WALIOKUWA wafanyakazi wa mahakama ya kimataifa ya mauaji ya kimbari ya Rwanda, UN –ICTR, ambayo imemaliza kazi yake , wameishitaki mahakama hiyo kwenye mahakama ya kazi wakidai kutolipwa stahiki zao.
Wafanyakazi hao wakizungumza kwenye ofisi ya Idara ya kazi mkoa wa Arusha, wamesema wanaishitaki mahakama hiyo kutokana na kutowalipwa stahiki zao ambazo zinahusisha Likizo na nyongeza ya mishahara kulingana na mikataba yao.
Wafanyakazi hao wanaidai mahakama hiyo jumla ya dola za kimarekani, 800,000, ambazo hawajalipwa hadi leo ambapo mahakama hiyo ya Umoja wa mataifa ambayo imedumu kwa kipindi cha miaka 21 ilifunguliwa mjini Arusha mwaka 1994 nayo imemaliza kazi yake mwezi uliopita.
Wafanyakazi hao ambao waliajiriwa na Mahakama hiyo mwaka 1998 walikuwa wakihudumia wafungwa na mabusu wa mahakama hiyo iliyopo kwenye gereza kuu la Arusha .
Wamesema walipoaanza kudai na kufuatilia stahiki zao ndipo walipopewa barua za kuachishwa waliachishwa kazi Septemba 30 mwaka huu .
Wamesema mara baada ya kupewa barua zao hawakutakiwa tena kufika ofisi za Mahakama hiyo zilizokuwa jengo la mikutano ya kimataifa AICC na ndipo walipofika Idara ya Kazi mkoa kwa ajili ya kufungua shauri la madai yao.
Ofisi hiyo ya Kazi iliandikia mahakama hiyo barua ya kutaka kufahamu stahiki za wafanyakazi hao lakini mahakama hiyo haikujibu mpaka leo.
Wafanyakazi hao wamewasiliana na kituo cha haki za binadamu , LHRC, mjini Arusha ambapo kimewapatia msaada wa sheria ili kudai stahiki zao.
Akizungumza Wakili wa kituo cha haki za binadamu, Shirinde Ngalule, amesema Umoja wa mataifa una kinga ya kutokushitakiwa katika taasisi yeyote ile ikiwemo mahakamani.
Lakini kwa mjibu wa mkataba wa kuanzishwa kwa mahakama hiyo hapa nchini Mahakama hiyo inatakiwa kuendesha shughuli zake kwa kuzingatia sheria za nchi husika zikiwemo sheria ya mahusiano ya kazi.
Amesema kwa msingi huo mahakama hiyo inapaswa kuheshimu sheria na haki za binadamu, badala ya kwanyanyapaa waliokuwa watumishi wake kwa kisingizio cha cha kuwa na kinga ya kutokushitakiwa.
Amesema mahakama hiyo imekiuka taratibu katika kuwaachisha watumishi hao ambao taratibu hazikufuatwa ikiwemo kupewa notisi na badakla yake walipewa barua ya kuachishwa kazi kitendo ambacho ni kinyume na haki za binadamu.
Ameongeza kuwa chanzo ni pale walipoanza kudai mkataba wa kazi ndipo walipoaanza kufukuzwa mmoja mmoja
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni