KIWANJA CHA MPIRA MAO TSE TUNG-ZANZIBAR CHAFANYIWA UTAFITI KWAAJILI YA KUJENGWA

Matayarisho ya awali ya maandalizi ya ujenzi wa Kiwanja cha Michezo cha Mao Tse tung kiliopo Mperani Kikwajuni Mjini Zanzibar yameanza rasmi kwa hatua ya utafiti wa uchunguzi wa udongo wa eneo hilo.
Mhandisi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Ali Mbarouk alieleza hayo wakati akimpatia ufafanuzi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliyefanya ziara fupi ya kuangalia matayarisho hayo.
Mhandisi Ali Mbaouk alimueleza Balozi Seif kwamba utafiti huo wa udongo unaofanywa kwa kuchukuwa  aina tofauti  za udongo kwenye vishimo 34 vinavyochimbwa  ndani ya eneo la uwanja huo unatarajiwa kuchukuwa muda wa siku 20.
Alisema udongo huo utafanyia utafiti wa kina na wataalamu waliobobea ambao kukamilikwa kwake watatoa ripoti kamili itakayofuatiwa na utangazaji wa tenda kwa Makampuni yatayokuwa tayari kujenga uwanja huo.
Alifahamisha kwamba ujenzi kamili wa uwanja wa Mao Tse Tung unatarajiwa kuanza rasmi mwezi wa Febuari mwaka 2016 chini ya ufadhili wa Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China.
Akitoa ufafanuzi wa Ramani ya  ujenzi  wa uwanja huo Mhandisi Ali Barouk alimueleza Balozi Seif kwamba uwanja huo utakapomalizika utakuwa na Viwanja viwili vya mchezo wa soka, kimoja kitakachokidhi michezo ya Pete pamoja na  Kikapu.
Alieleza kwamba lipo eneo litakalotengwa maalum kwa michezo mbali mbali ya ndani { INDO GAMES }, Majukwaa ya watazamaji eneo la watu Maarufu { VIP } pamoja na ofisi za watendaji wa uwanja huo.
Akielezea furaha yake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kukamilika kwa uwanja wa huo wa Mao Tse Tung kutasaidia kuupunguzia mzigo mkubwa uwanja wa michezo wa Amani.
Balozi Seif alisema uwanja wa Amani kwa sasa ndio pekee unaobeba michezo yote ya Kimataifa na Kitaifa ,Sherehe tofauti ikiwemo ile kubwa ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na matamasha mbali mbali.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kati kati akisalimiana na wataalamu wa Kichina wanaosimamia utafiti wa udongo katika uwanja wa  Mao Tse Tung katika matayarisho ya awali na maandalizi ya ujenzi wake.
 
 Eneo la Uwanja wa Michezo wa Mao Tse Tung likionekana kuwa katika maandalizi ya awali ya matayarisho ya ujenzi mpya unaotarajiwa kugharamiwa na Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China.
 Gari ya Kijiko likiwa katika harakati za uwekaji sawa eneo la Uwanja wa Mao Tse Tung ili kupatana udongo kwa ajili ya kufanyiwa utafiti wa kina kabla ya kuanza rasmi ujenzi wake.
  Mhandisi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Ali Mbarouk  aliyepo kati kati akimuonyesha  Balozi Seif ramani ya uwanja wa Mao utakavyokuwa baada ya kukamilika ujenzi.
Picha na – OPMR – ZNZ.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni