Waziri
 wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kushoto) akizungumza 
jambo wakati wa ziara yake kwenye kituo cha kuzalisha umeme cha Kidatu. 
Katikati ni Meneja wa Kituo hicho cha Kidatu, Mhandisi Justus Mtolera na
 anayemfuatia ni Meneja wa Kituo cha kuzalisha umeme cha Mtera, Mhandisi
 Abdallah Ikwasa.
Waziri
 wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kushoto) akimsikiliza 
Meneja wa Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Kidatu cha Mkoani Morogoro, 
Mhandisi Justus Mtolera wakati wa ziara yake kituoni hapo lengo likiwa 
ni kujionea uzalishaji umeme wa kituo hicho.
Bwawa la maji la kuendeshea mitambo ya kuzalisha umeme la Kidatu likionekana katika hali ya kupungukiwa na maji.
Serikali
 imeagiza matoleo ya maji ya kumwagilia mashamba  yanayotumia maji ya 
mito inayotiririsha kwenye mabwawa ya kuzalisha umeme ya Mtera na Kidatu
 yafungwe.
Agizo 
hilo limetolewa leo na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter 
Muhongo alipotembelea Bwawa la Kidatu na kujionea namna ambavyo kina cha
 maji kwenye bwawa hilo kilivyopungua.
Waziri
 Muhongo alisema tatizo kubwa la uzalishaji mdogo wa umeme wa maji 
nchini ni umwagiliaji usio zingatia taratibu za matumizi sahihi ya maji.
Alisema
 mfumo wa umwagiliaji unaotumika ni wa kienyeji sio wa kitaalamu. 
"Nimeshuhudia mtu anazuia maji kutiririka kwa kutumia mawe, magogo ama 
viroba vya mchanga; hii sio sahihi," alisema.
Akizungumzia
 umeme unaozalishwa kwa nguvu ya maji, Waziri Muhongo alisema kwa hivi 
sasa ni asilimia ishirini tu inayozalishwa kutoka kwenye vyanzo vya maji
 nchini.
Alisema
 jumla ya uwezo wa mitambo yote ya maji (installed capacity) ni Megawati
  561.84 ambapo wastani wa uzalishaji kwa sasa kutoka kwenye mitambo 
hiyo ni Megawati 110 hiyo ni kuanzia tarehe 13 hadi tarehe 16 mwezi huu.
"Nimetembelea
 Nyumba ya Mungu, Hale, Pangani, Mtera, Kihansi na Kidatu na kugundua 
kwamba tatizo  sugu ni umwagiliaji na siyo tabianchi," alisema.
Alisema mashamba ya umwagiliaji yanaongezeka Mikoani Mbeya, Iringa na Morogoro.
Aliongeza kuwa vibali vya umwagiliaji vimetolewa kienyeji bila kutafakari athari itakayotokea.
Profesa
 Muhongo alisema kipindi hiki ni cha mvua hivyo wenye mashamba ya 
umwagiliaji watumie maji ya mvua badala ya kuendelea kutumia mito.
Alisema
 wakati mazungumzo yanaendelea, Bodi ya Maji- Bonde la Rufiji 
wahakikishe wanakagua mifereji yote ya umwagiliaji inayoingiza maji 
kwenye Mto wa Ruaha mkuu na kuifunga ili kuruhusu bwawa la Mtera kupata 
maji.
Alieleza
 kwamba kwa kufunga mifereji hiyo ndani ya siku nne hadi tano maji 
yatakua yameingia kwenye bwawa la Mtera na hivyo kuweza kuendesha 
mitambo.
Awali 
akimueleza Waziri hali halisi ya uzalishaji umeme kwenye kituo hicho cha
 Kidatu, Meneja wa Kituo, Mhandisi Justus Mtolera alisema umeme 
unaozalishwa kituoni hapo kwa sasa ni megawati 50 wakati kituo hicho 
kinao uwezo wa kuzalisha jumla ya megawati 204.
Mhandisi
 Justus alisema kituo hicho kinayo mitambo minne ya kuzalisha umeme 
lakini kutokana na tatizo la maji, mitambo miwili tu inafanya kazi 
ambapo kila mmoja unazalisha kiasi cha Megawati 25.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni