Mwanasheria atangaza kumvaa Kafulila Kigoma


Mbunge David Kafulila amepata mpinzani katika jimbo la Kigoma kusini
WAKATI mchakato wa kutangaza nia ukiendelea kwa wagombea wa nafasi ya urais nchini, Mwanasheria wa Halmashauri ya wilaya ya Kigoma mkoani Kigoma Iddi Ndabhona ametangaza nia kuwania ubunge katika jimbo la Kigoma Kusini wakati wa uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Akizungumza alipopewa nafasi ya kusalimia wakati wa mkutano mkuu wa wakulima wa tumbaku mkoani Kigoma, Ndabhona amesema kuwa anayo nafasi na uwezo wa kuwatumikia wananchi wa jimbo la Kigoma Kusini na kuwaletea maendeleo.
Kwa sasa jimbo hilo liko chini ya mbunge, David Kafulila kupitia chama cha NCCR – Mageuzi ambaye ameonesha nia ya kugombea tena na mtangaza nia huyo ametangaza kugombea kupitia Chama Cha Mapinduzi. Mwanasheria huyo ambaye ni Mkurugenzi wa kampuni ya uwakili ya Lake Tanganyika Attorney and Law Chambers alisema kuwa iwapo chama chake cha CCM kitampitishia kupitia vikao rasmi ataweza kulirudisha jimbo hilo CCM. Wakati akitangaza nia ya kugombea ubunge katika jimbo la Kigoma Kusini, tayari kamati ya ushauri ya mkoa Kigoma imepitisha azimio la kuligawa jimbo hilo na kupata majimbo mawili ya Buhingu na Uvinza. Kutokana na hali hiyo mwanasheria huyo alisema kuwa iwapo tume ya Taifa ya uchaguzi itaridhia mapendekezo ya kamati ya ushauri ya mkoa Kigoma kuhusu mgawanyo wa majimbo mkoani Kigoma na majimbo hayo kugawanya atagombea kwa jimbo la Uvinza.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni