Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad
BARAZA 
Kuu la uongozi la Chama cha Wananchi (CUF) limemchagua kwa kura zote 56 
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad kuwa mgombea wa nafasi ya 
urais wa Zanzibar kwa tiketi ya chama hicho katika uchaguzi mkuu wa 
Oktoba mwaka huu.
Akizungumza
 na waandishi wa habari hapo katika ofisi ndogo ya CUF Shangani mjini 
hapa, Mkurugenzi wa Mipango na Uchaguzi wa chama hicho, Omar Ali Shehe 
alisema maalim amepita bila ya mpinzani katika kinyang’anyiro cha nafasi
 ya urais wa Zanzibar kutokana na imani kubwa ya wanachama wa chama 
hicho dhidi yake.
Alisema 
uamuzi huo sasa utamfanya Maalim Seif kumsubiri mgombea kutoka katika 
Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa ajili ya kinyang’anyiro cha nafasi hiyo.
“Chama 
cha CUF kimebadilisha utaratibu zamani jina la mgombea wa nafasi ya 
urais linaamuliwa na mkutano mkuu wa chama, lakini tumebadilisha maamuzi
 hayo kutokana na gharama kubwa za kuitisha mkutano katika chama 
kichanga kama hiki,” alisema.
Mapema 
Shehe alitangaza majina ya mwisho ya wagombea wa nafasi ya Uwakilishi na
 Ubunge katika chama cha CUF katika majimbo 50 ya Unguja na Pemba.
Katika 
majina hayo yanaonesha kwamba Mbunge wa Mkanyageni, Mohamed Habib Mnyaa 
ambaye aliangushwa katika kura za maoni amerudishwa kuwania nafasi hiyo 
katika jimbo hilo.
Aidha, 
Mbunge wa jimbo la Mji Mkongwe kwa tiketi ya CUF, Mohamed Ibrahim Sanya 
ameondolewa katika kinyang’anyiro hicho na nafasi yake kuchukuliwa na 
mwandishi mkongwe aliyekuwa akifanya kazi katika Shirika la Utangazaji 
la Uingereza (BBC), Ali Saleh.
Sanya 
aliibuka nafasi ya kwanza katika mchakato wa kura za maoni huku 
akimuangusha vibaya kwa kupata kura 21 Ali Saleh ambaye alishika nafasi 
ya tatu.
Mkurugenzi
 wa Mipango na Uchaguzi alipoulizwa kuhusu maamuzi ya Baraza la Kuu la 
Uongozi wa CUF, alisema baadhi ya vigezo muhimu vilipewa kipaumbele cha 
kwanza ikiwemo suala zima la matokeo ya kura za maoni kutoka katika 
majimbo ya uchaguzi kwa wanachama.
Aidha, 
alisema suala la utekelezaji na kukubalika katika jamii ni suala la pili
 ambalo lilizingatiwa kwa lengo la kuona mgombea anafanikiwa na 
kukivusha chama hadi kupata ushindi.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni