
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akisoma hotuba ya kuahirisha Mkutano wa  11 wa Bunge,  jijini Dodoma Juni 29, 2018. 
Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu
………………….
*Ni baada ya Serikali na wananchi kulinda rasilimali za nchi 
IMEELEZWA kuwa jitihada za 
Serikali za kulinda rasilimali za nchi na ushirikiano kutoka kwa 
wananchi zimesababisha ongezeko kubwa la idadi ya wanyama pori, hivyo 
kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye wanyama wengi barani Afrika. 
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa 
ameyasema hayo leo (Ijumaa, Juni 29, 2018) katika hotuba yake aliyoitoa 
bungeni wakati wakuahirisha Mkutano wa 11 wa Bunge jijini Dodoma. 
Amesema ili kuitumia vema fursa ya
 kuwa na vivutio vingi ikiwemo wanyamapori wengi na kuleta tija kwa 
nchi, Serikali imeendelea kuandaa utambulisho wa Tanzania Kimataifa 
(Destination Branding), lengo likiwa ni kuitambulisha Tanzania kama 
kituo mahsusi cha utalii duniani.
“Tunalenga kuvutia wageni wa 
kimataifa waje kuitembelea Tanzania, kuongeza wigo wa kutangaza vivutio 
na kufanya vivutio vya utalii vifahamike duniani. Pia, Serikali 
inakamilisha mchakato wa kuanzisha Channelmaalum katika Television ya Taifa (TBC1) kwa ajili ya kutangaza utalii,” amesema. 
Waziri Mkuu amesema maandalizi ya 
kuanzisha studio ya kutangaza utalii kwa njia ya Teknolojia ya Habari na
 Mawasiliano (TEHAMA) yanaendelea vizuri, ambapo studio hiyo itawezesha 
kutambua, kufuatilia na kuwasiliana moja kwa moja na watu wanaofuatilia 
Tanzania na vivutio vyake.
Pia, Serikali inakusudia kuanzisha
 chombo kitakacho simamia fukwe za bahari, mito na maziwa lengo la hatua
 hiyo ni kuimarisha utalii wa fukwe Bara na Visiwani kwa kujenga hoteli,
 maeneo ya mapumziko na michezo mbalimbali. 
Wakati huo huo, Waziri Mkuu 
amezungumzia jitihada zinazofanywa na Serikali katika kukabiliana na 
changamoto ya migogoro ya matumizi ya ardhi miongoni mwa watumiaji kwa 
kuunda timu ya kisekta ikijumuisha watendaji wa sekta mbalimbali 
zinazohusika kwenye masuala hayo. 
Sambamba na hilo, Waziri Mkuu 
amesema Serikali imeandaa mipango ya matumizi ya ardhi, kupima mipaka ya
 vijiji, kutunga na kurekebisha sera, sheria na kuandaa mipango 
mbalimbali ya kuboresha matumizi na utawala wa ardhi.
Kadhalika, Waziri Mkuu amesema 
Serikali imeandaa mipango ya kupanga, kupima na kumilikisha kila kipande
 cha ardhi nchini. “Ni matumaini yangu kwamba programu hii ikitekelezwa,
 ardhi itatoa mchango mkubwa katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii na 
pia kudhibiti migogoro ya ardhi,”. 
Waziri Mkuu amesema katika mwaka 
wa fedha 2018/19, Serikali itaendelea kutatua migogoro inayojitokeza na 
pia kutoa elimu kwa umma ili watumiaji wote wa ardhi waweze kuzingatia 
mipango ya matumizi ya ardhi inayoandaliwa katika vijiji. 
Amesema katika juhudi za kudhibiti
 migogoro kwenye maeneo mbalimbali ya utawala, jumla ya vijiji 11,256 
kati ya vijiji 12,545 vilivyopo nchini vimepimwa, hiyo ni sawa na 
asilimia 90 ya vijiji vyote, huku lengo likiwa ni kupima mipaka ya 
vijiji vyote na kuvipatia vyeti vya kijiji kwa kushirikiana na wadau wa 
maendeleo. 
“Hatua hii itasaidia kwa kiwango 
kikubwa kutatua migogoro ya mipaka kati ya vijiji. Ili kuharakisha kasi 
ya upimaji nchini, Serikali itaendelea kutumia makampuni binafsi ya 
upimaji na upangaji makazi kwa vibali maalum,”.
Akizungumzia kuhusu hifadhi ya 
mazingira, Waziri Mkuu amesema misitu inaendelea kukatwa hovyo kwa 
sababu mbalimbali ikiwemo matumizi ya nishati ya mkaa na kuni, ili 
kukabiliana na tatizo hilo Serikali itaendelea kuhamasisha matumizi ya 
nishati mbadala kote nchini.
Amesema Serikali itashirikiana na 
sekta binafsi kuweka utaratibu mahsusi wa kuwawezesha na kuwaratibu 
wajasiramali wanaojishughulisha na nishati mbadala ili kuwa na 
uzalishaji wa kutosha wa nishati hiyo na iweze kusambazwa katika maeneo 
yote nchini. 
Aidha, Serikali itaendelea 
kuboresha na kukamilisha Mkakati wa Tungamotaka (National Biomass Energy
 Strategy) na kusambaza kwa wadau nchini ili kuratibu vyema upatikanaji 
na matumizi ya nishati hiyo. 
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni