Katibu
 Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Mhandisi Omar Chambo (wa kwanza kulia)
 akiangalia moja ya mashine zinazotumika katika shughuli za uchimbaji 
madini katika eneo la Mirelani mkoani Manyara wakati alipotembelea eneo 
hilo mara baada ya kumaliza kikao kikao chake na Kamati za Ulinzi na 
Usalama za mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara ambazo zimeamua 
kufanya kazi kwa pamoja ili kudhibiti utoroshaji wa madini ya Tanzanite.
Katibu
 Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Mhandisi Omar Chambo (wa pili kulia) 
akitembelea baadhi ya vitalu vya uchimbaji madini ya Tanzanite katika 
eneo la Mirelani mkoani Manyara mara baada ya kumaliza kikao kikao chake
 na Kamati za Ulinzi na Usalama za mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na 
Manyara ambazo zimeamua kufanya kazi kwa pamoja ili kudhibiti utoroshaji
 wa madini ya Tanzanite.Kulia kwake ni Afisa Madini Mkazi katika Ofisi 
ya Madini Mirelani, Mhandisi Henry Mditi.
Makamishna
 Wasaidizi wa Madini,Wizara ya Nishati na Madini, kutoka kulia ni Julius
 Sarota (Wachimbaji Wadogo), Latifa Mtoro (Uthaminishaji madini), Salim 
Salim (Uchumi na Biashara) pamoja na Mkurugenzi wa Sheria, Justus 
Mulokozi (wa kwanza kushoto) wakiwa katika kikao kilichojumuisha Kamati 
za Ulinzi na Usalama za mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara (hawapo 
pichani) ambazo zimeamua kufanya kazi kwa pamoja ili kudhibiti 
utoroshaji wa madini ya Tanzanite nje ya nchi.
Mwenyekiti
 wa Kamati za Ulinzi na Usalama za mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na 
Manyara na Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Amos Makalla (aliyesimama) 
akizungumza na wajumbe wa Kamati za Ulinzi na Usalama za mikoa ya 
Arusha, Kilimanjaro na Manyara (hawapo pichani) ambazo zimeamua kufanya 
kazi kwa pamoja ili kudhibiti utoroshaji wa madini ya Tanzanite nje ya 
nchi. Wa kwanza kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, 
Mhandisi Omar Chambo, wa kwanza kulia ni Katibu Tawala mkoa wa Manyara, 
Eliakim Maswi na wa pili kutoka kulia ni Mkuu wa mkoa wa Arusha, Daud 
Ntibenda.
Katibu
 Mkuu Wizara ya Nishati na Madini Mhandisi Omar Chambo (wa kwanza kulia)
 akizungumza na baadhi ya wajumbe wa Kamati za Ulinzi na Usalama za 
mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara ambazo zimeamua kufanya kazi kwa
 pamoja ili kudhibiti utoroshaji wa madini ya Tanzanite nje ya nchi.
Afisa
 Madini Mkazi katika Ofisi ya Madini Mirelani, Mhandisi Henry Mditi 
akitoa taarifa ya kazi zinazofanywa na Ofisi hiyo iliyopo katika wilaya 
ya Simanjiro mkoani Manyara.Wanaosikiliza ni Katibu Mkuu Wizara ya 
Nishati na Madini, Mhandisi Omar Chambo (wa pili kushoto), Wa kwanza 
kushoto ni Kaimu Kamishna wa Madini, Mhandisi Ally Samaje. Wengine 
katika picha ni Kamishna Msaidizi wa Madini sehemu ya Uthaminishaji 
Madini, Latifa Mtoro (wa kwanza kulia) na wa pili kulia ni Mkurugenzi wa
 Taasisi ya Uunganishaji na Ushirikishi Wadau katika Tasnia ya Uziduaji 
(EISF), Catherine Lyombe.
Na Teresia Mhagama na Asteria Muhozya
Katibu
 Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Mhandisi Omar Chambo ameeleza kuwa 
 madini aina ya Tanzanite yaliyokamatwa yakitoroshwa nje ya nchi bila 
kuwa na vibali tarehe 15 Desemba, 2015  kupitia uwanja wa ndege wa 
Kilimanjaro (KIA) yamefikia  thamani ya Dola za Marekani milioni 
1,207,990.
Katibu
 Mkuu alisema hayo jijini Arusha wakati wa kikao chake na Kamati za 
Ulinzi na Usalama za mikoa ya  Arusha, Kilimanjaro na Manyara ambazo 
zimeamua kufanya kazi kwa pamoja ili kudhibiti utoroshaji wa madini ya 
Tanzanite na kufuatilia kwa karibu shughuli za uchimbaji na biashara ya 
madini hayo ili  yanufaishe taifa.
Katibu
 Mkuu alisema kuwa Tanzanite hiyo ghafi yenye uzito wa gramu 2,015.59 
ilikuwa ikitoroshwa na raia wa India, Jain Anurag aliyekuwa akitaka 
kuelekea mji wa Jaipur kwa kutumia shirika la ndege la Qatar.
“Nataka
 niwaeleze watanzania wanaoshirikiana na raia wa kigeni kutorosha 
Tanzanite kuwa wajiepushe na biashara hii haramu  kwani hatua kali 
zitaendelea kuchukuliwa dhidi yao na hatuna mzaha katika hili,” alisema 
Mhandisi Chambo.
Alieleza
 kuwa madini hayo  yaliyokamatwa yameshataifishwa  kama ambavyo sheria 
na kanuni za madini zinavyoelekeza na kwamba zoezi hilo la ukamataji 
watorosha madini hufanywa na Wizara ya Nishati na Madini kupitia Wakala 
wake wa Ukaguzi wa Madini (TMAA) kwa kushirikina na Taasisi nyingine 
kama Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, Jeshi la Polisi, Idara ya Usalama wa 
Taifa, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Idara ya Uhamiaji.
Aidha
 alieleza  kuwa serikali itafuta leseni za wafanyabiashara wa madini 
watakaobainika kutorosha rasilimali hiyo nje ya nchi ikiwemo kuwakamata 
wachimbaji na wafanyabiashara wanaokwepa kulipa kodi stahiki kwa 
serikali.
“Ili
 kudhibiti utoroshaji madini unaofanywa na wafanyabiashara wenye leseni 
na wasio na leseni, wazawa na wasio wazawa, tumeshajipanga kwa 
kushirikiana na Kamati za Ulinzi na Usalama za mikoa mitatu ya Manyara, 
Kilimanjaro na Arusha ili kudhibiti hali hii na Tanzania ibaki kama 
kinara katika uzalishaji na uuzaji wa madini haya na sio nchi nyingine,”
 alisema Mhandisi Chambo.
Kuhusu
 wachimbaji wadogo nchini, alisema kuwa serikali itaendelea kugawa 
maeneo ya uchimbaji madini kwa wachimbaji hao ikiwa ni pamoja na utoaji 
ruzuku, uagizaji wa zana kama baruti na utoaji wa mafunzo huku akitoa 
angalizo kuwa  wachimbaji hao wanapaswa kuwa waaminifu na kuhakikisha 
kuwa wanalipa kodi stahiki serikalini badala ya kusubiri kuchukuliwa 
hatua za kisheria.
Wakati
 huohuo Mwenyekiti wa Kamati za Ulinzi na Usalama za mikoa ya  Arusha, 
Kilimanjaro na Manyara na Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Amos Makalla 
ametoa masaa 24 kwa raia wa kigeni wote wanaojihusisha na biashara ya 
madini ya Tanzanite na madini mengine kinyume cha sheria kuondoka nchini
 mara moja na watakaokaidi agizo hilo watachukuliwa hatua kali za 
kisheria.
Agizo
 hilo alilitoa baada ya Kamati hiyo kubaini kwamba uwepo wa wageni 
mbalimbali kutoka nje ya nchi hususani Kenya, Sri Lanka, Nepal na India 
ambao hujihusisha na biashara ya Tanzanite bila kuwa na leseni 
zinazowaruhusu kufanya hivyo na hatimaye hutorosha madini hayo kwenda 
nje ya nchi.
“Madini
 haya yanauzwa kama njugu hivyo tumeona kwamba sisi Kamati za Ulinzi na 
Usalama za mikoa hii mitatu tukishirikiana kuimarisha ulinzi tutakomesha
 suala hili, tunataka kuona watu watu wanaouza madini ni wale wenye 
leseni tu, na wachimbaji na wafanyabiashara wahakikishe wanalipa kodi 
stahiki kwani kuanzia tarehe Tano Januari operesheni ya kuwakamata 
itaanza,” alisema Makalla.
Vilevile
 alieleza kuwa wafanyakazi wa kigeni waliopo katika mgodi wa Tanzanite 
One unaomilikuwa na kampuni ya Sky Associates kwa kushirikiana na 
serikali  ambao hawana vibali vya kufanya kazi na wale wenye vibali vya 
kufanya kazi ambazo zingeweza kufanywa na watanzania waondoke mgodini 
hapo.
“Mchango
 wa madini katika Pato la Taifa bado hauridhishi na sisi tunafanya kila 
jitihada ili Tanzanite hii ambayo inachimbwa Tanzania peke yake 
ifaidishe nchi, kila mwananchi anao wajibu wa kuhakikisha hili 
linafanikiwa, wadau wa madini wana wajibu wa kuhakikisha kwamba wanalipa
 kodi stahiki na kutoa taarifa za hujuma zozote zinazofanyika ambazo 
baadhi ya wazawa wanashirikiana na wageni kuiibia nchi rasilimali hii 
muhimu,” alisema Makalla.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni