HALMASHAURI YA WILAYA YA MONDULI YAINGIA LAWAMANI (3)

Image result for nembo ya halmashauri monduli
Mahmoud Ahmad Monduli

Monduli,Uongozi wa halmashauri ya wilaya ya Monduli mkoani Arusha umeingia lawamani mara baada ya wakazi wa kijiji cha Engeruka kuushutumu ya kwamba umekuwa ukikusanya mapato ya vivutio vya utalii ndani ya kijiji hicho  bila kuwapa gawio lolote pamoja na wao kuwa walinzi wa rasilimali hiyo.

Mapato hayo yanatokana na vivutio vya kihistoria vya  magofu ya Engaruka ambayo yanasadikika kuwa ni mabaki ya makazi ya watu wa zamani ambao waliishi eneo hilo miaka 500 iliyopita.

Akizungumza kwa niaba ya kijiji hicho mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Engaruka Juu,Mohammed Yusuph alisema kwamba pamoja na halmashauri ya Monduli kukusanya mapato mbalimbali kupitia vivutio hivyo lakini kijiji chao hakinufaiki na rasilimali hiyo.

“Tumeshalipigia kelele sana suala hili lakini sisi kama kijiji pamoja na kutunza vivutio hivyo lakini hatunufaiki na chochote “alisema Yusuph

Hatahivyo,alisisitiza kwamba wameshachukua hatua mbalimbali za kufika mbele ya halmashauri hiyo kujua namna  watakavyonufaiki na rasilimali hiyo lakini hadi sasa hakuna majibu ya uhakika.

Hatahivyo,msimamizi mkuu wa eneo hilo la kihistoria,Israel Mollel alisema kwamba uongozi wa halmashauri hiyo uliweka uzio na kutoza kila mtalii kiasi cha $10 sawa na sh,13000 katika maneo ya Engaruka,Gilai na Engaresero kama ada ya kiingilio lakini wao kama wasimamizi hawaambulii  chochote.

Alisema kwambatangu  utaratibu huo uanzishwe umechangia kushuka kwa idadi ya watalii wanaotembelea eneo hilo ambapo miaka ya nyuma walikuwa wakipokea watalii 50 kwa siku lakini kwa sasa hupokea watalii 10 kwa siku.

Akijibu malalamiko hayo mwenyekiti wa halmashauri ya Monduli,Isaack Joseph maarufu kama Kadogoo alisema kwamba hana taarifa kuhusu suala hilo lakini uongozi wake utafuatilia ili kujua kama hawapokei gawio lolote.

Alifafanua kwamba halmashauri yake ilitoa kiasi cha sh,2 milioni kwa kila kata mwaka jana kama gawio la fedha za makusanyo ya vivutio mbalimbali vya utalii na watafuatilia kujua kama fedha hizo zilifika au la.

Hatahivyo,alisema kwamba halmashauri yao kwa kushirikiana na halmashauri za wilaya ya Karatu,Longido na Ngorongoro wameweka utaratibu wa ukusanyaji wa mapato ya vivutio vyote vya utalii vilivyomo ndani ya wilaya hizo ambapo mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro(NCAA) itakuwa ikikusanya mapato hayo kwa utaratibu waliojipangia ili kudhibiti mapato hayo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni