Msimamizi
 Mkuu wa Mradi wa usafirishaji wa umeme mkubwa, maarufu kama ‘Backbone’,
 Mhandisi Khalid James (aliyenyoosha mkono), akitoa maelezo kwa Naibu 
Waziri wa Nishati na Madini Dkt Medard Kalemani (wa pili kutoka 
kulia-mbele), kuhusu upanuzi wa Kituo cha kupoza umeme cha Iringa ili 
kuwezesha Kituo hicho kupokea umeme mkubwa wa Backbone.
Msimamizi
 Mkuu wa Kituo cha kupoza umeme cha Iringa, Theopist Semanini akimweleza
 Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani (wa tatu kutoka 
kushoto), utendaji kazi wa Kituo hicho, wakati wa ziara yake kukagua 
miundombinu ya umeme hivi karibuni.
Ofisa
 anayeshughulikia uangalizi wa Gridi katika Kituo cha kupoza umeme cha 
Iringa, John Havie, akimwonesha Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt 
Medard Kalemani (kulia kwa John) namna anavyoongoza mitambo kupitia 
chumba maalum cha uangalizi (control room).
Naibu
 Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani (kulia) akimweleza 
jambo Mbunge wa Jimbo la Kilolo, Venance Mwamoto (kushoto) walipokutana 
katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa wakati wa ziara ya Naibu Waziri 
kukagua miradi ya umeme mkoani humo hivi karibuni.
Naibu
 Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani (wa tatu kutoka 
kushoto), akitoa maagizo kwa baadhi ya maofisa wa Shirika la Umeme 
Tanzania (Tanesco), wanaosimamia Bwawa la Maji la Mtera mkoani Iringa, 
alipotembelea Bwawa hilo ambalo maji yake hutumika kuzalisha umeme, 
akiwa katika ziara kukagua miradi ya umeme hivi karibuni.
Naibu
 Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani (mwenye Suti ya Bluu –
 Kulia), akizungumza na waandishi wa habari wa Iringa kuhusu 
utekelezwaji wa miradi mbalimbali ya umeme mkoani humo, alipopitia 
katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, akiwa katika ziara ya kukagua miradi 
mbalimbali ya umeme hivi karibuni.
Na Veronica Simba - Njombe
Serikali
 imewataka wakandarasi wanaotekeleza miradi mbalimbali ya umeme hapa 
nchini kuachana na visingizio vya uchelewaji wa fedha kutoka kwa 
wafadhili na badala yake watumie fedha zao kukamilisha miradi hiyo kwa 
wakati.
Naibu
 Waziri wa Nishati na Madini, Dkt Medard Kalemani aliyasema hayo hivi 
karibuni mkoani Njombe akiwa katika ziara kukagua utekelezaji wa miradi 
mbalimbali ya umeme.
Dkt
 Kalemani alisema kuwa, kumekuwepo na tabia ya baadhi ya wakandarasi 
kuchelewesha utekelezaji wa miradi wanayoisimamia kwa kisingizio kuwa 
hawajapokea fedha kutoka kwa wafadhili na hivyo aliwataka kuachana na 
tabia hiyo mara moja.
Alisema,
 mojawapo ya sifa katika kuchagua Mkandarasi ni pamoja na uwezo wake wa 
kifedha katika kutekeleza mradi husika hivyo hakuna sababu ya Mkandarasi
 kuchelewesha kazi kwa kisingizio cha fedha.
“Serikali
 haitavumilia wakandarasi wanaosuasua katika utekelezaji wa miradi 
wanayoisimamia kwa kisingizio cha fedha. Fedha kutoka kwa wafadhili 
inapochelewa, wao watumie fedha zao kwani uhakika wa kulipwa upo,” 
alisisitiza.
Akizungumza
 mara baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa Mradi wa Umeme wa 
Makambako – Songea, Dkt Kalemani aliwataka Maofisa wa Shirika la Umeme 
Tanzania (Tanesco) wanaosimamia miradi mbalimbali ya umeme nchini 
kuhakikisha wanawasimamia wakandarasi ipasavyo ili kukamilisha miradi 
husika kwa wakati na viwango vinavyotakiwa.
Alisema,
 Mradi wa Makambako – Songea ni mojawapo ya Miradi muhimu kwa Taifa, 
hususan kwa wananchi wa maeneo husika hivyo ni lazima ukamilike kwa 
wakati uliopangwa ambao siyo zaidi ya mapema 2018.
Naibu
 Waziri alisema kuwa, matarajio ya Serikali ni kuhakikisha ifikapo mwaka
 2025, vijiji vyote vya Tanzania vinakuwa na umeme hivyo ni lazima 
kufanya kazi kwa bidii ili kufikia malengo hayo.
Awali,
 akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mradi huo, Meneja wa Mradi 
husika, Mhandisi Didas Lyamuya alisema kuwa Mradi wa Makambako – Songea 
unatekelezwa chini ya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (Big Results 
Now-BRN) na unalenga kuunganisha umeme kutoka makambako hadi songea na 
kunufaisha wananchi katika maeneo husika yaani mikoa ya Njombe na 
Ruvuma.
Aidha,
 Mhandisi Lyamuya aliongeza kuwa, Mradi huo ni wa umeme wa kilovolti 220
 kwa umbali wa kilomita 250 na umelenga kuwanufaisha watu 22,700 katika 
vijiji 120 vya maeneo husika.
Naibu
 Waziri Kalemani yupo katika ziara kukagua utekelezaji wa miradi 
mbalimbali ya umeme katika mikoa ya Iringa, Njombe, Katavi na Rukwa. 
Ziara hiyo inatarajiwa kuhitimishwa mwishoni mwa mwezi huu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni