MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amekabidhi ramani ya jengo 
la Ofisi ya Makao Makuu ya Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), 
ikiwa ni ahadi ya kuwajengea jengo hilo.
Akizungumza wakati akikabidhi ramani hiyo, Makonda alisema jengo hilo 
linatarajiwa kuwa na ghorofa tatu na litagharimu zaidi ya Sh bilioni 
tano.
“Ijumaa nitakuja hapa kwa ajili ya kuweka jiwe la msingi na niseme tu 
ujenzi utaanza hivi karibuni na nimeshawaambia watu wangu wahakikishe 
jengo hilo linajengwa kwa muda usiozidi miezi 14 tu,” alisema Makonda.
Licha ya kukabidhi ramani hiyo, Makonda pia aliwataka viongozi hao wa 
dini kuendelea kuhubiri amani ili taifa liendelee kuwa na amani na 
mshikamano. Alisema ujenzi wa jengo hilo, umekuja baada ya kuona kuwa 
Bakwata imekuwa na mchango mkubwa kwa taifa ikiwemo kuhubiri amani na 
mshikamano.
“Viongozi wa dini ni watu muhimu sana wamekuwa wakituhubiria amani na 
pia viongozi hao wamekuwa wakituongoza katika safari ya kutupeleka kwa 
mola, endeleeni kudumisha na kuihubiri amani ili taifa ili liendelee 
kusifika,” alisema Makonda.
Kwa upande wake, Mufti wa Tanzania, Shehe Mkuu Abubakar bin Zubeir 
alimshukuru Makonda kwa uamuzi alioufanya; na kusema ameonesha njia kwa 
wadau wengine walio na wasio waislamu kujitolea kuchangia.
“Najua jamii inaweza kushangaa kwa nini nimepokea msaada kutoka kwa mtu 
ambaye si Muislamu, lakini niseme tu hata Mtume alipokea misaada kutoka 
kwa watu kama hawa, ni rai yangu kuwaombeni na ninyi Waislamu mjitokeze 
kuunga mkoa juhudi hizi kwa hali na mali,” alisema.
Jisajili kwenye:
Chapisha Maoni (Atom)

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni