Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais 
Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo akifungua warsha
 ya kujadili changamoto za Uendeshaji wa Mabaraza ya Biashara Tanzania 
inayofanyika kwa siku mbili Jijini Dodoma.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Dkt. 
Bilinith Mahenge akizungumza na wadau wa baraza la biashara kabla ya 
kumkaribisha mgeni rasmi kufungua warsha hiyo.
Kaimu Mkurugenzi wa Tawala za 
Mikoa OR-TAMISEMI Beatrice Kimoleta(kwanza Kushoto) akiwa na Mkurugenzi 
Msaidizi wa Utawala bora na Huduma OR-TAMISEMI Angelista Kihaga (kwanza 
kulia) pamoja na wadau wa Baraza la Biashara katika warsha ya kujadili 
uendeshaji wa Mabaraza ya Biashara.
Mshauri wa Majadiliano baina ya 
Sekta Umma na Binafsi wa LIC Bw. Donald Liya (Kwanza kushoto) akifuatiwa
 na Kiongozi Msaidizi wa Timu ya LIC Bw. Peter Laizer, Mshauri wa Mradi 
wa LIC toka Taasisi ya Sekta Binafsi Bi. Rehema Mbugi pamoja na 
Kaimu Mkurugenzi wa TCCIA Bw. Gotfried Muganda wakifuatilia warsha ya 
kujadili changamoto ya Uendeshaji wa Mabraza ya Biashara.
Mkurugenzi Msaidia wa Utawala toka OR-TAMISEMI Bw. Mrisho Mrisho akiongoza warsha ya Mabaraza ya Biashara Tanzania.
………………..
Nteghenjwa Hosseah, OR-TAMISEMI.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais 
Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo amewataka Wakuu 
wote wa Mikoa na Wilaya Nchini kuhakikisha wanaanzisha kituoa kimoja cha
 huduma ‘One Stop Center’ kwa ajili ya wawekezaji.
Mhe. Jafo ameyasema hayo wakati wa
 ufunguzi wa Warsha ya namna ya Uendeshaji wa  Mabaraza ya Biashara kwa 
Mikoa na Halmashauri zote Nchini iliyoandaliwa na Ofisi ya Rais TAMISEMI
 kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na Mradi wa Local Investiment Climate (LIC) inayofanyika kwa siku mbili Jijini Dodoma.
Katika Warsha hiyo inayowajumuisha
 viongozi wa Ngazi za Mkoa na Wilaya Mhe. Jafo amesema mazingira magumu 
ya upatikanaji wa taarifa za uwekezaji na urasimu uliopo katika Mikoa na
 Wilaya ndio unaowakwaza Wawekezaji katika harakati zao za kutaka 
kuwekeza katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.
“Imekuwa ni vigumu sana kwa 
Muwekezaji kupata taarifa sahihi na kwa wakati katika maeneo yetu na hii
 imekua ikiwakatisha moyo na kupelekea hata kusitisha mpango mzima na 
nia yao ya kuwekeza katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, inatakiwa 
tubadilike na tuweke mazingira rahisi yatakayomuweza kila mdau anayetaka
 kuwekez kupata taarifa anazozihitaji kwa urahisi.
Hali hii inarudisha nyuma juhudi 
zetu za kuhamasisha uwekezaji sasa basi kila kiongozi wa Mkoa na Wilaya 
kuhakikisha wanaanzisha kituo kimoja “One Stop Center” ambacho 
kitatoa huduma zote kwa Wawekezaji kama vile upatikanaji wa maeneo ya 
uwekezaji, Leseni za biashara, Hati miliki, usajili wa kampuni, namna ya
 ulipaji wa kodi nk” alisema Jafo.
Aliongeza kuwa warsha hii 
imewakutanisha wadau kutoka Sekta ya umma na binafsi katika kila ngazi 
ya utawala ili kujadiliana namna bora ya kuboresha mazingira ya biashara
 na uwekezaji Nchini na hivyo basi ni wakati wa kukubaliana kwa pamoja 
namna mabaraza ya Biashara yatakavyosaidia katika kukuza Uchumi wa 
Viwanda ambao ndio muelekeo wetu kama Taifa kwa hivi sasa.
Sambamba na hilo Jafo 
aliwakumbusha viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuwa pamoja na 
majukumu mengine wanapaswa kutengeneza mazingira bora ya kufanyia 
biashara na uwekezaji, kuibua fursa za uwekezaji, kuzinadi fursa 
zilizoibuliwa kupitia Makongamano ya uwekezaji na kuandaa midahalo 
mahususi.
Pia Mhe. Jafo alisisitiza kuwa 
mara baada ya kikao hiki kila kiongozi akahakikishe kuwa Vikao vya 
mabaraza ya Biashara vinafanyika kwa mujibu wa Sheria na viongozi 
washiriki katika vikao hivyo na maazimio ya vikao hivyo yakashughulikiwe
 kwa wakati na kutoa mrejesho kwa upande wa sekta za umma na binafsi.
Aidha kila Halmashauri zikatenge 
bajeti kwa ajili ya uendeshaji wa Mabaraza ya biashara  na kwa upande wa
 Sekta binafsia ziandae utaratibu mzuri wa kuchangia gharama za 
uendeshaji wa vikao hivyo.
Alimalizia kuwa Mradi wa LIC kwa 
kushirikiana na Ofisi ya Rais TAMISEMI pamoja na Baraza la Taifa la 
Biashara kuandaa utaratibu wa kueneza uzoefu uliopatikana katika Mikoa 
miwli ya Dodoma na Kigoma ambapo mradi huu umetekelezwa ili mikoa 
mingine iweze kujifunza na kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji.
Mabaraza ya Biashara Tanzania 
yameanzishwa kwa mujibu wa Waraka wa Rais Na. 1 wa mwaka 2001 na 
kuchapishwa kwenye Gazeti la Serikali Na. 691 la tarehe 28 Seot,2001.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni