Wagombea 
ubunge wa majimbo 10 wana kazi ya ziada ya kufanya kabla ya Jumapili 
wakati wananchi watakapopiga kura kuamua ushindani mkali uliotanda kwa 
karibu miezi miwili ya kampeni za Uchaguzi Mkuu, kwa mujibu wa uchunguzi
 wa Mwananchi.
Ushindani
 huo mkubwa unatokana na vyama vya wagombea hao kuwekeza nguvu nyingi 
kwenye majimbo ili kuyarejesha, kuyalinda au kuwaengua wagombea ambao 
wanaonekana kuwa watakuwa wasumbufu iwapo watafanikiwa kuingia Bunge la 
11.
Iringa 
Mkoani 
Iringa, majimbo ya Iringa Mjini na Kilolo yana ushindani mkali.Jimbo la 
Kilolo linawaniwa na wagombea kutoka vyama vinne, Venance Mwamoto wa 
CCM, Taji Mtuga (ACT Wazalendo), Brian Kikoti (Chadema) na Lameck Mgimwa
 wa Chausta.
Hata 
hivyo, upinzani mkali unaonekana kuwa kwa Mwamoto, ambaye amerejea tena 
kwenye kinyang’anyiro hicho baada ya kuenguliwa kwenye kura za maoni za 
CCM mwaka 2010, na Kikoti, ambaye nguvu yake inatokana na kuungwa mkono 
na vyama vinne vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Ushindani
 huo unaelezwa kuanzishwa na mpasuko ndani ya CCM ulitokana na kura za 
maoni. Baada ya Mwamoto kumshinda Profesa Peter Msolla, aliyekuwa 
mbunge, na baadhi ya makada wa chama hicho kutimikia Chadema.
Mkazi wa 
Kilolo, Paulo Ngayomela, aliyekuwa mpambe wa Msolla, alisema yeye na 
wenzake walimuaga mbunge huyo wa zamani na kuungana na kambi ya upinzani
 baada ya kutoridhishwa na mchakato wa kumpata mgombea ndani ya CCM.
Mwamoto, 
ambaye aliangushwa na Profesa Msolla mwaka 2010, alisema bado ana nafasi
 ya kushinda kwa kuwa ni kama anatetea jimbo kwa kuwa aliliongoza jimbo 
hilo kuanzia mwaka 2005 hadi 2010.
Iringa Mjini 
Jimbo 
jingine gumu kutabiri ni Iringa Mjini ambalo linawaniwa na Robert 
Kisinini wa DP, Daudi Masasi (ADC), Mchungaji Peter Msigwa wa Chadema, 
Chiku Abwao (ACT Wazalendo) na Frederick Mwakalebelea wa CCM.
Hata hivyo, Mchungaji Msigwa anayetetea kiti chake na Mwakalebela ndiyo wanaonekana kupambana vikali.
Mwakalebela
 anabebwa na falsafa inayotumiwa na CCM za kukomboa jimbo ambayo 
imefanikisha kuvunjwa makundi yaliyoundwa na wagombea wa nafasi hiyo 
wakati wa kura za maoni.
Mmoja wa makada wa chama hicho, Abdallah Mpogole alisema kwa sasa wanachama wote wameshikamana na wanachoangalia ni ushindi.
Hata 
hivyo, kada mmoja wa Chadema, Mussa Ali alisema: “Tukubali tusikubali 
tangu jimbo lilipoanzishwa, hakuna aliyefanya kazi kama Msigwa akiwa 
mbunge. Alipigania masilahi ya wakazi wa Iringa ikiwamo ujenzi wa 
barabara, maji na kutoa misaada ya vitanda katika Hospitali ya Wilaya ya
 Iringa.
Jimbo 
hilo linaangaliwa kwa karibu na uongozi wa kitaifa wa vyama hivyo. 
Mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa alikuwa wa kwanza kupita Iringa
 Mjini na kuvuta maelfu ya watu. Lakini Mgombea urais wa CCM, Dk John 
Magufuli alifuta nyayo zake alipopita muda mfupi baadaye.
Ilemela 
Mkoani 
Mwanza, Jimbo la Ilemela lina mchuano kutokana na CCM kutaka kulirejesha
 kutoka Chadema waliolitwaa mwaka 2010. CCM imemsimamisha Anjelina 
Mabula kupambana na mbunge anayemaliza muda wake, Highness Kiwia wa 
Chadema.
Kada wa 
CCM na mkazi wa Kata ya Kirumba, Yusuf Juma alisema uchaguzi wa Jimbo la
 Ilemela hauna mvutano kama Nyamagana, kwa sababu mgombea amekuwa na 
ushawishi mkubwa kuliko mwenzake wa Chadema.
Hata 
hivyo, mkazi wa National ambaye ni mfuasi wa Chadema, Shadrack Magafu 
alipinga akisema uchaguzi mwaka huu umekuwa mgumu kutokana na kila mtu 
kuhubiri mabadiliko.
Bukoba Mjini 
Hali pia 
ni ngumu kwenye Jimbo la Bukoba Mjini mkoani Kagera, ambako ushindani ni
 mkali zaidi ya ule wa mwaka 2005. Linawakutanisha wagombea ambao ni 
mahasimu wakubwa, Wilfred Lwakatare wa Chadema, na Balozi Khamis 
Kagasheki wa CCM.
Wakati 
Kagasheki akitetea jimbo hilo kwa kipindi cha tatu, mshindani wake 
anawatumia makada wa CCM waliohamia upinzani kujiimarisha kisiasa 
akiwamo aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Bukoba, Dk Anatory Amani 
aliyehamia NCCR- Mageuzi iliyo ndani ya Ukawa.
Kundi la 
Dk Amani lililojiunga linaongezewa nguvu na aliyekuwa mwenyekiti wa 
UVCCM wa Manispaa ya Bukoba, Chifu Karumuna aliyehamia Chadema na 
kuongeza ushindani, huku Balozi Kagasheki akitajwa kuungwa mkono na 
wanawake wengi.
Baadhi ya
 wakazi wa Bukoba wanafananisha ushindani uliopo sasa na ule wa mwaka 
2005. Mkazi wa Mtaa wa Miembeni, Levina Paul alisema anaona ushindani 
mkubwa.
“Wanawake
 wengi tunamuunga mkono Kagasheki tofauti na inavyoonekana kwa vijana, 
ila wagombea wote wanaweza kuwa na nguvu sawa,” alisema Paul.
Musoma Mjini 
Mkoani 
Mara, vita kali inaonekana Jimbo la Musoma Mjini, kati ya Vincent 
Nyerere wa Chadema na Vedastus Mathayo wa CCM aliyeangushwa na mshindani
 wake huyo mwaka 2010.
Jimbo 
hilo lina wagombea tisa ambao ni Tongora Eliud (ACT–Wazalendo), Ibrahim 
Seleman (Tadea), Maimuna Matola (ADC), Ruttaga Sospeter (AFP), Vedastus 
Mathayo (CCM), Vincent Nyerere (Chadema), Gabriel Ocharo (CUF), 
Nyakitita Chrisant (DP) na Makongoro Jumanne (UMD).
Mkazi wa 
mjini hapa, Leonard Lugwisha alisema kati ya wagombea hao mwenye nguvu 
zaidi na uhakika wa ushindi ni Nyerere, kwa kuwa ndiye mbunge 
anayependwa na vijana na watu wengi wamechoka kuongozwa na CCM.
Moshi Mjini 
Hali ni 
mbaya zaidi Moshi Mjini, ambako wagombea wa CCM na Chadema wanachuana 
vikali kumrithi Philemon Ndesamburo ambaye ameamua kutogombea.
CCM 
imemsimamisha Davis Mosha na Jaffar Michael anagombea kwa tiketi ya 
Chadema, ambao wamefanya uchaguzi wa mwaka huu kuwa na ushindani ambao 
haujawahi kuonekana tangu mwaka 1995.
Mkazi wa 
Soweto, George Mberesero alisema ushindani wa vyama hivyo viwili ni 
mkubwa na kueleza kuwa kama si makosa ya kiufundi, CCM ingepata kura 
kuliko miaka ya nyuma.
“Huko nyuma ni kama CCM ilikuwa inafanya utani kwenye kampeni lakini safari hii imefanya kampeni,” alisema Mberesero.
Mfanyabiashara Patrick Boisafi alisema awali CCM ilianza vizuri harakati za kukomboa jimbo, lakini vurugu zimewatia doa.
Mkazi 
mwingine wa jimbo hilo, Goodluck Moshi alisema: “CCM wanaenda nyumba kwa
 nyumba, lakini Chadema wanaenda mitaani. Vijana wengi wa mtaani si wa 
jimbo hili. Davis anakubalika kwenye kata zenye watu wengi kama Njoro na
 Bomambuzi,” alisema.
Katika jimbo hilo, wagombea wa vyama vya ACT-Maendeleo, Buni Ramole na Issack Kireti wa SAU hawana nguvu.
Kawe 
Jijini 
Dar es Salaam, nguvu ya Ukawa na CCM imeelekezwa Jimbo la Kawe ambako 
CCM imemsimamisha Kippi Warioba na wakati Chadema imeendelea kumuamini 
mbunge aliyemaliza muda wake, Halima Mdee.
Inaelezwa
 kuwa Kippi anategemea ushawishi wa baba yake, Jaji Joseph Warioba, 
ambaye apia ameshasimama jukwaani kumpigia debe mwanaye.
“Watu wanaweza kumchagua kwa kumfananisha na uzalendo wa baba yake,” alisema Maria Mashasi, mkazi wa Kawe.
Hata 
hivyo, Aliko Mwansisya ambaye pia ni mkazi wa Kawe, alisema Mdee anayo 
nafasi kubwa zaidi ya kutetea jimbo hilo kutokana na ushawishi wake 
ndani ya Bunge.
Ubungo 
Hali 
kadhalika, Jimbo la Ubungo lina upinzani mkali kati ya mgombewa wa 
Chadema, Saed Kubenea, ambaye ni mwandishi wa habari, na wa CCM, Dk 
Didas Masaburi, ambaye ni meya wa jiji anayemaliza muda wake.
“Kubenea ana nafasi ya kushinda kutokana na umaarufu wake na nguvu ya chama,” alisema mkazi wa Ubungo, Charles Temba.
Lakini 
Vicent Julius alisema pamoja na umaarufu, Kubenea atakuwa na wakati 
mgumu wa kushinda jimbo hilo kutokana na ushawishi, uzoefu wa Dk 
Massaburi.
Ushindani mkali pia upo Same Mashariki, Mtama, Vunjo, Tarime Mjini, Tarime Vijijini, Bunda Mjini na Ukerewe.
Imeandikwa na Geofrey Nyang’oro, Midraji Ibrahim na Phinias Bashaya na Kelvin Matandiko
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni