Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo 
Vikuu Tanzania Prof Yunus Mgaya akizungumza na waandishi wa habari 
(hawapo pichani) Kuhusu uamuzi wa Tume kufuta usajili wa vyuo vikuu 
vishiriki vya Mtakatifu Joseph tawi la Songea. Picha na Raymond 
Mushumbusi MAELEZO
……………………………………………………………………………………..
Na Nyakongo Manyama MAELEZO
Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU)
 imeamua kufuta kibali kilichoanzisha vyuo vikuu viwili vishiriki vya 
Mtakatifu Joseph ambavyo ni Chuo Kikuu kishiriki cha Sayansi ya Kilimo 
na Teknolojia (SJUCAST) na Chuo Kikuu kishiriki cha Teknolojia ya Habari
 na Mawasiliano (SJUIT) vilivyopo Songea.
Akizungumza na waandishi wa habari leo katika ofisi za Tume hiyo, Katibu Mtendaji wa Tume
 ya Vyuo Vikuu Tanzania Prof Yunus Mgaya amesema kutokana na mapungufu 
yaliyobainishwa na Tume ambayo ni matatizo ya ubora wa elimu na 
ukiukwaji wa Sheria za uendeshaji wa Chuo Kikuu kama ulivyobainishwa na 
Sheria ya Vyuo Vikuu hii  imepelekea Tume kuchukua hatua ya kufuta 
usajili wa vyuo hivyo.
“ kutokana na yaliyobainishwa 
hapo awali tunapenda kutaarifu umma kwamba ,Tume imejiridhisha kuwa hivi
 vyuo vikuu vishiriki viwili havitoi elimu ya Chuo kikuu ya viwango 
stahiki na ukizingatia wanafunzi katika Vyuo hivi ndio waathirika 
wakubwa wa matatizo yaliyopo”Alisema Prof Mgaya.
“Napenda kufafanua kwamba Vyuo 
vikuu vishiriki tuliyovifutia usajili ni tawi la Songea na Vyuo vingine 
vishiriki vya Mtakatifu Joseph vilivyopo Dar es Salaam na Arusha 
vitaendelea kufanya kazi kama kawaida”Alisema Prof Mgaya.
Prof Yunus Mgaya amesema 
wanafunzi wote wanaosoma katika vyuo vishiriki vilivyofutwa usajili 
wanaarifiwa kuwa watahamishiwa kwenye vyuo vikuu vingine vinavyofundisha
 programu za masomo zinazofanana na masomo wanayosoma hivi sasa chini ya
 utaratibu uliopangwa.
Amevitaja vyuo ambavyo 
watapelekwa wanafunzi walipo katika vyuo vishiriki vilivyofutwa usajili 
kuwa ni Chuo Kikuu cha kilimo Sokoine (SUA), Chuo Kikuu cha Dodoma 
(UDOM),Chuo Kikuu cha  Kikatoliki cha Mwenge(MWECAU) na Chuo Kikuu cha 
Kikatoliki cha Ruaha(RUCU).
Amesisitiza kuwa orodha ya 
majina ya wanafunzi na vyuo watavyohamishiwa yatawekwa kwenye tovuti ya 
Tume hivi karibuni na wale wote wanaonufaika na Mikopo toka Bodi ya 
Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu, mikopo yao itahamishiwa katika vyuo
 watakavyokuwa wamehamishiwa.
Vyuo vikuu vyote chini 
vinakumbushwa kufata Sheria na kuzingatia utoaji wa elimu inayokidhi 
viwango vya ubora vinavyokubalika kitaifa na kimataifa, hivyo Tume 
haitasita kuchukua hatua stahiki kwa chuo kikuu chochote 
kitakachobainika kutoa elimu isiyokidhi viwango vya ubora kwa kisingizio
 cha aina yoyote.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni