CHAMA cha Mapinduzi wilaya ya Arusha kimesema kuwa kitaanika hadharani
majina yote ya viongozi na wanachama wasaliti wa chama hicho ikiwemo
kuwachukulia hatua za kuwafukuza uanachama wa chama hicho kwani
kuendelea kuwepo kwao kunakimaliza chama hicho.
Wakizungumza na waandishi wa habari , jana Mbunge wa viti maalumu
mkoa wa Arusha na Mjumbe wa baraza la Mkoa, Catherine Magige alisema
kuwa, hivi sasa chama hicho kinafanya uchunguzi wa kina katika
kuwabaini wasaliti wote wa chama hicho ambao
wamekuwa wakikihujumu chama na kufanya kampeni za vyama vya
upinzani.
Alisema kuwa, ni bora chama hicho kibaki na viongozi na wanachama
wachache ambao wana mapenzi mema na chama hicho kuliko kubaki na
wanafiki wanaokihujumu chama kwa siri , kwani hivi sasa hawapo
tayari kufanya kazi na mamluki tena, na kuwa muda sio mrefu wataanikwa
hadharani .
Magige aliyasema hayo ikiwa ni siku chache tu, aliyekuwa Mwenyekiti wa
UWT wilaya ya Arusha mjini , Vicky Mollel ahamie Chadema na kusema
kuwa ,kuhama kwake hakujaleta pigo lolote kwa chama hicho kwani
walishamwandikia barua ya onyo muda mrefu kutokana na tabia yake ya
kukisaliti chama kwa muda mrefu.
‘kitendo cha Mwenyekiti huyo kuhama chama hakuja leta madhara yoyote
zaidi ya nafasi yake kuwa wazi,lakini kwa maana ya utendaji wake hakuna
pengo lolote , tena tunasema kuwa amechelewa kuondoka kwa kuwa muda
mrefu amekuwa msaliti kwa chama chetu tangu kumalizika kwa mchakato wa
kupatikana kwa mgombea wa Urais wa chama chetu Dokta John Pombe
Magufuli’alisema Magige.
Katibu wa CCM wilaya ya Arusha mjini, Feruz Bano alisema kuwa,
kuondoka kwa mwenyekiti huyo amelazimika kutokana na ukweli kwamba
alishafahamu kwamba amebainika kuwa ni mamluki na alikuwa akiendelea
kuchunguzwa ili hatua zichukuliwe dhidi
yake juu ya usaliti aliokuwa akiendelea kuufanya.
Bano alisema kuwa,mnamo novemba 25 mwaka huu mwenyekiti huyo alipewa
barua ya kumtaka kutoshiriki kampeni za ubunge wa jimbo la Arusha
zinazoendelea kutokana na kufanya hujuma mbalimbali dhidi ya chama.
‘chama chetu kwa ujumla kimefurahishwa sana na kitendo chake hicho
na bado tunatoa wito kwa wote wanaojitambua kuwa ni mamluki wa CCM
waondoke kabla ya kuondolewa kwa kuwa kazi ya kuwachunguza vitendo
vyao inaendelea na hatua kali zitachukuliwa ikiwemo kunyang’anywa kadi
ya uachama’alisema Bano.
Katibu wa UWT mkoa wa Arusha, Fatuma Tsea alisema kuwa ,kuondoka kwa
Mwenyekiti huyo kwa ujumla hakujaleta pigo lolote na hakuna taarifa
yoyote ya wanawake wengine wanaofuatana naye kwani alikuwa
anajulikana kwa muda mrefu kuwa ni msaliti wa chama hicho .
Alisema kuwa,wanatambua bado kuna mamluki waliobaki ndani ya chama
hicho , hivyo aliwataka waondoke kwa kuwa kasi ya chama cha Mapinduzi
kwa sasa hawataiweza chini ya kauli mbiu ya ‘Hapa kazi tu’,hivyo
aliwataka wanachama wa chama hicho kutovunjika moyo wala kushtushwa na
wanaokimbia chama kwani hayo ni mambo yanayotarajiwa kutokana na kazi
inayofanywa ya kusafisha chama.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni