Na Frank Geofray wa Jeshi la Polisi.
Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini 
IGP Ernest Mangu amewataka Makamanda wa Polisi kote nchini kuendesha 
oparesheni kali ya kuwachukulia hatua kali za kisheria waendesha 
pikipiki maarufu kama bodaboda wasiotii sheria za usalama barabarani 
ikiwemo kubeba abiria zaidi ya mmoja, kupita katika taa nyekundu pamoja 
na kutovaa kofia ngumu.
IGP Mangu alitoa kauli hiyo 
wakati akizungumza na Maafisa wakuu wa Polisi wakiwemo Makamanda wa 
Polisi wa mikoa, vikosi na makao makuu katika kikao kazi kilichokuwa 
kikifanyika jijini Dar es Salaam ambacho kilifunguliwa na Waziri wa 
Mambo ya Ndani ya nchi.
Alisema waendesha bodaboda 
wamekuwa wakikaidi kufuata sheria za usalama barabarani lakini sasa 
mwisho wao umefika na kuwataka makamanda wa polisi wa mikoa kote nchini 
kutekeleza maelekezo hayo ili kuleta nidhamu kwa bodaboda katika kufuata
 sheria za usalama barabarani.
IGP Mangu alisema suala la 
kufuata sheria za usalama barabarani kwa bodaboda halina mjadala na kila
 kamanda ahakikishe kuwa wale wote wasiofuata sheria na kukaidi 
wanakamatwa bila kuoneana muhali kwakuwa wamekuwa wakisababisha ajali 
zinazoweza kuzuilika.
“ Pamoja na kuendelea kudhibiti
 uhalifu wa aina zote, natoa maelekezo  kwa kila mkoa kuhakikisha 
 unaendesha oparesheni kali  dhidi ya bodaboda ili kupunguza ajali 
zinazosababishwa na bodaboda ambao wengi wao hawataki kufuata sheria na 
kanuni za usalama barabarani, tusiwaonee muhali maana maisha ya watu ni 
muhimu sana na jambo la msingi ni kusimamia sheria tu” Alisema IGP 
Mangu. 
Awali akifungua kikao
 kazi hicho Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mh. Charles Kitwanga 
alilitaka Jeshi la Polisi kuendelea na mapambano yake dhidi ya uhalifu 
na wahalifu ili usalama wa raia na mali zao uendelee kuimarika na 
watanzania waendelee na shughuli zao za kujiletea maendeleo bila hofu ya
 kutendewa uhalifu.  
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni