Serikali imeridhishwa na maendeleo na kasi ya ujenzi wa 
Mahakama ya Kimataifa ya Umoja wa Mataifa ya Masalia ya kesi za Mauaji 
ya Kimbari ya Rwanda (Mechanism for International Criminal Tribunals 
(MICT) katika eneo la Lakilaki jijini Arusha, uliozinduliwa rasmi Julai 
mosi mwaka huu.
 Akikagua ujenzi huo na 
kupokea taarifa kutoka kwa wakandarasi na wasimamizi wa ujenzi wa 
majengo hayo, Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, 
Kikanda na Kimataifa Mheshimiwa Dkt. Augustine Mahiga, amesisitiza kuwa 
ujenzi huo uzingatie viwango vya kimataifa ili kuhakikisha usalama wa 
nyaraka na ushahidi utakaohifadhiwa kwenye majengo hayo.
Alieleza kuwa
 ahadi ya Serikali iko palepale kushirikiana na Umoja wa Mataifa na 
kuhakikisha kuwa miundombinu muhimu kama vile barabara, umeme na maji 
vinapatikana kwenye eneo hilo ambapo ujenzi unaendelea kwa kasi ya 
kuridhisha.
“Nimefurahishwa na maendeleo ya ujenzi huu kwani 
hii ilikua kazi yangu ya mwisho nilipokuwa mwakilishi wa kudumu wa 
Tanzania kule Umoja wa Mataifa, kutetea mahakama hii ijengwe hapa 
Arusha.
Akifafanua miundombinu 
iliyowekwa na Serikali ya Mkoa wa Arusha, Katibu Tawala Msaidizi upande 
wa miundombinu Nd. Hamdouny Mansour alisema kuwa kwa upande wa 
upatikanaji wa maji, mkoa umefanikisha upatikanaji wa bomba maalum 
linaloleta maji kwenye eneo la ujenzi mojakwamoja bila kuathiri 
upatikanaji wa maji maeneo mengine pembezoni ili kutimiza azma hiyo ya 
Serikali.
Ujenzi huo wa Mahakama 
unaosimamiwa na Umoja wa Mataifa unatarajiwa kuwa na majengo makuu 
manne; jengo la mahakama, jengo la uhifadhi wa nyaraka, jengo la ulinzi 
na jengo la ofisi za Umoja wa Mataifa. Msimamizi wa ujenzi wa Umoja wa 
Mataifa alielezea teknolojia ya kisasa itakayotumika kujenga jengo la 
kuhifanyia nyaraka haitahitaji kutumia viyoyozi ili kuhifadhi uhasilia 
wa nyaraka.
Kwa upande wa wakandarasi 
wanaojenga ambao ni kampuni kutoka India walielezea changamoto iliyopo 
kwenye ujenzi huo ni kutekeleza mpango wa kupanda mti aina ya 
mshita-acacia, utakaomaanisha haki ambayo kihistoria na jadi za kiafrika
 ilipatikana kwa mazungumzo kwenye mabaraza ya kijiji. Mti huo wa mshita
 au Tree of Justice utapandwa ndani katikati ya majengo hayo manne.
 Serikali kupitia Hazina 
ilinunua eneo hilo la Lakilaki lenye ekari 431 na kukabidhiwa Wizara ya 
Mambo ya Nje ambapo limetengwa mahsusi kwa ajili ya ujenzi wa taasisi 
mbalimbali za kimataifa. Taasisi nyingine zinazotarajiwa kujengwa kwenye
 eneo hilo ni African Union Advisory Board on Corruption (AUABC), 
African Institute of International Law (AIIL) na African Court on Human 
and Peoples' Rights 
(ACHPR).
 Ujenzi wa majengo haya ya 
awali kwenye eneo la Lakilaki unatarajiwa kukamilika mwezi Aprili 
mwakani. Ujenzi huo ulizinduliwa rasmi Julai mwaka huu wa 2015 na Rais 
wa Awamu ya Nne Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete.MWISHO.
Kitengo cha Mawasiliano ya 
Serikali kwa Umma, Wizara ya Mambo ya Nje na 
Ushirikiano wa Kimataifa.





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni