Mbunge David Kafulila amepata mpinzani katika jimbo la Kigoma kusini
WAKATI 
mchakato wa kutangaza nia ukiendelea kwa wagombea wa nafasi ya urais 
nchini, Mwanasheria wa Halmashauri ya wilaya ya Kigoma mkoani Kigoma 
Iddi Ndabhona ametangaza nia kuwania ubunge katika jimbo la Kigoma 
Kusini wakati wa uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Akizungumza
 alipopewa nafasi ya kusalimia wakati wa mkutano mkuu wa wakulima wa 
tumbaku mkoani Kigoma, Ndabhona amesema kuwa anayo nafasi na uwezo wa 
kuwatumikia wananchi wa jimbo la Kigoma Kusini na kuwaletea maendeleo.
Kwa sasa 
jimbo hilo liko chini ya mbunge, David Kafulila kupitia chama cha NCCR –
 Mageuzi ambaye ameonesha nia ya kugombea tena na mtangaza nia huyo 
ametangaza kugombea kupitia Chama Cha Mapinduzi. Mwanasheria huyo ambaye
 ni Mkurugenzi wa kampuni ya uwakili ya Lake Tanganyika Attorney and Law
 Chambers alisema kuwa iwapo chama chake cha CCM kitampitishia kupitia 
vikao rasmi ataweza kulirudisha jimbo hilo CCM. Wakati akitangaza nia ya
 kugombea ubunge katika jimbo la Kigoma Kusini, tayari kamati ya ushauri
 ya mkoa Kigoma imepitisha azimio la kuligawa jimbo hilo na kupata 
majimbo mawili ya Buhingu na Uvinza. Kutokana na hali hiyo mwanasheria 
huyo alisema kuwa iwapo tume ya Taifa ya uchaguzi itaridhia mapendekezo 
ya kamati ya ushauri ya mkoa Kigoma kuhusu mgawanyo wa majimbo mkoani 
Kigoma na majimbo hayo kugawanya atagombea kwa jimbo la Uvinza.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni