Na Richard Mwaikenda
NAIBU Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na 
Mawasiliano, Mhandisi Edwin Ngonyani, amepiga marufuku kwa Halmashauri 
zote nchini, kuwatumia wajenzi wa barabara wasiosajiliwa na Bodi ya 
Wahandisi nchini (ERB).
Mhandisi Ngonyaji alichukua hatua hiyo 
alipofanya ziara ya kujua utendaji wa Bodi ya Mfuko wa Barabara nchini, 
Dar es Salaam juzi, ambapo alielezwa na Meneja wa Bodi hiyo, Joseph 
Haule, kuwa barabara nyingi kwenye halmashauri zinajengwa chini ya 
viwango kwani wanaopewa tenda hawana utaalam wa ujenzi wa 
barabara.
Alisema kuwa, kuanzia sasa halmashauri 
ziachane kabisa kuwatumia mafundi wasio na utaalam, bali 
wawatumie wahandisi waliosajiliwa na Bodi ya Wahandisi nchini, ili 
barabara zijengwe kwa viwango vinavyotakiwa, na watakaokaidi agizo hilo 
wanyimwe fedha za mgao kutoka kwenye bodi hiyo.
Pia , Mhandisi Ngonyani, ameitaka bodi 
hiyo, kutokutuma fedha za ujenzi wa barabara kwa 
halmashauri yoyote ambayo imetumia fedha walizopelekewa na kuzitumia 
kinyume cha malengo yaliyokusudiwa.
Amemwagiza Meneja wa Bodi hiyo, 
kuzichukulia hatua halmashauri zote ambazo zimetumia fedha hizo tofauti 
na malengo yake ikiwa ni pamoja na kutopelekewa fedha  hadi 
hapo watakapoziresha walizozitumia.
"Ongezeni nguvu zaidi katika kusimamia 
matumizi ya fedha za mfuko wa barabara kwa halmashauri ambazo fedha hizo
 zinatumiwa kwa shuguli zisizo za barabara", alisisitiza Mhandisi 
Ngonyani.
Naye Meneja wa Bodi ya mfuko huo, Joseph 
Haule, alielezea mafanikio ya mfuko huo tangu ianzishwe  miaka 
 15 iliyopita kwamba kuwa mapato yameongezeka kutoka sh. 
bilioni 73 mwaka 2005 hadi sh bilioni 752.
"Kutokana na kupanda kwa mapato mtandao wa
 barabara umeboreshwa kwa kiwango kikubwa kwa kuwa barabara nyingi 
zimejengwa kutokana na kipato hicho", alisema Meneja 
Haule.
Aidha, Meneja wa Bodi ya mfuko huo, Haule,
 alisema kuwa mfuko huo ambao chanzo chake kikubwa ni 
ukusanyaji wa fedha kutoka sehemu ya mauzo ya mafuta ya petroli na 
dizeli nchini, Bodi italitia mkazo katika ufuatiliaji wa matumizi ya 
mfuko kuhakikisha vyanzo vipya vya mapato 
vinapatikana.
Alisema kuwa, katika kuhakikisha 
ufuatiliaji wa usimamizi wa fedha hizo unatekelezwa, mfuko tayari 
umezichukulia hatua halmashauri tatu zikiwemo za Kinondoni, Songea 
Vijijini na Bukoba Vijinini ambazo zimetumia fedha za mfuko wa barabara 
kinyume na malengo yaliyokusudiwa.
Alisema Bodi ya Mfuko wa Barabara 
ilianzishwa kwa lengo la kukusanya mapato, kufuatilia matumizi ya fedha 
hizo na kugawa kwenye taasisi ambapo asilimia 63 zinapelekwa Wakala wa 
Barabara wa Serikali (Tanroads) kwa ajili ya matengezo barabar kuu na za
 mikoa, asilimia 30 katika halmashauri 166 kwa ajili ya ujenzi wa 
barabara za halmashauri na asilimia 7 zinapelekwa wizara ya 
ujenzi
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni