IGP ATANGAZA OPERESHENI KALI DHIDI YA BODABODA.

IG
Na Frank Geofray wa Jeshi la Polisi.
Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Ernest Mangu amewataka Makamanda wa Polisi kote nchini kuendesha oparesheni kali ya kuwachukulia hatua kali za kisheria waendesha pikipiki maarufu kama bodaboda wasiotii sheria za usalama barabarani ikiwemo kubeba abiria zaidi ya mmoja, kupita katika taa nyekundu pamoja na kutovaa kofia ngumu.
IGP Mangu alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na Maafisa wakuu wa Polisi wakiwemo Makamanda wa Polisi wa mikoa, vikosi na makao makuu katika kikao kazi kilichokuwa kikifanyika jijini Dar es Salaam ambacho kilifunguliwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi.
Alisema waendesha bodaboda wamekuwa wakikaidi kufuata sheria za usalama barabarani lakini sasa mwisho wao umefika na kuwataka makamanda wa polisi wa mikoa kote nchini kutekeleza maelekezo hayo ili kuleta nidhamu kwa bodaboda katika kufuata sheria za usalama barabarani.
IGP Mangu alisema suala la kufuata sheria za usalama barabarani kwa bodaboda halina mjadala na kila kamanda ahakikishe kuwa wale wote wasiofuata sheria na kukaidi wanakamatwa bila kuoneana muhali kwakuwa wamekuwa wakisababisha ajali zinazoweza kuzuilika.
“ Pamoja na kuendelea kudhibiti uhalifu wa aina zote, natoa maelekezo  kwa kila mkoa kuhakikisha  unaendesha oparesheni kali  dhidi ya bodaboda ili kupunguza ajali zinazosababishwa na bodaboda ambao wengi wao hawataki kufuata sheria na kanuni za usalama barabarani, tusiwaonee muhali maana maisha ya watu ni muhimu sana na jambo la msingi ni kusimamia sheria tu” Alisema IGP Mangu. 
Awali akifungua kikao kazi hicho Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mh. Charles Kitwanga alilitaka Jeshi la Polisi kuendelea na mapambano yake dhidi ya uhalifu na wahalifu ili usalama wa raia na mali zao uendelee kuimarika na watanzania waendelee na shughuli zao za kujiletea maendeleo bila hofu ya kutendewa uhalifu. 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni