WAZIRI APIGA MARUFUKUWAHANDISI 'UCHWARA' KUPEWA TENDA ZA UJENZI WA BARABARA


Na Richard Mwaikenda
 
NAIBU Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Edwin Ngonyani, amepiga marufuku kwa Halmashauri zote nchini, kuwatumia wajenzi wa barabara wasiosajiliwa na Bodi ya Wahandisi nchini (ERB).

Mhandisi Ngonyaji alichukua hatua hiyo alipofanya ziara ya kujua utendaji wa Bodi ya Mfuko wa Barabara nchini, Dar es Salaam juzi, ambapo alielezwa na Meneja wa Bodi hiyo, Joseph Haule, kuwa barabara nyingi kwenye halmashauri zinajengwa chini ya viwango kwani wanaopewa tenda hawana utaalam wa ujenzi wa barabara.

Alisema kuwa, kuanzia sasa halmashauri ziachane kabisa kuwatumia mafundi wasio na utaalam, bali wawatumie wahandisi waliosajiliwa na Bodi ya Wahandisi nchini, ili barabara zijengwe kwa viwango vinavyotakiwa, na watakaokaidi agizo hilo wanyimwe fedha za mgao kutoka kwenye bodi hiyo.
 
Pia , Mhandisi Ngonyani, ameitaka bodi hiyo, kutokutuma fedha za ujenzi wa barabara kwa halmashauri yoyote ambayo imetumia fedha walizopelekewa na kuzitumia kinyume cha malengo yaliyokusudiwa.

Amemwagiza Meneja wa Bodi hiyo, kuzichukulia hatua halmashauri zote ambazo zimetumia fedha hizo tofauti na malengo yake ikiwa ni pamoja na kutopelekewa fedha  hadi hapo watakapoziresha walizozitumia.
 
"Ongezeni nguvu zaidi katika kusimamia matumizi ya fedha za mfuko wa barabara kwa halmashauri ambazo fedha hizo zinatumiwa kwa shuguli zisizo za barabara", alisisitiza Mhandisi Ngonyani.

Naye Meneja wa Bodi ya mfuko huo, Joseph Haule, alielezea mafanikio ya mfuko huo tangu ianzishwe  miaka  15 iliyopita kwamba kuwa mapato yameongezeka kutoka sh. bilioni 73 mwaka 2005 hadi sh bilioni 752.

"Kutokana na kupanda kwa mapato mtandao wa barabara umeboreshwa kwa kiwango kikubwa kwa kuwa barabara nyingi zimejengwa kutokana na kipato hicho", alisema Meneja Haule.

Aidha, Meneja wa Bodi ya mfuko huo, Haule, alisema kuwa mfuko huo ambao chanzo chake kikubwa ni ukusanyaji wa fedha kutoka sehemu ya mauzo ya mafuta ya petroli na dizeli nchini, Bodi italitia mkazo katika ufuatiliaji wa matumizi ya mfuko kuhakikisha vyanzo vipya vya mapato vinapatikana.

Alisema kuwa, katika kuhakikisha ufuatiliaji wa usimamizi wa fedha hizo unatekelezwa, mfuko tayari umezichukulia hatua halmashauri tatu zikiwemo za Kinondoni, Songea Vijijini na Bukoba Vijinini ambazo zimetumia fedha za mfuko wa barabara kinyume na malengo yaliyokusudiwa.

Alisema Bodi ya Mfuko wa Barabara ilianzishwa kwa lengo la kukusanya mapato, kufuatilia matumizi ya fedha hizo na kugawa kwenye taasisi ambapo asilimia 63 zinapelekwa Wakala wa Barabara wa Serikali (Tanroads) kwa ajili ya matengezo barabar kuu na za mikoa, asilimia 30 katika halmashauri 166 kwa ajili ya ujenzi wa barabara za halmashauri na asilimia 7 zinapelekwa wizara ya ujenzi

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni