Utunzi mahiri wa mashairi na 
ughani uliotukuka wa Mrisho Mpoto, umeligusa sikio la Rais wa Jamhuri wa
 Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli ambaye ameeleza kuwa 
shabiki mkubwa wa kazi za msanii huyo hususan wimbo wake ‘Sizonje’.
Akizungumza na Mpoto jana, muda 
mfupi baada ya kuwasili jijini Dar es Salaam katika Uwanja wa Ndege wa 
Kimataifa wa Julius Nyerere, Rais Magufuli alimueleza msanii huyo kuwa 
anazifahamu vizuri kazi zake na kwamba anaupenda sana wimbo wake wa 
‘Sizonje’ huku akichambua baadhi ya mistari iliyomo kwenye beti za wimbo
 huo.
Mpoto alikuwa msanii pekee 
aliyeongozana na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, Waziri wa Habari, 
Utamaduni, Michezo na Sanaa, Nape Nnauye, Mkuu wa Mkoa wa Dar es  
Salaam, Paul Makonda, Wakuu wote wa Wilaya za Dar es Saalam pamoja na 
viongozi wengine waliofika katika uwanja huo wa ndege kumpokea Mkuu huyo
 wa nchi.
“Nasikiliza nyimbo zako sana, ila 
huu wimbo wako wa Sizonje nimeuelewa sana na nausikiliza kila siku, 
kwangu umekuwa kama wimbo wa taifa, mwanzoni nilipata tabu kuuelewa 
lakini sasa hivi… aaaah, nimeuelewa vizuri sana. Halafu Sizonje namjua, nimtaje?,” yalisikika baadhi ya maneno ya Rais Magufuli kwa Mrisho Mpoto.
Akielezea tukio hilo lililoleta 
msisimko wa aina yake uwanjani hapo, Mpoto alisema kuwa baada ya 
kumsikia Rais ameanza kuusifia wimbo wake alishtuka na kujawa na furaha 
ya aina yake kwani kwa msanii ni jambo la thamani kubwa kusifiwa kazi 
yake na Mkuu wa Nchi.
Alisema kuwa pamoja na kuusifia 
wimbo huo, Rais alionesha kuufahamu vizuri zaidi baada ya kuanza 
kuipitia baadhi ya mistari na kuahidi kumfumbulia fumbo lililofichwa 
kwenye wimbo huo watakapokutana tena.
“Unapopata thamani kutoka kwa Mkuu
 wa Nchi inaleta faraja sana,” amesema Mpoto. “Kwahiyo, mheshimiwa Rais 
leo kuniambia kwamba yeye ni shabiki wa kazi zangu na kwamba anapenda 
sana wimbo wa Sizonje, na akafunguka kwa mistari ‘minane’ ya Sizonje 
ikiwa ni pamoja na ile inayosema ‘huyu mgeni anayepitia madirishani 
wakati milango ipo!’ Na akaniambia siku tukikutana ataniambia vile 
vyumba vitatu kwanini havifunguki,” ameongeza.
Msanii huyo amemshukuru Rais 
Magufuli kwa kuthamini mchango wake katika sanaa kwakuwa anaamini 
kuthaminiwa ni hitaji kubwa la kila msanii.
“Kwakweli leo ni siku yenye furaha
 sana. Najisikia furaha sana. Asante sana mheshimiwa Rais John Pombe 
Magufuli. Umenifanya nimekuwa na siku nzuri sana,” Mpoto amefunguka kwa 
furaha.
Mwaka huu mwanzoni, Mrisho Mpoto 
aliachia audio na video ya ‘Sizonje’ aliomshirikisha Banana Zorro ambapo
 kwa muda mfupi tu, wimbo huo uligeuka kuwa mkubwa na kufanya vizuri. 
Kutokana na ufanisi wa kazi zake, Mpoto ameendelea kukubalika akipata 
mikataba ya ubalozi wa mashirika na taasisi kubwa nchini ikiwa ni pamoja
 na mfuko wa pensheni wa PSPF.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni