uchumi wa nchi.
“Tunataka taifa hili lijulikane 
ulimwengu mzima kama chimbuko la mabingwa, na tumeanza na riadha. 
Tumedhamiria kukuza mchezo huu na kuufanya kama chanzo kikubwa cha ajira
 kwa vijana wetu, lakini pia riadha ni mchezo, ni burudani, na ni sekta 
nyeti kiuchumi kama ikiendelezwa” alisema Mshana na kuongeza “Tunataka 
kuusikia wimbo wetu wa taifa katika mashindano makubwa ya kimataifa, 
tunataka kuiona bendera yetu ikipepea juu katika kila mashindano makubwa
 ya riadha ya kimataifa, tunataka mamia ya vijana wetu wenye uwezo 
mkubwa katika riadha washiriki kwenye mashindano makubwa, waweze 
kujipatia kipato, kuwekeza na kuwa chanzo cha maelfu ya ajira na 
hatimaye kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya kiuchumi ya nchi yetu”
Amefafanua kuwa udhamini huo 
utakuwa wa mwaka mmoja na utaendelezwa na kuboreshwa kulingana na hali 
itakavyokuwa pamoja na mafanikio yatakayopatiokana. “ Huu ni mkakati 
wetu endelevu, ni mpango wetu maalum unaojulikana kama ‘Ni Zamu Yetu’! 
ambao umejikita katika kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana wetu 
katika riadha.” Amesema Mshana.
Mbali na kumdhamini Damiano, 
MultiChoice pia itadhamini kambi maalum ya mafunzo itakayokuwa wilayani 
Mbulu ambayo inatarajiwa kuanza mafunzo rasmi hivi karibuni. Amebainisha
 kuwa taratibu za kuanza kwa kambi hiyo zipo katika hatua nzuri na kambi
 inatarajiwa kuanza rasmi Agosti mwaka huu na itakuwa na wanariadha 
kinda wasiopungua sita – wasichana na wavulana.
Kwa upande wake mwanariadha 
Damiano ambaye ni mshindi wa medali ya shaba katika mashindano ya vijana
 ya Jumuia ya Madola yaliyofanyika visiwa vya Bahamas, amesema udhamini 
huo utamfanya aweze kufanya mazoezi yake vizuri kwani sasa hyo ndiyo 
itakuwa kazi yake ya kudumu. Amesema kilicho mbele yake ni ushindi tu. 
“Nashukuru sana kwa udhamini wa MultiChoice, na mimi naahidi kuwa 
nitafanya kila niwezalo kuhakikisha kuwa siwaangushi MultiChoice na 
siwaangushi watanzania.”
Katibu mkuu wa Shirikisho la 
Riadha Tanzania Wilhelm Gida-Buday, amesema wamefarijika sana kuona kuwa
 MUltiChoice inaendelea kudhamini riadha na akasema udhamini huo siyo tu
 utamsaidia mwanariadha husika, bali pia ni chachu hata kwa wanariadha 
chipukizi kuwa na moyo na ari ya kushiriki katika mchezo huo.
Amesema Shirikisho la Riadha 
Tanzania litahakikisha kuwa udhamini huo unakuwa wa manufaa na unazaa 
matunda yaliyotarajiwa ya kuleta medali zaidi kutaka katika mashindano 
ya kimataifa. “Ufadhili wa aina hii ni muhimu sana kwa maendeleo ya 
mchezo wa riadha. Tunaahidi ushirikiano wetu wa hali na mali ili 
kufanikisha malengo na tutahakikisha kuwa tunatoa ushirikiano 
unaostahili kwa wadhamini wetu” alisema Gida.
Mwanariadha Francis Damiano 
Damasi, anatarajiwa kushiriki mashindano makubwa ikiwemo Mashindano ya 
vijana ya Afrika Mashariki yanayofanyika mwishoni mwa wiki hii jijini 
Dar es Salaam, Mashindano ya vijana ya Dunia (World Junior Championship)
 mwezi Julai nchini Finland, Mashindao ya vijana ya Olympic kanda ya 
Afrika mwezi Julai nchini Algeria, Mashindano ya vijan ya Olympic (Youth
 Olympic Games) mwezi Oktoba nchini Argentina, na mashindano ya nyika ya
 vijana (World Junior Cross-country) mapema mwakani nchini Denmark.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni