Balozi Seif Ali Iddi aupongeza Uongozi wa Chama cha Michezo cha Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar

Mwalimu wa Timu ya Mchezo wa Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar {Special Olympic} Maalim Amour Ali Khamis akisoma risala wakati wa hafla fupi ya kukabidhi medali za ushindi kwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kwenye mashindano ya Kitaifa yaliyofanyika Kibaha.
Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Michezo cha Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar Bibi Saada Hamad Ali akimkabidhi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Medali 32 walizopata wachezaji wa Zanzibar katika mashindano ya Kitaifa Mkoani Kibaha.
Balozi Seif akimvisha Medali Mchezaji Fahad Juma Khamis ambae alishinda kwenye mashindano ya Kitaifa yaliyofanyika Mkoani Pwani Tanzania Bara.
Mchezaji Huzaima Haji Ali wa Timu ya Mchezo wa Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar akivishwa Medali na Balozi Seif baada ya kushinda mashindano ya Kibaha Tanzania Bara.
Baadhi ya wachezaji wa Timu ya Mchezo wa Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar wakifuatilia hotuba ya Balozi Seif ambaye hayupo pichani wakati akiwapongeza baada ya kufanya vizuri kwenye mashindano yao. Wa kwanza kutoka kulia ni mchezaji wa soka Mbarak Awesu Moh’d wa Zanzibar aliyebahatika kuwa miongoni mwa Wachezaji wa Tanzania watakaokwenda Nchini Marekani kushiriki mashindano ya Kimataifa.
Balozi Seif akiwa katika picha ya pamoja na wachezaji wa Timu ya Mchezo wa Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar baada ya kuwapongeza kwa kuja na ushindi Zanzibar. Picha na – OMPR – ZNZ.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi ameupongeza Uongozi wa Chama cha Michezo cha Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar {Special Olympic}  kwa jitihada uliochukuwa kwa kuiwezesha Timu ya Zanzibar kurejea na ushindi mkubwa kwenye mashindano ya Taifa yaliyofanyika Kibaha Tanzania.

Alisema jina la Zanzibar tayari linaanza kuibika tena kwenye medani ya Michezo katika Nyanja ya Kimataifa baada ya kufifia katika miaka ya nyuma kutokana na kukosa kutoa wachezaji wenye kiwango kinachokubalika Kimataifa.

Balozi  Seif Ali Iddi alitoa Pongezi hizo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar baada ya kupokea Medani 32  ambazo kati ya hizo 17 za dhahabu, Tano za Fedha na 10 za Shaba walizopata wachezaji wa Zanzibar kwenye mashindano hayo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amefarajika kutokana na ushindi huo na kushawishika kuwavisha nishani hizo baadhi ya wachezaji hao akiwemo Mbarak Awesu Moh’d aliyefanikiwa kuchaguliwa katika Timu ya Taifa ya Tanzania inayotarajiwa kushiriki mashindano ya Kimataifa ya Special Olympic Nchini Marekani Mwezi uajo wa Julai mwaka huu.

Balozi Seif alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Ilani ya Chama cha mwaka 2010 iliyotilia Mkazo Michezo itajitahidi kutoa msukumo katika kuunga mkono michezo hasaya wachezaji vijana wenye mahitaji maalum.

Katika kuunga mkono jitihada za Viongozi na wachezaji hao wa  Special Olympic Balozi Seif alitoa ahadi kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itagharamia Tiketi kwa Mchezaji Mbarak Awesu Moh’d wa Zanzibar aliyebahatika kuwa miongoni mwa Wachezaji wa Tanzania watakaokwenda Nchini Marekani.

Akisoma Risala ya wanamichezo hao Mwalimu wa Timu ya Mchezo wa Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar {Special Olympic}   Maalim Amour Ali Khamis  alisema chama cha Mchezo huo kimesajiliwa Tarehe 12 Oktoba mwaka 2009 kwa lengo la kuendeleza michezo kwa watu wenye akili pungufu.

Maalim Amour alisema ufinyu wa fedha unaokikabili chama cha mchezo huo Zanzibar umechangia kukosa ushiriki sahihi wa wachezaji wa mchezo huo  kwa pande zote mbili za Zanzibar katika mashindano ya Kitaifa.

Mwalimu  huyo wa Timu ya Mchezo wa Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar {Special Olympic} kwa niaba ya Viongozi na wachezaji waliochini ya Chama hicho ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa uamuzi wake wa kuunga Mkono timu yao.

Alisema jitihada hizo za Serikali kwa kushirikiana na wafadhili tofauti kutoka Taasisi za Umma na Watu Binafsi  zimewawezesha Vijana hao wa Zanzibar kushiriki michezo mbali mbali ya Kitaifa na Kimataifa.

Akimkabidhi Medali hizo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi, Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Michezo cha Watu wenye ulemavu wa Akili Zanzibar Bibi Saada Hamad Ali alisema vitendo vya udhalilishaji wanavyofanyiwa watoto wenye ulemavu wa akili hivi sasa vimekithiri mno.

Bibi Saada alisema inasikitisha kuona baadhi ya wasimamizi wa sheria wanakataa ushahidi unaotolewa na wazazi au walezi wa watoto wenye ulemavu wa akili kwa kisingizio kwamba ushahidi kamili haujakamilika.

Alisema jamii inaendelea kushuhudia udhalilishaji huo kwa kuwapa nguvu watu waovu kuendeleza vitendo viovu kutokana na kuelewa kuwa wanaotendewa vitendo hivyo kati yao wanashindwa kujieleza mahakamani kutokana na ulemavu wao.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni