Baadhi
 ya wenyeviti toka Halmashauri ya wilaya ya Kishapu wakimsikiliza 
mkufunzi (hayupo pichani) wakati wa mafunzo ya uraghabishi  
yaliyofanyika wilayani hapo
Na Krantz Mwantepele
“Unakuja
 kwenye ofisi yangu na kutoa taarifa za ubadhirifu wa mtendaji wa 
kijiji. Nakuuliza, je umechukua hatua zipi kama kiongozi wa kijiji kabla
 kuja kwenye ofisi yangu? Unanijibu hapana, hii si sahihi,” 
Hayo 
ni maneno ya mkuu wa wilaya ya Ngorongoro, Hashim Mgandilwa, aliyoyatoa 
wakati wa uzinduzi wa mafunzo ya  wenyeviti wa vijiji, watendaji wa kata
 na vijiji kwenye ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Loliondo, mwezi 
Agosti  mwaka huu.
Alisema
 hayo kwa lengo la kufafanua dhana ya uwajibikaji kwa viongozi kama njia
 muhimu ya kutatua kero zinazowakabili wananchi wa maeneo ya vijijini 
katika wilaya yake.
Ni dhahiri kwamba viongozi wa ngazi za vijiji na kata wanakabiliwa na changamoto mbalimbali za kiutendaji katika maeneo husika. 
Kuna 
nafuu kwa watendaji wa kata na vijiji,  ambao ni waajiriwa wa serikali 
na hupewa kazi kutokana  na miongozo, lakini siyo kwa wenyeviti wa 
vijiji na madiwani, wakati mwingine hata wabunge.
Akielezea
 changamoto hiyo wakati wa mafunzo ya wenyeviti wa vijiji kupitia mradi 
wa Chukua Hatua yaliyofanyika Septemba mwaka huu na shirika mdau la 
CABUIPA, mwenyekiti wa kijiji cha Nyakafulu kilichopo wilaya ya Mbogwe, 
mkoani Geita, Salum Said amesema: 
“Baada
 ya kuchaguliwa kuwa mwenyekiti wa kijiji hiki, hakika sikufahamu vya 
kutosha kuhusu majukumu yangu mapya kama kiongozi. Na hii ni changamoto 
kubwa kwa wenyeviti wa vijiji karibu vyote vya wilaya yetu.” 
Yeye ni mmoja kati ya wenyeviti 200 wanaopatiwa mafunzo katika mikoa ya Shinyanga, Geita na Simiyu. 
Hii ni
 kutokana na ukweli kwamba, katika awamu ya kwanza ya mradi wa Chukua 
Hatua, nguvu kubwa iliwekwa katika kuwawezesha wananchi kuwachukulia 
hatua watendaji na viongozi wabadhirifu wa mali za umma. 
Wakati
 wananchi wakiwezeshwa kuwasimamia viongozi wao, viongozi hawakuwa 
wakiwezeshwa kutimiza majukumu yao kuwasikiliza na kuwahudumia wananchi 
wao.  Hivyo, haja ya kutoa mafunzo kwa viongozi hao ili waweze kutimiza 
majukumu yao kwa wananchi waliowachagua, ilikuwa lazima. 
Akielezea
 umuhimu wa kuwawezesha wenyeviti wa vijiji  wakati wa uzinduzi wa 
mafunzo ya wenyeviti na watendaji wa kata Julai 2015, mkurugenzi 
mtendaji wa Halmashauri  ya Wilaya ya Kishapu, mkoani Shinyanga, Jane 
Mutagurwa alisema:
“Kwa 
muda mrefu wenyeviti mmekuwa mkilalamika kusahaulika kwenye programu 
zetu za mafunzo, fursa ndio hii imekuja. Tunafahamu kwamba wenyeviti 
wetu mnakutana na changamoto nyingi za kiutendaji zinazotokana na 
uwelewa mdogo katika majukumu yenu, hasa kwa wale wanaoingia madarakani 
kwa mara ya kwanza. Hivyo mtumie mafunzo haya vizuri.” 
Pamoja
 na umuhimu wa mafunzo hayo kwa viongozi wa ngazi  ya kijiji na kata, 
bado imekuwa ni changamoto kubwa kwa serikali kuwawezesha wenyeviti 
kujua majukumu yao. Na hii inatokana bajeti kuwa na vipaumbele vingine 
ambavyo halmashauri huwa wamejiwekea katika  kutimiza majukumu yao."
Kwa upande wa Ngorongoro, mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya hiyo mkoani Arusha anaeleza:
“Tangu
 tulipofanya uchaguzi mwaka jana hatujawahi kutoa mafunzo kwa wenyeviti.
 Kwa hiyo tunaunga mkono mafunzo haya yanayotolewa na PALISEP yatasaidia
 sana kwenye kuwawezesha viongozi hawa na watendaji wetu,” 
Kutokana
 na hali hii, wenyeviti wamekuwa na changamoto za kuelewa mipaka ya 
majukumu yao, hivyo muda mwingine hujikuta kwenye mzozo na watendaji wa 
vijiji vyao.  Mwenyekiti anawajibika kwa mwananchi aliyemchagua, wakati 
mtendaji anawajibika kwa mkurugenzi aliyemwajiri.
Kutokana
 na tofauti hizo, mafunzo ya sasa ya wenyeviti na watendaji yanaendeshwa
 kwa pamoja kuwafanya waelewe mipaka yao ya kiutendaji, hivyo kuboresha 
utendaji wao. 
Afisa 
Programu wa CABUIPA, Michael Ikila anafafanua: “Tunawafundisha vitu sita
 muhimu; taratibu za uendeshaji serikali za mitaa, majukumu na haki za  
wenyeviti wa vijiji, uwajibikaji na utawala bora,  mamlaka za vijiji, 
masuala ya fedha, ikiwamo uandaaji wa  bajeti na mawasiliano mazuri 
baina ya viongozi wa  vijiji.” 
Mada hizi ni kwa mujibu wa mwongozo wa wizara ya Tawala za Mikoa and Serikali za Mitaa (TAMISEMI). 
Majukumu
 mengine ya wenyeviti hawa ni pamoja na  kuhamasisha shughuli za 
maendeleo, utawala na  kuhakikisha usalama wa watu katika maeneo yao kwa
 kushirikiana na watendaji wa kata na vijiji. 
Kwa 
upande wa Wilaya ya Ngorongoro, hii ni mara ya kwanza kwa wenyeviti 
kufundishwa majukumu yao. Mwanzoni mafunzo haya yaliwalenga madiwani 
ambao kimsingi hawakuyapenda kwa sababu ya kutokuwapo kwa posho. Hivyo 
mafunzo yao yakaamishiwa kwa wenyeviti wa vijiji ambao walipokea mwaliko
 kwa furaha pasipo kudai posho.
“Mafunzo
 haya yatatusaidia kuboresha mahusiano na utendaji wetu. Mara kadhaa 
unakuta wenyeviti wanaingilia mipaka yetu ya kazi, hivyo kuathiri 
uhamasishaji wa shughuli za maendeleo. Na hii hutokea pale mwenyekiti 
mpya anapotaka kuwaonyesha wapigakura wake kwamba mwenzake aliyepita 
hakufanya kazi,” anaelezea mmoja wa watendaji wa kijiji aliyehudhuria 
mafunzo hayo.
Pamoja
 na changamoto hizo, bado washiriki ambao ni wenyeviti, watendaji wa 
kata na vijiji wamekiri kwamba mafunzo hayo yatakuwa chachu ya kumaliza 
tofauti zinazojitokeza baina yao. 
Lakini
 si hivyo tu, viongozi wa wilaya wameonyesha kuunga mkono mafunzo hayo 
kwa kuwa yanasaidia kuhamasisha wananchi kutimiza majukumu yao.
Lakini
 pia viongozi hao walionyesha umuhimu wa kufikia wajumbe wengi zaidi ya 
halmashauri za serikali ya kijiji. Kwa mfano, wakati akizungumza na 
wakufunzi kwenye ofisi yake, mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya 
Kishapu, alisema:
Halmashauri
 ya Wilaya ya Kishapu ina jumla ya vijiji 117 vyenye wajumbe 2,925. Kwa 
mantiki hiyo, mafunzo haya yanayoendeshwa kupitia mradi wa Chukua Hatua 
yamefikia asilimia 4 tu ya wajumbe wanaounda uongozi wa serikali za 
vijiji, hivyo wengi bado wanahitaji mafunzo. Katika mazingira hayo, 
mkurugenzi alitoa ombi maalumu la kusaidiwa kuwawezesha wakufunzi 25 wa 
wilaya watakaotoa mafunzo kwa wajumbe wa halmashauri za vijiji hivyo. 
Gharama za wakufunzi hawa kuwafikia wajumbe wengine zitakuwa ni za 
serikali. 
Na huu
 ni ushirikiano unaotakiwa baina ya sekta ya umma na binafsi kwa kuwa ni
 jukumu letu sote kwa mustakabali wa maendeleo yetu. 

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni