CUF yaweka hadharani wagombea Zanzibar

Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad
BARAZA Kuu la uongozi la Chama cha Wananchi (CUF) limemchagua kwa kura zote 56 Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad kuwa mgombea wa nafasi ya urais wa Zanzibar kwa tiketi ya chama hicho katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari hapo katika ofisi ndogo ya CUF Shangani mjini hapa, Mkurugenzi wa Mipango na Uchaguzi wa chama hicho, Omar Ali Shehe alisema maalim amepita bila ya mpinzani katika kinyang’anyiro cha nafasi ya urais wa Zanzibar kutokana na imani kubwa ya wanachama wa chama hicho dhidi yake.

Alisema uamuzi huo sasa utamfanya Maalim Seif kumsubiri mgombea kutoka katika Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa ajili ya kinyang’anyiro cha nafasi hiyo.

“Chama cha CUF kimebadilisha utaratibu zamani jina la mgombea wa nafasi ya urais linaamuliwa na mkutano mkuu wa chama, lakini tumebadilisha maamuzi hayo kutokana na gharama kubwa za kuitisha mkutano katika chama kichanga kama hiki,” alisema.

Mapema Shehe alitangaza majina ya mwisho ya wagombea wa nafasi ya Uwakilishi na Ubunge katika chama cha CUF katika majimbo 50 ya Unguja na Pemba.

Katika majina hayo yanaonesha kwamba Mbunge wa Mkanyageni, Mohamed Habib Mnyaa ambaye aliangushwa katika kura za maoni amerudishwa kuwania nafasi hiyo katika jimbo hilo.

Aidha, Mbunge wa jimbo la Mji Mkongwe kwa tiketi ya CUF, Mohamed Ibrahim Sanya ameondolewa katika kinyang’anyiro hicho na nafasi yake kuchukuliwa na mwandishi mkongwe aliyekuwa akifanya kazi katika Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), Ali Saleh.

Sanya aliibuka nafasi ya kwanza katika mchakato wa kura za maoni huku akimuangusha vibaya kwa kupata kura 21 Ali Saleh ambaye alishika nafasi ya tatu.

Mkurugenzi wa Mipango na Uchaguzi alipoulizwa kuhusu maamuzi ya Baraza la Kuu la Uongozi wa CUF, alisema baadhi ya vigezo muhimu vilipewa kipaumbele cha kwanza ikiwemo suala zima la matokeo ya kura za maoni kutoka katika majimbo ya uchaguzi kwa wanachama.

Aidha, alisema suala la utekelezaji na kukubalika katika jamii ni suala la pili ambalo lilizingatiwa kwa lengo la kuona mgombea anafanikiwa na kukivusha chama hadi kupata ushindi.

“Vipo vigezo tulivipa kipaumbele cha kwanza ikiwemo matokeo ya awali ya kura za maoni za wanachama katika majimbo ya uchaguzi, lakini pia suala zima la utekelezaji na kukubalika katika jamii,” alisema.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni