WAZIRI
 wa zamani wa Nishati na Madini Sospeter Muhongo, ametangaza nia rasmi 
ya kuwaomba Wana CCM kumteua kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa 
Tanzania mwezi Oktoba, huku akisema ni yeye pekee mwenye uwezo wa 
kuikwamua nchi katika hali mbaya ya umasikini na ukosefu wa wataalamu, 
hali inayoifanya nchi ishindwe kupiga hatua.
Pamoja
 na mambo mengine, Muhongo alitumia muda mwingi kutoa takwimu hali ya 
umasikini na utajiri kwa wananchi wa Tanzania, bila kusahau baadhi ya 
nchi ambazo zimeweza kupiga hatua kubwa kwa kujikita kwenye kuzalisha 
wataalamu na watafiti, akiwamo yeye, ambaye si tu ni Profesa, bali pia 
amebobea kwenye nishati kwa miaka mingi.
Akizungumza
 kwa kujiamini mbele ya wanachama wa CCM na Watanzania katika Ukumbi wa 
Chuo Kikuu Huria, Musoma Mjini, Profesa Muhongo alisema kwamba anayo 
tiba ya umasikini wa Watanzania kwa kuhakikisha kwamba anatumia utaalamu
 wake kwa kusimamia mambo ya gesi, mafuta, umeme, bila kusahau elimu kwa
 ajili ya kuwakwamua wananchi wake.
“Nchi 
ina upungufu mkubwa wa takwimu hali inayowafanya viongozi washindwe 
kujua namna gani wanaweza kuondoa umasikini na kero zinazowakumba 
wananchi wake, hivyo hata wale wanaosema wanataka uongozi, hawajui 
wangapi wenye uhitaji.
“Ukiacha
 takwimu ambayo kwa Dunia ya sasa ni lazima, nchi yetu lazima ijiamini, 
kuongeza ushindani, kuongeza upendo, bila kusahau rushwa ambayo kwa 
uhakika inapaswa kupigwa vita kwa vitendo ili nchi yetu isonge mbele,” 
alisema Muhongo.
Kuhusu
 uchumi, Profesa Muhongo alisema kwamba ni aibu Tanzania kupitwa 
kiuchumi na Mataifa waliyokuwa nayo sawa, akitolea mfano wan chi za 
Brazil, China, India na Kenya ambao wao wamewekeza kwa kiasi kikubwa 
kwenye elimu na utafiti.
Alisema
 nchi ikiwa na watafiti, wananchi wao hawataishi kwa mashaka, huku 
akisema endapo atapitishwa kuwania nafasi hiyo na kuwa rais wa Tanzania,
 atahakikisha kwamba anakuza uchumi wan chi kutoka asilimia 7.5 hadi 
asilimia 10 na 15 kwa kipindi cha miaka mitano hadi 10 ya urais wake.
“Nimeweza
 kufanya kazi ya gesi na mafuta kwa miaka kadhaa kwenye nchi mbalimbali,
 hivyo hakika kama chaguo ni wataalamu, basi mimi nastahili kwa sababu 
sioni mwingine mwenye uwezo wa kutangaza kuondoa kero za Watanzania na 
jinsi atakavyoziondoa.
“Ndio 
unaweza kusema utaondoa umasikini kwa wananchi au kuongeza mishahara, 
lakini ili hilo liweze kufanikiwa kwa vitendo, ni lazima pia katika 
kipindi cha uongozi wako uweze kukuza uchumi wako kwa kiasi kikubwa, 
bila hivyo hakuna kitu,” alisema Muhongo.
Aidha 
Profesa Muhongo alisema kwamba Duniani kote nchi zimepiga hatua kwa 
kuwekeza kwenye wataalamu na viwanda, hivyo Tanzania inapaswa kuangalia 
namna ya kuwekeza kwenye sekta hizo, bila kusahau sekta ya elimu yenye 
umuhimu mkubwa.
Katika
 hatua nyingine, Profesa Muhongo alisema kwamba akiwa Waziri wa Nishati 
na Madini, ndio mtu ambaye alifanikiwa kwa vitendo kutekeleza ilani ya 
CCM kwa kuhakikisha kwamba vijiji vingi vinapata umeme kwa kuongeza 
bajeti na kusimamia kwa vitendo wakala wa umeme vijijini (REA).
Alisema
 kusudio la kuhakikisha kwamba wananchi wake wanaendelea kupata umeme 
kwa bei nafuu ni kati ya mambo anayoona yanafaa kuongezewa chapuo na 
usimamizi wa aina yake, hivyo mwenye uwezo wa kulitatua hilo ni yeye.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni