UCHUKUZI SPORT CLUB YAPONGEZWA KWA KUWA NA WACHEZAJI WENGI KATIKA MICHEZO YA MEI MOSI

                                                                                        Na Mwandishi Wetu, Dodoma

MKUU wa mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbana ameipongeza timu ya Uchukuzi SC kwa kuleta wachezaji wengi kwenye mashindano ya Mei Mosi yaliyoanza Aprili 18 mwaka huu kwenye uwanja wa Jamhuri Dodoma.

Mh. Rugimbana katika hotuba ya ufunguzi wa mashindano hayo iliyosomwa jana na Afisa Maendeleo Vijana wa ofisi ya mkuu wa mkoa, Tumsifu Mwasambale kwa niaba yake, alisema kuwa amedokezwa na waandaaji kuwa Uchukuzi SC ndio timu pekee iliyoweza kuleta wachezaji wengi, hivyo anawapongeza viongozi wao.

“Ninaipongeza Uchukuzi SC pamoja na kudokezwa pia nimeona kwa macho yangu wakati wa maandamano ya timu zikiingia uwanjani kuwa Uchukuzi SC ndio wenye wachezaji wengi zaidi, nawapongeza sana viongozi wao, wanatambua umuhimu wa michezo mahala pa kazi,” alisema.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa timu ya Uchukuzi SC, Alex Temba amesema timu yake imekuja na wachezaji takribani 96 ambao watashiriki kwenye michezo ya kuvuta kamba, netiboli, riadha, kuendesha baiskeli, soka, bao, karata na darts.

Tayari timu hiyo inayoundwa na wachezaji kutoka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA), Bandari (TPA), Anga (TCAA), Hali ya Hewa (TMA) na Chuo cha Bandari (DMI), imeshinda kwenye mechi zake za soka dhidi ya Ukaguzi magoli 3-1 na upande wa netiboli waliwafunga CDA magoli 23-15.

Hatahivyo, Mh. Rugimbana aliwashutumu na kusema sababu zilizotolewa na viongozi hao kuzuia timu zao kushiriki kwenye mashindano ya mwaka huu kwa kisingizio cha Mh. Rais John Magufuli kuzuia michezo hii, hazina mashiko na ni kisingizio kilichopaswa kukemewa vikali.

Alisema hajawahi kumsikia Mh. Rais Magufuli akizuia michezo ya Mei Mosi, na mingine yeyote bali walimsikia akitoa maelekezo ya kuzuia sherehe za Uhuru na sasa Muungano, na kutoa maelekezo na tayari yanmefatwa kwa ufanisi mkubwa na wahusika.

“Ni uoga usiokuwa na mashiko, kwani hata ingekuwa Mh Rais kazuia michezo, hata Mh. Waziri Mkuu (Kassim Majaliwa) asingekuwa na nguvy ya kukutana na viongozi wa mashirikisho na vyama vya michezo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, takribani miezi mitatu iliyopita wakijadili uimarishaji wa michezo, na walaumu sana viongozi waliowanyima haki wanamichezo kushiriki kwenye michezo hii,” alisema Rugimbana.

Mashindano ya mwaka huu yenye kauli mbiu ya hapa kazi tu isiwe kisingizio kwa waajiri kuondoa michezo kazini, yamekuwa na idadi ndogo ya washiriki, ambapo hadi jana ni timu 14 pekee ndizo zilizofika Dodoma.

Hatahivyo, awali Kaimu Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mei Mosi, Joyce Benjamin, naye katika hotuba ya ufunguzi aliwalaumu viongozi kuzuia timu zao kwa kumsingizia Mh. Rais kuwa amezuia michezo.

“Kumbukeni Mh. Rais wetu ni mmoja wa wanamichezo na ndio maana hata wakati wa kampeni tulimuona wote akipiga pushapu jukwaani, sasa iweje leo hii viongozi wa sehemu za kazi waseme amekataza michezo, michezo huu ni mikubwa imepata Baraka zote kutoka TUCTA (Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi) na Baraza la Michezo la Taifa (BMT),” alisema Benjamin.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni