HATIMA YA MWILI WA MAWAZO KUAGWA AMA KUTOAGWA JIJINI MWANZA KUJULIKANA LEO

                                           Na:George Binagi-GB Pazzo wa Binagi Media Group

Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza jana imeahirisha kesi ya madai ya kuomba ridhaa ya kufanya ibada ya Mazishi ya aliekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema Mkoani Geita Marehemu Alphonce Mawazo iliyowasilishwa na Mchungaji Charles Lugiko ambae ni baba mlezi
wa marehemu Mawazo.
 

Katika kesi hiyo, mlalamikaji anaiomba mahakama kuondoa zuio la jeshi la polisi Mkoani Mwanza la kutoruhusu shughuli ya kuuaga mwili wa marehemu Mawazo kufanyika Jijini Mwanza, kabla ya kwenda kuzikwa Mkoani Geita.

John Mallya ambae ni miongoni mwa Mawakili watatu wa Chadema ambao wanaitetea kesi hiyo, amebainisha kuwa Mahakama imeahirisha kesi hiyo hadi leo majira ya saa saba mchana, ambapo Jaji wa Mahakama hiyo Mhe.Lameck Mlacha anatarajiwa kutoa maamuzi yake baada ya leo kusikiliza utetezi wa pande zote mbili zinazohusika.

Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema bara Salum Mwalimu, amewasihi wanafamilia pamoja na wafuasi wa chama hicho kuendelea kuwa watulivu, wakati maamuzi ya mahakama hiyo yakisubiriwa ambapo ameeleza kuridhika na mwenendo wa kesi hiyo.

Nje ya Mahakama, ulinzi ulikuwa umeimarishwa zaidi ambapo kulikuwa na polisi pamoja na mbwa ambapo baada ya kesi hiyo kuahirishwa, umati mkubwa wa wananchi uliokuwa umetanda mita chache kutoka Mahakamani hapo ulianza kuimba nyimbo za maombolezo na kuwasindikiza viongozi mbalimbali wa chedema hadi katika hoteli waliyofikia.

John Mallya ambae ni mmoja wa Mawakili wa Chadema akizungumza baada ya kesi kuahirishwa
Katibu Mkuu Msaidizi Chadema bara, Salum Mwalimu akizungumza baada ya kesi kuahirishwa

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni