WAZIRI
 MKUU Kassim Majaliwa amepiga marufuku chakula cha msaada kutumiwa 
kutengeneza pombe za kienyeji na kwamba atakayekamatwa atachukuliwa 
hatua za kinidhamu. 
 
Ametoa
 kauli hiyo wakati akizungumza kwa nyakati tofauti kwenye mikutano ya 
hadhara iliyofanyika leo (Jumatatu, Desemba 21, 2015) kwenye vijiji vya 
Nangurugai, Machang’anja na Narungombe katika kata za Mbwemkuru na 
Narungombe wilayani Ruangwa, mkoani Lindi. 
  Waziri Mkuu alikuwa
 akijibu hoja za diwani wa Narungombe, Bw. Rashid Nakumbya aliyetoa ombi
 la kuongezewa chakula cha msaada kwa sababu wana hali mbaya. Alisema 
msimu uliopita haukuwa mzuri kiuzalishaji kutokana na hali mbaya ya 
hewa. Pia aliomba wasaidiwe kuboreshewa huduma za maji safi na salama. 
  “Natambua kuwa kuna tani 2,000 za chakula zimeletwa katika mkoa wetu 
lakini hizo hazitoshi kwa sababu mahitaji yetu ni zaidi ya tani 5,000. 
Chakula hiki hakitoshi kwa sasa lakini kitasaidia kupunguza makali ya 
njaa,” aliwaeleza wakazi hao. 
  “Tumepiga marufuku kutumia 
chakula cha msaada kupikia pombe. Mwananchi atakayekutwa akitumia 
chakula hicho, atachukuliwa hatua za kinidhamu,” alisisitiza. 
  
Alitumia fursa hiyo kuwahakikishia kauli ya Rais Dk. John Pombe Magufuli
 kwamba hakuna mwananchi atakayekufa kwa njaa. “Mheshimiwa Rais ameahidi
 kuwa hakuna Mtanzania atakayekufa kwa njaa. Tuna mahindi ya kutosha 
kwenye maghala ya Songea, Dodoma na Makambako lakini changamoto ni namna
 ya kuyasafirisha kutoka huko hadi kuyafikisha huku. Tunaendelea pia 
kupeleka misaada kwenye mikoa mingine,” alisema Waziri Mkuu. 
  
Akijibu hoja nyingine zilizotolewa, Waziri Mkuu ambaye pia ni mbunge wa 
jimbo hilo alisema anatambua changamoto walizonazo za ukosefu wa maji 
safi, ubovu wa barabara, zahanati na nyumba za waganga na kwamba ameanza
 kuzishughulikia. 
  “Hivi sasa nimeanza kushughulikia suala la 
uwekaji wa nishati ya umeme wa jua kwenye shule za msingi na zahanati. 
Mtaalam ameshafika hapa wilayani kwetu na ameanza hiyo kazi, na hivi 
karibuni mtamuona akifika maeneo ya huku,” alisema. 
  Kuhusu 
maji safi na salama, Waziri Mkuu aliwaeleza wakazi hao kwamba tatizo la 
maji analijua na kwamba changamoto kubwa waliyonayo ni upatikanaji wa 
chanzo cha maji baridi kwani kiasi kikubwa eneo hilo lina vyanzo vya 
maji yenye chumvi. “Wataalamu wanakuja kutafuta chanzo cha maji baridi 
kwa sababu asilimia kubwa ya eneo hili maji yake yana chumvi,” alisema. 
  Aliwataka wakazi hao waendelee kuwaombea yeye pamoja na Rais Magufuli 
na Makamu wake, Samia Suluhu Hassan ili waweze kutimiza malengo 
waliyoahidi kwa Watanzania wakati wa kampeni. 
Jisajili kwenye:
Chapisha Maoni (Atom)

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni