Mwonekano wa barabara ya Airport Jijini Mwanza, katika eneo la Furahisha ambapo upanuzi wa barabara unafanyika hadi eneo la Pasiansi. Na BMG
Utandikaji wa miundombinu ya maji ukiendelea
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, ameagiza utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa daraja la watembea kwa miguu pamoja na upanuzi wa barabara ya Airport kuanzia eneo la Furahisha hadi Pasiansi jijini Mwanza, kukamilika kwa wakati.
Mongella ametoa agizo hilo hii leo, alipofanya ziara ya kukagua utekelezaji wa ujenzi wa miradi hiyo baada ya awali kuwepo kwa changamoto kadhaa ikiwemo miradi kusimama kwa muda ili kupisha uondoaji wa miundombinu mbalimbali barabarani ikiwemo ya maji, umeme pamoja na simu.
Akiwa eneo la ujenzi wa daraja la watembea kwa miguu, Mongella alielezwa kwamba ujenzi wake umekuwa ukisimama kwa muda kutokana na baadhi ya vifaa ikiwemo vyuma vya daraja ambavyo vimeagizwa nchini Uchina kuchelewa kuwasili.
Zoezi la uondoaji wa miundombinu mbalimbali katika eneo la miradi bado linaendelea ili kuruhusu utekelezaji wa miradi hiyo kukamilika kwa wakati, kama anavyobainisha Mhandisi Antony Sanga ambae ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Mkoani Mwanza, Mwauasa.
Pamoja na changamoto hizo, Mhandisi Mushubila Kamuhabwa ambae ni Mhandisi Mshauri wa miradi hiyo kutoka Wakala wa Barabara Tanroads Mkoa wa Mwanza, amesema kwamba miradi hiyo itakamilika kwa wakati.
Ujenzi wa daraja la watembea kwa miguu katika eneo la Furahisha, unatekelezwa na Kampuni ya Nyanza Road Works kwa zaidi ya shilingi bilioni nne ikiwa ni fedha kutoka Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi ambapo Meneja wa kampuni hiyo, Ahabyoona Gilbert, ameahidi kukamilisha kwa wakati ujenzi wake ambao ni hadi kufikia Novemba 26 mwaka huu.
Pia ameahidi kukamilisha kwa wakati upanuzi wa barabara ya Arport kuanzia eneo la Furahisha hadi Pasiansi kwa umbali wa Kilomita mbili ambapo upanuzi huo unagharimu kiasi cha shilingi shilingi bilioni mbili ambazo ni fedha zilizopatikana baada ya Rais Dkt.John Pombe Magufuli kufuta sherehe za Muungani wa Tanganyika na Zanzibar mwaka huu.
Kukamilika kwa upanuzi wa barabara ya Airport kutoka njia mbili hadi nne, kunaelezwa kuleta neema kwa wakazi wa Jiji la Mwanza, ikiwemo kuondokana na msongamano wa magari barabarani.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni