Mraghbishi Kootu Tome (wa pili kushoto) akiwa na mtendaji wa 
kijiji Rabie Lebuna (mwenye shati la njano) na Mwenyekiti wa Kijiji, 
Kerry Dukonya (wa pili toka kulia). 
Na Kisuma Mapunda,Loliondo
Sasa ni dhahiri waraghbishi wanatambua majukumu na haki zao ndani 
ya jamii. Uelewa wao umewapa fursa ya kuchukua hatua na kusimamia kile 
wanachoamini kwa manufaa ya wanajamii wanaowatumikia.
Watu hawa wamekuwa mhimili muhimu wa kuleta mabadiliko katika 
maeneo wanayoishi. Lakini inapendeza zaidi kuona waraghbishi hao 
wakijawa na dhamira ya dhati ya kuwatumikia wananchi wao kwa kujitokeza 
kuwania nafasi mbalimbali za uongozi kama ilivyo kwenye Kijiji cha 
Ololosokwani, kilichopo katika tarafa ya Loliondo, wilayani Ngorongoro, 
mkoani Arusha. 
Kijiji hiki kina jumla  ya kaya 1,520 zinazoundwa na vitongoji 
vinne vya kijiji, ambavyo ni Sero, Ololosokwani, Mairowa A na B. Baadhi 
ya wanaounda kaya hizo ni pamoja na waraghbishi wanaofanya kazi na mradi
 wa Chukua Hatua, akiwamo Kootu Tomu, mama wa watoto sita kutoka 
kitongoji cha Mairowa. 
Mraghbishi Kootu Tome (kushoto) akigawa nakala za Riwaya za Chukua
 Hatua kwa baadhi wa wananchi wa kijiji cha Ololosokwani ikiwa kama 
sehemu yake ya uraghbishi. (Picha na Kisuma Mapunda)
Tomu ni mmoja wa waraghbishi wa kwanza kuanza kufanya  kazi na 
mradi wa Chukua Hatua wakiwa na jukumu la  kufuatilia ahadi za wagombea 
wakati wa uchaguzi wa mwaka  2010. Ni katika uraghbishi huu wa 
kufuatilia ahadi zilizokuwa zinatolewa na wagombea, ndipo alipojifunza 
taratibu na kanuni za kuwa kiongozi bora.
Miaka mitano baadaye, alijitokeza katika kinyang’anyiro cha kuomba
 kuchaguliwa na wanachama wenzake wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika 
kura ya ndani ya maoni. Na baada ya hapo alipata fursa ya kupeperusha 
bendera ya chama chake na kuchaguliwa katika uchaguzi uliofanyika mwezi 
Disemba mwaka 2014. 
Mkurugenzi Mtendaji wa PALISEP, Roberth Kamakia,akielezea jambo 
katika mkutano uliokutanisha waraghabishi toka mikoa ya Arusha ,Simiyu 
na Shinyanga uliofanyika hivi karibuni 
Akielezea jinsi ilivyokuwa Kootu Tomu anasema:
“Nilifahamu jukumu lililokuwa mbele yangu katika kusimamia haki 
kwenye migogoro ya ardhi katika eneo letu. Hivyo, katika uchaguzi 
uliopita wa serikali za mitaa niliomba ridhaa ya kuchaguliwa kuwa mjumbe
 wa kijiji kupitia CCM na nilichaguliwa. Sasa naweza kuwafikia wananchi 
wengi zaidi hasa akinamama kupitia fursa hii ya uongozi niliyopata,”
Ndani ya halmashauri ya serikali ya kijiji cha Ololosokwani, 
mraghbishi huyu amechaguliwa kuwa mmoja kati ya wajumbe 9 wanaounda 
kamati ya elimu. 
Akiwa kama mjumbe wa kamati hiyo, anafafanua majukumu yake:
“Moja ya jukumu la kamati yetu ni kusimamia upatikanaji wa ada kwa
 wanafunzi. Kijiji chetu kinapata fedha kutoka idara ya wanyama pori, 
ambazo ndiyo hutumika kulipia ada za watoto kwenye kijiji chetu.” 
Katika kijiji cha Ololosokwani, kila mtoto anapata fursa ya kupata
 elimu kwa kulipiwa gharama stahiki kuanzia ngazi ya shule ya msingi 
hadi kiwango cha shahada ya uzamili. 
Serikali ya kijiji hiki imejiwekea utaratibu wa kuhakikisha 
walengwa wanapata huduma husika na kuhakikisha wanatoa taarifa za 
kweli. 
Akifafanua utaratibu huo, mwenyekiti wa kijiji cha Ololosokwani, Kerry Dukonya anasema:
“Jambo la kwanza ni mwanafunzi kutafuta shule na baada ya kupata 
atatakiwa kuleta fomu na barua ya kukubaliwa kujiunga na shule husika 
kama kielelezo. Barua hiyo ndio inayotoa maelezo ya ada na mahitaji 
mengine ya shule.  Ndipo hapo kamati inafuatilia na kuhakiki taarifa, 
kabla ya kupitishwa na halmashauri ya serikali ya kijiji.”
Waraghbishi wamekuwa msaada mkubwa katika kutimiza majukumu ya 
serikali kwa kuwa mstari wa mbele katika harakati za kuhimiza wananchi 
kutambua haki na majukumu yao katika kijiji. Na viongozi wa kijiji 
wanakiri kwamba waraghbishi wamekuwa wakishawishi wananchi kuchukua 
hatua mbalimbali, ikiwamo kuwawajibisha viongozi wazembe.
Akifafanua hali hiyo na jinsi viongozi wanavyojisikia iwapo 
uraghbishi utagusia masilahi yao hasa linapokuja suala la kuwawajibisha,
 mwenyekiti wa kijiji anasema:
“Sisi kama viongozi, tunamruhusu Kootu kwenda popote na akinamama 
hawa wamekuwa mstari wa mbele kutukosoa na kutukumbusha majukumu yetu. 
Hii ni njia mojawapo ya kuruhusu haki itendeke. Hivyo ni haki ya 
wananchi kujua mapato na matumizi ya serikali yao ambayo sisi kama 
viongozi  tunayasimamia.”
Kama mwanamke ndani ya halmashauri ya serikali ya kijiji, 
amepatiwa jukumu maalumu la kuhakikisha wanawake na wasichana 
wanashiriki katika shughuli za maendeleo.  Akifafanua jambo hilo, 
mwenyekiti wa Ololosokwani, Kerry alisema: 
“Tungependa kuona anakuwa kielelezo cha mwanaharakati mwanamke 
kutokana na nafasi yake kama mjumbe wa halmashauri ya serikali ya 
kijiji. Lakini pia wanawake wamekuwa ni kundi la pembezoni, ikiwamo 
walemavu. Mraghbishi huyu atakuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wenzake 
kutambua umuhimu wa elimu.” 
Mraghbishi Tome, kwa kutumia mbinu za kiuraghbishi, anahakikisha 
watoto wa kike wanakwenda shule. Katika hili, anaeleza anaeleza mikakati
 yake:
“Kama mraghbishi, nimepata fursa ya kukutana na akinamama na 
kuhakikisha watoto wa kike wanapata nafasi za kusoma. Lakini siku zote 
nimekuwa nikiwataka kuwasiliana na walimu ili watambue changamoto 
zinazowakabili watoto wao wa kike, hasa kwa wale ambao wapo mashuleni 
tayari,”
Kwa upande wake, mtendaji wa kijiji Rabia Legula anasema:
“Ninapozungumzia mraghbishi, namaanisha wale wanaohamasisha 
wananchi kudai haki zao za msingi, ikiwamo kuwawajibisha viongozi. Si 
hivyo tu, waraghbishi wamekuwa mstari wa mbele kunisaidia masuala 
yanayohusu wanawake. Kupitia ujuzi wao na kama wanawake waraghbishi 
tunatoa kipaumbele kwa wanawake.”
Katika jamii ya kimasai ambayo bado wanawake hawajapata nafasi ya 
kutosha, uwepo wa waraghbishi wanawake umekuwa chachu nzuri ya 
kuwawezesha wenzao kuongea katika mikutano ya hadhara.
“Tunapenda waraghbishi waendelee kuhamasisha akinamama kuongelea 
masuala yao katika mikutano ya vijiji. Kwa kutumia nafasi yangu ya 
utendaji, nitahakikisha natoa fursa kwa waraghbishi hawa kuzungumza kwa 
uwazi mambo ya  wanawake.” 
Kama mjumbe wa halmashauri ya serikali ya kijiji, mraghbishi 
amekuwa na jukumu la kuhakikisha  wananchi wanahudhuria mikutano ya 
kijiji.
“Huwa nawahamasisha akinamama wenzangu kuhudhuria mikutano ya 
kijiji kila tunapokutana kwenye vikundi vyetu vya ushirikiano,” 
anasema. 
Awamu ya pili ya mradi wa Chukua Hatua, unalenga kuwawezesha 
waraghbishi wa zamani kufundisha waraghbishi wapya waliochaguliwa na 
serikali za kijiji, kama anavyoelezea Mkurugenzi Mtendaji wa PALISEP, 
Roberth Kamakia,
“Tuliwaandikia barua serikali za vijiji tukiwaomba watuchagulie 
watu wanaofaa kuwa waraghbishi. Tuliwapa sifa za watu hao na mwongozo wa
 jinsi ya kuwachagua.
Baada ya waraghbishi hao kuchaguliwa, waliandaliwa kwa ajili ya 
mafunzo ya pamoja ikijumuisha wale wa zamani na wapya. Na baada ya hapo 
waraghbishi wa zamani walikuwa na jukumu la kuwafundisha wenzao jinsi ya
 kufanya uraghbishi. 
Katika mafunzo hayo, walikumbushwa maana ya uraghbishi na sifa za 
uraghbishi. Ndipo wale waraghbishi wa zamani, akiwamo Kootu walipopewa 
jukumu la kufundisha wenzao kwa kutumia uzoefu waliopata wa uraghbishi.
Akielezea jinsi wao waraghbishi wa zamani wanalivyofundisha 
waraghibishi wapya wanaotoka vitongoji vya Ololosokwani na Njoroi, Kootu
 anasema:
“Tulikaa pamoja PALISEP na kuwafundisha waraghbishi wapya. Kwa 
upande wangu, nilifundisha maana ya uraghbishi na kutoa maana ya mtu 
anayeitwa mraghbishi Kazi yake ni kuwahamasisha wananchi. Mraghbishi 
anatakiwa awe na sikio kubwa la kusikiliza, mdomo mdogo wa kuongelea na 
macho makubwa ya kuangalia,” anasema. 
Kootu si mraghbishi pekee aliye kwenye halmashauri ya serikali ya 
Kijiji cha Ololosokwani, mraghbishi mwingine ni Noorkishili Naing’isa ni
 mjumbe wa halmashauri na  kamati ya fedha. Ni dhahiri waraghbishi 
wanawake wameendelea kuwa chachu ya maendeleo kutokana na utendaji wao 
mzuri kwenye serikali za kijiji. Hivyo ni jukumu letu sote kuhakikisha 
harakati hizi za uraghbishi ndani ya halmashauri za vijiji vyetu 
zinaungwa mkono.


Hakuna maoni:
Chapisha Maoni