Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Mrisho Gambo leo ametekeleza 
agizo la Mhe Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dr. John 
Joseph Pombe Magufuli la kusitisha safari ya kwenda Mkoani Simiyu kwenye
 sherehe za kwenda kuhitimisha kilele cha mbio za mwenge wa Uhuru kwa 
kurejesha kiasi cha Jumla ya Shilingi 1,389,300 ambayo yalikuwa ni 
malipo kwa ajili ya Mkuu wa Mkoa, Msaidizi wa Mkuu wa Mkoa , Dereva wa 
Mkuu wa Mkoa na gharama za mafuta.
Kwa mujibu wa mchakato wa malipo ya posho kwa safari hiyo 
ya kwenda mkoani Simiyu kwa siku tatu, posho ya RC ilikuwa ni  Sh 
360,000, Msaidizi wa RC Sh 240,000, posho ya dereva 240,000 na Sh 
549,300 kwa ajili ya Mafuta ya gari.
Akiongea na mwandishi huyu ofisini kwake leo, Mkuu huyo  wa
 Mkoa wa Arusha amesema wakati agizo hilo linatolewa yeye alikuwa bado 
hajaanza safari ya kuelekea Mkoani Simiyu, na kwamba amelipokea bila 
kinyongo na mara moja akaamua kurejesha posho hiyo, akionesha stakabadhi
 ya kuthibitisha hilo (pichani).
Pia Rc Gambo ameahidi kusimamia zoezi hilo kwa wahusika 
wote mkoani Arusha na  kuhakikisha wanatekeleza agizo hilo kwa wakati na
 fedha hizo zielekezwe kwenye ujenzi wa madarasa kama sehemu ya 
maandalizi ya kuwapokea wanafunzi wa kidato cha kwanza, darasa la kwanza
 na darasa la awali kwa mwaka 2017.
Rais Dkt. Magufuli  jana aliagiza viongozi wote wa Serikali
 walioalikwa kuhudhuria sherehe za Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru 
kitaifa zitakazofanyika tarehe 14 Oktoba, 2016 katika Wilaya ya Bariadi 
Mkoani Simiyu kutohudhuria sherehe hizo na wale ambao walishalipwa fedha
 ya posho na safari kwa ajili hiyo wazirejeshe.
Rais Magufuli alitoa maagizo hayo ikiwa ni utekelezaji wa 
azma ya Serikali ya awamu ya tano ya kubana matumizi yasiyo ya lazima na
 kuelekeza rasilimali nyingi katika shughuli za maendeleo ya nchi.
Viongozi waliotajwa kutakiwa kufuta safari zao za kwenda 
Bariadi ni pamoja na Wakuu wote wa Mikoa, Wakuu wote wa Wilaya, 
Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mameya na Wenyeviti 
wote wa Halmashauri za Majiji, Manispaa, Miji na Wilaya pamoja na 
watumishi ambao huambatana nao wakiwemo madereva na wasaidizi wao ambao 
kwa idadi hufikia takribani 1,500.
Kwa kuwa sherehe za Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru 
huambatana na Maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Muasisi wa Taifa na 
Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyefariki dunia 
miaka 17 iliyopita, agizo hilo limewataka Viongozi wote wa Mikoa na 
Wilaya kubaki katika maeneo yao ya kazi na kujiwekea utaratibu wa jinsi 
ya kuienzi siku hiyo.
Aidha, Rais Magufuli aliagiza kuwa Wilaya zote ambazo 
zimefanya vizuri katika shughuli za maendeleo wakati Mwenge ulipokuwa 
katika maeneo yao, zitambuliwe kwa kutangazwa rasmi katika siku ya 
kilele cha Mbio za Mwenge na kwamba zawadi zilizoandaliwa zitapelekwa 
kwa wahusika kwa utaratibu utakaoelekezwa na Mamlaka inayohusika kutoa 
zawadi hizo.
Hata hivyo Dkt. Magufuli ameelekeza kuwa kutokana na 
umuhimu wa Mwenge wa Uhuru kwa Taifa, Viongozi wote wa Serikali ya Mkoa 
wa Simiyu na Wilaya zake pamoja na wananchi wote wa mkoa huo wajitokeze 
kwa wingi na kushiriki katika sherehe za kuzima Mwenge wa Uhuru siku 
hiyo ya tarehe 14 Oktoba, 2016.
Mgeni Rasmi katika sherehe za kuzima Mwenge wa Uhuru 
atakuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. 
Ali Mohamed Shein.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni